2014-02-10 08:56:35

Changamoto inayofanyiwa kazi na Sekretarieti ya Vatican katika maisha na utume wa Kanisa!


Sekretarieti ya Vatican inapaswa kuwa mstari wa mbele katika mchakato wa kuleta mageuzi katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kuendelea kushirikiana kwa karibu zaidi na Baba Mtakatifu Francisko. Huu unapaswa kuwa ni mwanzo mpya baada ya kipindi cha kashfa iliyoikumba Vatican kwa baadhi ya wafanyakazi wake wasiokuwa waaminifu kuvujisha nyaraka za siri kutoka Vatican kwa mafao yao binafsi. Ni muda wa kujikita zaidi na zaidi katika uhusiano wa kidplomasia katika kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; haki na amani pamoja na mafao ya wengi.

Ni maneno ya Kardinali mteule Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican katika mahojiano maalum na Gazeti la "Avvenire" linalomilikiwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Italia. Changamoto kubwa iliyoko mbele ya Kanisa kwa sasa ni toba na wongofu wa ndani; upendo na mshikamano wa dhati unaosimikwa katika msingi wa kanuni auni kwa ajili ya kudumisha mshikamano wa kidugu kati ya watu, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa ajili ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Kutokana na changamoto hii anasema Kardinali mteule Parolin, kuna haja kwa Sekretarieti ya Vatican kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa la kiulimwengu kwa kuondokana na urasimu usiokuwa na tija wala mashiko; kwa kujikita katika huduma kwa Kanisa katika ujenzi na uimarishaji wa umoja na utume wa Kanisa sehemu mbali mbali za dunia. Hiki kinapaswa kuwa ni chombo cha kumsaidia Baba Mtakatifu na Maaskofu mahalia katika utekelezaji wa dhamana na majukumu yao.

Mabadiliko ya miundo mbinu ndani ya Vatican hayana budi kusindikizwa na toba pamoja na wongofu wa ndani. Licha ya mapungufu ya kibinadamu yanayoweza kujionesha katika Sekretarieti ya Vatican, lakini bado kuna umati mkubwa wa watakatifu wanaojitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo.

Baba Mtakatifu anaendelea kuwahimiza wafanyakazi wa Vatican kutekeleza wajibu wao kama binadamu, wakionesha upendo na ukarimu pamoja na kushiriki katika dhamana ya utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu.

Wizi wa nyaraka za siri kutoka Vatican ni kati ya mambo ambayo yamemsikitisha na kumhuzunisha sana Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Hii ni kashfa ambayo imewachafulia watu wengi sifa zao njema, changamoto kwa wahusika wakuu kuendelea kujiuliza ukweli na uaminifu wao kwa Injili ya Kristo.

Kardinali mteule Parolin anasema, Benki ya Vatican bado ina umuhimu wake katika maisha na utume wa Kanisa; jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, inatekeleza dhamana yake kwa kuzingatia misingi ya Injili, maadili, ukweli na uwazi. Kanisa litaendelea kuwa mstari wa mbele katika kulinda na kutetea misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano kati ya mataifa na kwamba, Jumuiya ya Kimataifa ina kiu ya amani ya kudumu huko Syria na sehemu nyingine ambako mtutu wa bunduki bado unaendelea kusababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao.

Vatican itaendelea kujenga na kuimarisha uhusiano wake wa kidiplomasia na China kwa njia ya majadiliano katika ukweli na uwazi na wanasiasa nchini humo. Mwelekeo wa Baba Mtakatifu Francisko katika masuala ya uchumi na maendeleo unajikita zaidi katika misingi ya maadili; upendo na mshikamano wa kidugu katika kupambana na baa la umaskini, njaa na maradhi sehemu mbali mbali za dunia, kwa watu kujali na kuguswa na mahangaiko ya jirani zao. Hii inatokana na ukweli kwamba, pengo kati ya maskini na matajiri linaendelea kuongezeka maradufu. Vatican itaendelea kushirikiana na Makanisa mahalia pamoja na wadau mbali mbali kwa ajili ya kutafuta mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.