2014-02-13 15:00:21

Licha ya madhulumu na nyanyaso za kidini wakati wa Ukomunisti, lakini Kanisa nchini Bulgaria kuwa kielelezo cha ushuhuda wa imani na mapendo


Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi, tarehe 13 Februari 2014 amekutana na kuzungumza na Maaskofu Katoliki Bulgaria ambao wako mjini Vatican katika hija ya kitume inayofanyika walau kila baada ya miaka mitano. Amewapongeza kwa ushuhuda wa imani na mapendo unaooneshwa na Wakristo nchini Bulgaria.

Papa amewapongeza pia kwa Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 150 ya uhusiano kati ya Bulgaria na Vatican, yaliyofanyika kunako mwaka 2010; Kumbu kumbu ya Miaka 60 tangu Mwenyeheri Evgenij Bossilkov alipouwawa kikatili pamoja na Maadhimisho mbali mbali sanjari na Mwaka wa Imani. Maadhimisho yote haya yanaonesha ushuhuda wa tunu msingi za maisha ya kimaadili na Kikristo, licha ya madhara makubwa yaliyosababishwa na nyanyaso za kidini kutokana na utawala wa Kikomunisti.

Changamoto iliyoko mbele yao kwa sasa ni kujikita katika mchakato wa maisha ya kimissionari unaofanyiwa kazi na Mama Kanisa kwa wakati huu, kwa kutambua kwamba, kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, Wakristo wote wanatumwa kutangaza Injili kwa furaha na kwa moyo mkuu pamoja na kuthamini Ibada mbali mbali zinazofanywa na waamini, bila kusahau kumwilisha Mafundisho Jamii ya Kanisa katika maisha na vipaumbele vya waamini; kwa kupambana na baa la umaskini, daima wakisimama kidete kulinda na kutetea mafao ya wengi, haki na amani. Kanisa litaendelea kuchangia katika ustawi na mafao ya wengi nchini Bulgaria, kwa kuheshimu uhuru wa kidini.

Baba Mtakatifu Francisko anawataka Maaskofu Katoliki Bulgaria kujikita katika majiundo endelevu kwa waamini walei kwa njia ya Katekesi, utume miongoni mwa vijana pamoja na kulea na kukuza miito mitakatifu ndani ya Kanisa, kama kielelezo cha ukomavu wa imani na changamoto ya kimissionari. Maaskofu waendeleze mchakato wa majadiliano ya Kiekumene na Kanisa la Kiorthodox; kwa kusali na kutafakari kwa pamoja Neno la Mungu, ili siku moja waweze kuadhimisha kwa pamoja Fumbo la Ekaristi Takatifu, kielelezo cha umoja kamili kati ya Wakristo.

Baba Mtakatifu Francisko amewapongeza waamini kutoka Bulgaria wanaotarajia kushiriki kwa wingi katika Ibada ya kuwatangaza watakatifu Mwenyeheri Yohane wa XXIII na Yohane Paulo II hapo tarehe 27 Aprili 2014. Hawa ni watu walioacha chapa ya kudumu katika maisha na utume wa Kanisa nchini Bulgaria; wakaacha taa ya imani inayoendelea kuwaka hadi leo hii.







All the contents on this site are copyrighted ©.