2014-02-05 08:06:55

Wanafunzi wa vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu wanayo dhamana ya kujenga na kukuza majadiliano ili kudumisha haki, amani na upendo kati ya watu!


Chuo Kikuu cha Notre Dame chenye tawi lake mjini Roma, hivi karibuni kiliwatunukia Udaktari wa heshima Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini pamoja na Mama Maria Voce, Rais wa Chama cha Kitume cha Wafokolari kutokana na mchango wao makini katika kudumisha majadiliano ya kidini miongoni mwa watu wa Jumuiya ya Kimataifa.

Hili lilikuwa ni tukio la furaha na heshima kubwa kwa Jumuiya ya Chuo Kikuu cha Notre Dame kumtunukia pia udaktari wa heshima Padre John Jenkins, CSC, Rais wa Chuo Kikuu cha Notre Dame kutokana na mchango wake katika sekta ya elimu. Watunukiwa wote walizungumzia kuhusu mchango wa Vyuo Vikuu vya Kikatoliki pamoja na Taasisi za Elimu ya Juu zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki sehemu mbali mbali za dunia, katika kujenga na kudumisha majadiliano ya kitamaduni, kiimani na kiakili.

Wanafunzi wa vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu daima wako kwenye mchakato wa majadiliano ya kidini, unaopania kujenga na kudumisha haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati kati ya watu wa mataifa anasema Kardinali Jean Louis Tauran.

Kwa upande wake, Mama Maria Voce, Rais wa Shirika la kitume la Wafokolari amekazia umuhimu wa Jumuiya za Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu kujikita katika fadhila ya upendo na maisha; mambo msingi yanayobubujika kutoka katika tunu msingi za Kiinjili.

Tafakari ya kina ya Neno la Mungu inaweza kuwajengea wanafunzi uwezo wa kufahamu na kuimwilisha sheria ya upendo kwa Mungu na binadamu katika kudumisha mahusiano mema kati ya watu. Ni katika Injili ya Upendo kwa Mungu na Jirani, watu wanaweza kugundua ile furaha ya kuwa ni wadau katika ujenzi wa ulimwengu unaosimikwa katika misingi ya haki, upendo, amani na udugu.

Chuo Kikuu cha Notre Dame tawi la Roma linatoa huduma ya elimu kwa wale wanaotaka kujiendeleza zaidi kwa kupata fursa ya masomo nje ya Italia. Ni mahali pa kukuza na kuendeleza shughuli za elimu na utamaduni kutoka mjini Roma.







All the contents on this site are copyrighted ©.