2014-02-15 15:31:26

Upendo wa daima hadi kifo kitakapowatenganisha!


Katika Maadhimisho ya Siku ya wapendanao kama njia ya kumuenzi Mtakatifu Valentino, Askofu na msimamizi wa wapendanao, aliyefariki dunia hapo tarehe 14 Februari mjini Roma kunako karne ya nne, wanandoa watarajiwa thelathini elfu walimiminika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro ili kumzunguka Baba Mtakatifu Francisko.

Mkutano wa wapendanao ni sehemu ya maandalizi ya Sinodi maalum ya Maaskofu Katoliki kuhusu Familia itakayofanyika mwezi oktoba hapa mjini Vatican. Wanandoa watarajiwa walipenda kukutana na kusali pamoja na Baba Mtakatifu Francisko aweze kubariki upendo wao, ili siku watakapofunga Sakramenti ya Ndoa, upendo wao udumu hadi watu washangae!

Hili ni kundi la Waamini linalotaka kuendeleza kazi ya uumbaji na malezi kwa watoto ambayo Mwenyezi Mungu amemkabidhi mwanadamu katika hija yake ya maisha ya hapa duniani, kwa kumuumba mwanaume na mwanamke ili waweze kutegemezana. Ni kundi linalotaka kujenga na kuimarisha misingi ya ndoa kadiri ya mpango wa Mungu na wala si katika hali ya kujisikia na vionjo vya kibinadamu, mambo ambayo kimsingi ni mambo mpito!

Ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Familia wakati alipokuwa anamkaribisha Baba Mtakatifu Francisko ili aweze kujibu maswali na duku duku za wanandoa watarajiwa waliokuwa wamefurika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Kanisa limewakumbuka wanandoa watarajiwa pamoja na watoto wanaokumbana na nyanyaso, vitisho na dhuluma, kwani haya ni mambo ambayo kamwe hayawezi kukubalika yaendelee bila kushughulikiwa kikamilifu.

Askofu mkuu Vincenzo Paglia anasema, wanandoa watarajiwa wametoka katika nchi thelathini, ongezeko kubwa kupita hata yale matarajio na idadi iliyokuwa imetolewa na Baraza la Kipapa la Familia siku chache zilizopita. Wanandoa hawa wanapenda kwa pamoja katika maisha ya ndoa na familia waweze kushirikiana ili kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika maisha.

Ni dhamana na jukumu la wanasiasa na watunga sera kuhakikisha kwamba, wanazisaidia familia kutekeleza dhamana na wajibu wake katika Jamii na Kanisa kwa ujumla. Kwa vijana wanaothubutu kujenga na kuimarisha msingi bora wa maisha ya kifamilia tangu ujana wao, hawa wanakuwa ni utajiri mkubwa kwa Jamii husika! Wanandoa watarajiwa wamekumbushwa kumualika Yesu katika maisha ya ndoa yao!

Baba Mtakatifu Francisko akijibu maswali ya wanandoa watarajiwa amewataka wajikite katika upendo dumifu hadi kifo kitakapowatenganisha na hivyo kukataa katu katu upendo mpito! Amewataka wajitahidi kumwilisha ndani mwao tunu msingi za maisha na mtindo wa ndoa ya Kikristo: kwa kuombana na kusameheana; kwa kushukuru! Haya ni mambo msingi yanayorutubisha udumifu wa maisha ya ndoa na familia.

Baba Mtakatifu amewataka wanandoa watarajiwa kuzingatia mambo msingi katika maadhimisho ya Sakramenti ya Ndoa, ili kuweza kufurahia siku hii muhimu katika maisha yao!







All the contents on this site are copyrighted ©.