2014-02-04 10:52:48

Kuna ukata wa rasilimali fedha ili kukabiliana na uhaba wa chakula duniani!


Shirika la Mpango wa Chakula Duniani, WFP limelazimika kupunguza mikakati yake ya kusaidia maeneo yanayokabiliwa na upungufu wa chakula kutokana na ukosefu wa rasilimali fedha. Shirika hili linahitaji zaidi ya dolla za Kimarekani billioni moja katika kipindi cha mwaka 2014 ili kukabiliana na uhaba wa chakula unaoendelea kujitokeza katika nchi kadhaa duniani.

Hayo yamebainishwa na Bi Erthrin Cousin, mkurugenzi wa Shirika la Mpango wa Chakula Duniani wakati wa ziara yake ya kikazi katika nchi wafadhili ili kuzihamasisha kuchangia zaidi. WFP inalazimika kutumia kiasi cha dolla za Marekani 40, 000 kwa juma kwa ajili ya kuwahudumia wananchi millioni nne waliokimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha yao nchini Syria. Hali bado ni tete huko Haiti, Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati, Zimbabwe, DRC, Madagascar, Niger, Mali na Kenya.

WFP inapenda kuhamasisha wadau mbali mbali kuchangia kwa kuwashirikisha pia watu, mashirika na makampuni ya watu binafsi kama ambavyo UNICEF inavyofanya kwa ajili ya kugharimia miradi mbali mbali ya huduma kwa watoto wadogo sehemu mbali mbali za dunia.

Ni matumaini ya WFP kwamba, nchi nyingine zitaendelea kuiga mfano wa China na Falme za Kiarabu katika kuchangia fedha ili kukabiliana na ukosefu wa chakula sehemu mbali mbali za dunia. Wafadhali wa kawaida wanaendelea kuhamasishwa kuchangia mara kwa mara kwani WFP inawategemea sana.







All the contents on this site are copyrighted ©.