2014-02-04 08:51:02

Ndoa na Familia ni kati ya vipaumbele vya kichungaji vya Askofu mkuu Ramaroson!


Tunu msingi za maisha ya ndoa na familia pamoja na majiundo makini ni kati ya vipaumbele vya kichungaji vinavyofanyiwa kazi na Askofu mkuu Benjamin Marc Ramaroson wa Jimbo kuu la Antsiranana, nchini Madagascar. Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu Ramaroson aliteuliwa hivi karibuni kuwa Askofu mkuu na Baba Mtakatifu Francisko na kusimikwa rasmi hapo tarehe 25 Januari 2014, Mama Kanisa alipokuwa anaadhimisha Siku kuu ya Kuongoka kwa Mtakatifu Paulo, Mwalimu na Mtume wa Mataifa.

Anasema, kati ya vipaumbele vyake vya kwanza ni majiundo makini ya tunu msingi za maisha ya ndoa na familia pamoja na kutoa majiundo endelevu kwa vijana ili waweze kutambua dhamana na nafasi yao katika maisha na utume wa Kanisa, tayari kumshuhudia Kristo na Kanisa lake kwa watu wanaokutana nao katika medani mbali mbali za maisha na kwa njia hii, wawe tayari kushuhudia Injili ya Furaha. Familia na Vijana ni kati ya makundi yanayoathirika vibaya kutokana na kinzani mbali mbali za kisiasa na kijamii nchini Madagascar.

Kumong'onyoka kwa tunu msingi za maisha ya kiutu na kimaadili ni changamoto kubwa kwa Wakristo na watu wenye mapenzi mema katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Kuna haja kwa Wakristo kuhakikisha kwamba, wanayatakatifuza malimwengu kwa njia ya utakatifu wa maisha yanayobubujika kutoka katika tunu msingi za Kiinjili; ili watu waonje Injili ya Furaha inayoendelea kutangazwa na Wakristo katika Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Waamini waendelee kutumia vyema karama na neema walizokirimiwa wakati wa Ubatizo na Kipaimara; waoneshe ari, mwamko wa kimissionari na huduma ya mapendo kwa jirani kama kielelezo cha imani katika matendo! Hii ni changamoto endelevu katika maisha na utume wa waamini hata baada ya kuhitimisha Maadhimisho ya Mwaka wa Imani.

Madagascar kwa sasa inahitaji kuanzisha mchakato wa maendeleo endelevu yanayojikita katika elimu makini kuhusu haki na amani; upatanisho na upendo kwa Mungu na jirani hasa kufuatia kinzani na migogoro ya kisiasa iliyojitokeza nchini humo kama sehemu ya mchakato wa utekelezaji wa demokrasia miongoni mwa wananchi.







All the contents on this site are copyrighted ©.