2014-02-07 10:36:16

Majadiliano ya kidini yanapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza ili kujenga misingi ya haki, amani na utulivu katika Jamii


Baraza la Maaskofu Katoliki India linaendelea na mkutano wake wa thelathini na moja wa kawaida uliofunguliwa hapo tarehe 5 Februari na unatarajiwa kuhitimishwa tarehe 12 Februari 2014. Askofu mkuu Salvatore Pennacchio, Balozi wa Vatican nchini India amelitaka Kanisa kujikita zaidi na zaidi katika mchakato wa majadiliano ya kidini nchini India pamoja na kuhakikisha kwamba, waamini wanapata huduma makini za kichungaji kutoka kwa Maaskofu wao mahalia.

Kama sehemu ya Unjilishaji Mpya Kanisa halina budi kuendeleza majadiliano ya kidini na kiekumene ili kujenga na kuimarisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa miongoni mwa watu wa dini na imani mbali mbali nchini India. Katika mikakati yake ya kichungaji, Kanisa linapaswa kwanza kabisa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili wao pia waweze kuonja na kufarijika kwa Injili ya Furaha inayomwilishwa katika imani tendaji.

Kanisa bado linahamasishwa kuendelea kujichotea utajiri unaofumbatwa katika Mafundisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican katika maisha na utume wake! Mkutano huu unahudhuriwa na Maaskofu 200 kutoka katika Majimbo 167 yanayounda Kanisa Katoliki nchini India. Maaskofu pamoja na mambo mengine wanajadili kuhusu uchaguzi mkuu nchini India unaotarajiwa kufanyika kati ya Mwezi Aprili na Juni 2014.







All the contents on this site are copyrighted ©.