Kampeni dhidi ya ujangiri kwenye mbuga za wanyama Tanzania
Ifuatayo ni hotuba ya Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania katika uzinduzi wa mabango ya
kampeni ya kupinga mauaji ya Tembo na Faru, iliyofanyika tarehe 11 Februari 2014 kwenye
Uwanja wa Kimataifa wa Mwalimu J. K. Nyerere.
Nakushukuru sana Naibu Waziri
kwa kunishirikisha kwenye tukio hili kubwa na la kihistoria la kuhamasisha wananchi
kupinga mauaji ya tembo na faru kupitia ujumbe kwenye mabango. Nawapongeza sana kwa
ubunifu huu wa aina yake. Dunia hivi sasa inakabiliwa na wimbi kubwa la ujangili
wa wanyama pori hususan ndovu na faru. Nchi nyingi zenye wanyama hao zimekuwa zinakabiliwa
na tatizo hilo. Nchi yetu ni moja ya nchi zinazokabiliwa na tatizo hili.
Ndugu
wananchi; Takwimu za hivi karibuni zilizotokana na Sensa iliyofanywa na serikali
kwa msaada wa Shirika linalojishughulisha na Uhifadhi la Ujerumani (Frankfurt Zoological
Society) katika mfumo wa ikolojia wa Selous-Mikumi pekee zimeonesha kuwa mwaka 2009,
katika mfumo wa ikolojia hiyo kulikuwa na tembo wapatao 38,975 na kwa sasa idadi hiyo
imeporomoka na kubaki tembo wapatao 13,084.
Takwimu hizi zinamaanisha kuwa
idadi ya tembo katika mfumo huo imepungua kwa asilimia 66, hali inayoashiria kuwa
kuna kila dalili za mnyama huyu kutoweka katika kipindi kifupi kijacho kama jitihada
za makusudi za kuwalinda hazitafanyika.
Katika jitihada za kukabiliana
na hali hiyo, Serikali imechukua na inaendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kutunga
sheria kali za uhifadhi wa wanyama pori; kuimarisha doria katika hifadhi za wanyama
pori na kuendesha opersheni maalum kutokomeza ujangili. Tuliwahi kufanya Operesheni
Uhai mwaka 1987 baada ya hali ya ujangili kuwa mbaya sana. Operesheni hiyo ilihusisha
jeshi na ilifanikiwa sana kumaliza tatizo la ujangili. Na kwa kweli na idadi ya tembo
ikaongezeka kutoka 55,000 mwaka 1989 mpaka 110,000 mwaka 2009.
Mabibi na Mabwana; Mwaka
jana Serikali iliamua kuendesha Operesheni maalum iliyojulikana kama Operesheni Tokomeza
baada ya kuona hali ya ujangili inazidi kuwa mbaya. Hata hivyo, kutokana na kasoro
zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wake, Serikali iliamua kuisitisha kwa muda operesheni
hiyo ili kufanya marekebisho. Sasa tunajipanga kuanza awamu ya pili ya operesheni
hiyo. Hatuwezi kuacha, ama sivyo tembo na faru wataisha wote.
Pamoja na kwamba
Serikali ina nia thabiti na inafanya kila linalowezekana kutokomeza ujangili, bado
tunakabiliwa na changamoto kubwa na ndogo zinazofanya tusifikie hapo tunapopataka.
Kwanza ni ule ukweli kwamba eneo linalotakiwa kufanyiwa doria ni kubwa mno. Lina
ukubwa wa kilometa za mraba 232,535 pungufu kidogo ya eneo lote la Uingereza. Kwa
bahati mbaya hatuna askari wa wanyamapori wa kutosha na vitendea kazi kama vile magari
ya doria, vifaa vya kuonea usiku au teknolojia ya kisasa ya kusaidia kufanya doria.
Tutafanya kila tuwezalo kupunguza uhaba huo.
Changamoto kubwa kuliko zote ni
kuwepo kwa soko kubwa la pembe za ndovu na faru duniani. Ni makusudio yetu kuomba
dunia kupiga marufuku biashara ya pembe hizo. Biashara hiyo ikikomeshwa hakuna tembo
atakayeuawa. Kichocheo cha ujangili hakitakuwepo.
Ufumbuzi wake unahitaji
nguvu ya Jumuiya ya Kimataifa. Hatuwezi peke yetu. Wapo marafiki zetu wanaosaidia
jitihada zetu, lakini bado tunahitaji zaidi. Tunahitaji msaada wa kiufundi, fedha
na teknolojia ili watu wetu wapate mafunzo bora, ili tuajiri askari wa wanyama pori
wengi zaidi na tuwe na teknolojia ya kisasa kukabiliana na ujangili.
Suala
la soko pia linahitaji msukumo mpya kutoka kwa Jumuiya ya Kimataifa. Inatakiwa tukubaliane
wote kupiga marufuku biashara ya ndovu na pembe za faru au bidhaa zinazotokana nazo.
Bahati nzuri usiku huu naenda Uingereza kushiriki kwenye mkutano utaozungumzia masuala
ya ujangili na biashara haramu ya bidhaa za wanyamapori. Kwa kutambua jitihada zetu
na changamoto zinazotukabili, nimepewa nafasi ya kuzungumza katika mkutano huo.
Itakuwa
nafasi nzuri kuwaeleza washirika wetu namna tunavyoweza kushirikiana. Nadhani na
wao watakuwa tayari kufanya hivyo kwa sababu magenge yanayofanya biashara hii ni hatari
kwa usalama wa dunia. Imethibitika baadhi yao wanasaidia vikundi vya kigaidi.
Navyosema
hivyo sina maana kuwa wananchi hususan wanaozunguka maeneo ya hifadhi hawana nafasi.
Wanayo nafasi na naomba nikiri kuwa ushirikishwaji wa wananchi katika uhifadhi wa
wanyamapori kwa wakati huu ni wa muhimu sana. Wao ndiyo wanafahamu majangili na wasafirishaji
wa ndovu na pembe za faru. Hivyo wananchi wakielimishwa vizuri na kushirikishwa kwenye
vita hii naamini tutashinda. Hivyo, naomba wananchi wote tukubaliane kwa kauli moja
kuwa tukishirikiana tunaweza kushinda.
Tunakubaliana na kauli mbiu yetu ya
“ACHA KUUA TEMBO NA FARU - BUNDUKI NA ASKARI PEKEYAO HAWAWEZI KUOKOA MAISHA YA TEMBO
NA FARU. TUUNGANE NA SERIKALI KATIKA MAPAMBANO YA KUOKOA WANYAMA HAWA”
Mabadiliko
ni mimi na wewe. Naomba tushirikiane kifichua majangili na kulinda wanyamapori kwa
faida ya sasa na vizazi vijavyo. Tanzania bila ujangili inawezekana. Ahsanteni sana
na nawashukuru sana kwa kunisikiliza.