2014-02-04 15:21:25

Boresheni mifumo ya haki Tanzania


Hotuba ya DR. Jakaya Mrisho Kikwete Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa sherehe ya kuadhimisha siku ya sheria nchini tarehe 3 Februari, 2014 Dar es Salaam.
Mheshimiwa Jaji Mkuu;
Nakushukuru sana Mheshimiwa Jaji Mkuu kwa kunialika kwa mara nyingine tena kuja kujumuika nanyi kwenye maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini na ya Mahakama kuanza kazi mwaka huu. Ni jambo la busara kuwa siku hii inaadhimishwa kila mwaka. Inatupa fursa nzuri sisi tusio wanasheria kujifunza masuala mengi yahusuyo sheria na utoaji haki nchini.

Naomba na mimi niungane na wenzangu walionitangulia kukupongeza na kukushukuru Mheshimiwa Jaji Mkuu, Waheshimiwa Majaji, Mahakimu na watumishi wote wa Mahakama kwa kazi nzuri mliyofanya mwaka jana. Nami nawatakia mafanikio mema na utendaji mzuri zaidi katika mwaka huu wa 2014.

Kaulimbiu ya Mwaka Huu

Mheshimiwa Jaji Mkuu;
Kama ilivyo kawaida yenu, kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka huu inayosema “Utendaji haki kwa wakati: Umuhimu wa Ushiriki wa Wadau” imebeba ujumbe mzito na muhimu kwa wadau wa utoaji haki nchini. Kwa jumla inatukumbusha kuwa ili haki iwe na maana, ni lazima ipatikane kwa wakati. Msemo wenu maarufu wa “Justice delayed is justice denied” unaelezea kwa ufasaha dhana hii. Ni ukweli usiopingika kwamba ili haki ipatikane kwa wakati, ushiriki kwa ukamilifu wa wadau wote ni jambo la lazima. Wadau hao ni pamoja na Mahakama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, Polisi, TAKUKURU, Mawakili, Serikali na wengineo.

Endapo mmoja wa wadau hao atashindwa kutimiza wajibu wake ipasavyo, haki ya mtu au watu itachelewa kupatikana au itadhulumiwa. Hali hii inatokana na ule ukweli kwamba kila mdau anao wajibu maalum ambao hana budi kuutimiza. Ufanisi wa mmoja unategemea sana utendaji wa mwingine. Ni kama mwili wa binadamu ulivyo, kila kiungo kina nafasi yake, kimoja kisipofanya kazi vizuri siha ya mwili hodhoofika. Ndiyo hivyo ilivyo pia kwa mfumo wa utoaji haki.

Mahakama ambapo ni kilele katika mtandao au mfumo wa utoaji haki haikamati wahalifu, haipelelezi mazingira ya utendaji kosa, haitayarishi wala haiendeshi mashtaka. Hivyo basi, kazi ya Polisi, TAKUKURU na Mkurugenzi wa Mashtaka husaidia sana kuharakisha utoaji haki, Mahakama ina uharaka wa kusikiliza kesi hasa pale ambapo upelelezi umekamilika mapema na waendesha mashtaka wako tayari, na pia, uharaka wa upatikanaji wa nakala ya hukumu ili mtu aweze kukata rufaa kwa wakati.


Mheshimiwa Jaji Mkuu;

Masuala mengi kuhusu kaulimbiu ya mwaka huu umeyaeleza vizuri pamoja na wazungumzaji waliotangulia. Jambo kubwa na muhimu ambalo limejitokeza ni kuwa ushiriki na ushirikiano wa wadau ni muhimu sana katika utoaji haki kwa wakati. Mahakama ni kilele katika mfumo wa utoaji haki nchini. Lakini, Mahakama haipelelezi, haifikishi wahalifu mahakamani, haiendeshi mashtaka. Hasikilizi mashauri na hutoa kutoa uamuzi kuhusu upande upi una haki.

Hivyo, wale wapelelezi na waendesha mashtaka na wanaotetea wasipofanya kazi yao ipasavyo haki huchelewa. Hii ina maana kuwa Polisi wahakikishe wahalifu wanakamatwa, upelelezi unafanyika kwa makini na kesi zao zinapelekwa kwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ili zipelekwe Mahakamani.

Hivyo kwa TAKUKURU nao wahakikishe kuwa upelelezi unafanywa vizuri ili shauri linapofikishwa Mahakamani halichelewi kwa sababu ya upelelezi kutokukamilika. Mkurugenzi wa Mashtaka nae ahakikishe shauri analolipeleka limeandaliwa vizuri ili lichukue muda mfupi kusikilizwa na kuamuliwa. Weledi na uadilifu wa Polisi, TAKUKURU na DPP ni mambo ya msingi sana. Hivyo hivyo, Mawakili nao wana nafasi yao. Naambiwa kuna wakati shauri huaihirishwa kwa sababu ya wakili wa utetezi kushindwa kufika Mahakamani. Ukiacha sababu ya kuumwa lakini wakati mwingine ni kwa sababu ya kuwa na kesi mahali pengine.


