2014-02-11 08:52:53

Miaka 85 ya Muafaka kati ya Italia na Vatican


Serikali ya Italia na Vatican kwa pamoja zinafanya kumbu kumbu ya Miaka 85 tangu nchini hizi mbili zilipowekeana sahihi katika Muafaka wa Laterano na kufanyiwa marekebisho ya msingi mintarafu Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na Sheria Mpya za Kanisa kunako tarehe 18 Februari 1984, miaka thelathini iliyopita.

Muafaka huu umezingatia maisha na utume wa Kanisa mintarafu mabadiliko ya kisiasa, kijamii, kiuchumi na kitamaduni nchini Italia. Muafaka huu umekuwa ni Waraka rejea wa mahusiano kati ya Vatican na nnchi mbali mbali duniani.

Muafaka unakubaliana kimsingi kwamba, Kanisa halichangamani katu na Jumuiya ya kisiasa, wala haifungamani na mtindo wowote wa mfumo wa kisiasa kwa sababu ya majukumu na uhalali wake. Serikali na Kanisa zina uhuru na mamlaka kila mmoja katika uwanja wake, zote mbili zipo kwa ajili ya kumtumikia mwanadamu. Serikali ya Italia inalitambua Kanisa Katoliki katika utekelezaji wa maisha na utume wake kwa uhuru kamili bila ya kuingiliwa katika shughuli za kichungaji, elimu, matendo ya huruma, ibada na katika dhamana yake ya kuwatakatifuza watu wa Mungu.

Muafaka huu umeliwezesha Kanisa Katoliki nchini Italia kuwa karibu na wananchi katika shida, mahangaiko, furaha na matumaini yao, kwa kuendelea kuhimiza misingi ya maadili na utu wema, mambo msingi katika kukuza na kudumisha demokrasia ya kweli. Kanisa limeendelea kuchagia katika ustawi na maendeleo ya wengi nchini Italia katika medani mbali mbali za maisha kwa kutumia utajiri mkubwa unaofumbatwa katika Mashirika mbali mbali ya kitawa na kazi za kitume. Kimsingi muafaka huu ni kwa ajili ya maendeleo ya mtu mzima na mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.