2014-02-15 15:11:13

Baraza la Maaskofu Katoliki Italia ni daraja kati ya Serikali na Vatican


Kanisa na Serikali vinaweza kushirikiana kwa karibu katika masuala ya uchumi bila ya kinzani wala kutazamana kwa "macho ya makengeza". Ili kufanikisha mchakato huu, kuna haja kwa Kanisa kuwa na sera na mikakati sahihi ya kiuchumi inayopania pamoja na mambo mengine kuhakikisha kwamba, inaboresha maisha ya watu: kiroho na kimwili. Mshikamano wa upendo unaoongozwa na kanuni auni ni muhimu sana kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watu sehemu mbali mbali za dunia.

Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican pamoja na Sheria za Kanisa za Mwaka 1984 zimeweka vipaumbele vya ushirikiano wenye tija na mashiko kati ya Serikali na Kanisa Katoliki kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi. Utekelezaji wa sheria na Mafundisho ya Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican unafanywa na Mabaraza ya Maaskofu Katoliki katika nchi husika, kwa kuongozwa na kanuni auni; mambo msingi katika Mafundisho Jamii ya Kanisa.

Askofu Nunzio Galantino, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia akichangia mada kwenye Kongamano la Siku moja kuhusu Maadhimisho ya Miaka thelathini tangu Serikali ya Italia na Vatican walipofanya marekebisha msingi katika Muafaka wa Laterano anasema kwamba, utekelezaji wake kimsingi unafanywa na Baraza la Maaskofu Katoliki Italia. Kumekuwepo na ushirikiano wa karibu kati ya Serikali ya Italia na Kanisa Katoliki kuhusiana na masuala ya fedha na uchumi.

Sehemu ya kodi inayotolewa na wananchi wa Italia inatumika kwa ajili ya kugharimia maisha na utume wa Kanisa ndani na nje ya Italia. Serikali pia imeanzisha mfumo kwa ajili ya kutoa ruzuku kwa Mapadre wanaowahudumia wananchi wa Italia: kiroho na kimwili.

Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linawajibika kutoa taarifa ya mapato na matumizi ya fedha za walipa kodi nchini Italia kwa serikali, jambo linaloonesha uwajibikaji wa pamoja kwa ajili ya mafao ya wengi.

Askofu Nunzio Galantino, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia anasema, kimsingi Baraza la Maaskofu Katoliki Italia ndilo daraja kuu kati ya Serikali ya Italia na Vatican katika utekelezaji wa Muafaka wa Laterano unaoadhimisha Miaka thelathini tangu ulipofanyiwa marekebisho.







All the contents on this site are copyrighted ©.