Nafasi ya Mahakama

Mheshimiwa Jaji Mkuu;
Ni ukweli usiopingika kuwa Mahakama inayo nafasi ya pekee katika mfumo wa kutoa haki nchini. Nakubaliana na wale wanaouita Mhimili huu wa dola kuwa ni “The temple of Justice” kutokana na ukweli kwamba watu wanapokuja Mahakamani wanategemea kutendewa haki. Hakuna mahali pengine pa kukimbilia kutafuta haki zaidi ya Mahakamani. Wanaweza wasijue sheria za vitabuni, lakini wakajua haki yao. Hivyo, Waheshimiwa Majaji, Mahakimu na watumishi wengine wa Mahakama mnayo dhamana na wajibu mkubwa wa kusimamia sheria kwa haki. Ili haki itolewe bila upendeleo wa aina yoyote ile.

Matarajio ya wananchi ni kuwa kesi zisicheleweshwe kusikilizwa na kuamuliwa. Pale ambapo upelelezi umekamilika na mashtaka yametayarishwa vizuri kuahirishwa kusikilizwa kwa kesi huzaa manung’uniko. Pale shauri linapoamuliwa kutolewa kwa nakala ya hukumu ili anayetaka kukata rufaa afanye hivyo ni jambo la muhimu. Kinyume chake watu wanakata tamaa na kuamua kuchukua njia za mkato ambazo madhara yake ni makubwa. Wanakuwa hawana mahali pengine pa kupeleka mashtaka yao. Ndiyo maana nakubaliana na kauli yako Mheshimiwa Jaji Mkuu kwamba tusiiache misingi ya haki ikamomonyoka katika jamii yetu mpaka ukafika wakati watu wakaamini kwamba bila kutumia jambia hakuna haki. Naomba muendelee na kazi nzuri muifanyayo ili muwe kimbilio la uhakika kwa yeyote ambaye anajiona haki yake inadhulumiwa.

Mheshimiwa Jaji Mkuu;
Nimefarijika sana kusikia kwamba mmejiwekea utaratibu mzuri na misingi ya ushirikiano wa mawasiliano baina yenu na wadau wengine kwa ajili ya kuboresha utendaji wenu. Utaratibu huo utasaidia sana kuhakikisha upelelezi wa mashauri unakamilika haraka na haki inapatikana kwa wakati. Vilevile nawapongeza kwa kuelewa umuhimu wa kuhuisha sheria, kanuni na taratibu mara kwa mara ili kukidhi mahitaji ya wakati. Bila shaka hatua zote hizi zitasaidia sana kutatua changamoto ya siku nyingi ya ucheleweshwaji wa kesi.

Wajibu wa Serikali

Mheshimiwa Jaji Mkuu
Napenda kukuhakikisha kuwa sisi Serikalini tutaendelea kutimiza wajibu wetu ili Mahakama na wadau wengine wa utoaji haki wafanye kazi ipasavyo.
Kwanza tumechukua na tunaendelea kuchukua hatua kadhaa kufanya marekebisho ya sheria mbalimbali kufuatia tafiti na mapendekezo ya Tume zilizoundwa kuangalia mifumo yetu ya kutoa haki kwa lengo la kuiboresha. Kazi hiyo tunaendelea nayo. Tumeanza na kurekebisha sheria na mifumo ya utoaji haki na kuweza kutenganisha upelelezi na uendeshaji wa mashtaka.

Pili, tumeanza kuchukua hatua thabiti kuongeza bajeti ya Mahakama ili muweze kutimiza kwa ufanisi zaidi wajibu wenu. Mwaka huu wa fedha kwa mfano, tumetenga shilingi bilioni 86 kwenye Mfuko wa Mahakama na shilingi bilioni 42.7 kwa ajili ya maendeleo. Kiasi hiki ni kikubwa maradufu ukilinganisha na mwaka wa fedha uliopita ambapo zilitengwa shilingi bilioni 57 kwa shughuli zote. Pamoja na hatua hii muhimu tumejitahidi sana kuwezesha Mahakama kuongeza rasilimali watu, yaani Majaji Mahakimu na watumishi wengine. Idadi ya Majaji wa Rufani sasa imefikia 16 kutoka 9 waliokuwepo mwaka 2005, na wa Mahakama Kuu ni 69 kutoka 35 waliokuwepo mwaka 2005. Nilishakubali Majaji 20 wapya waajiriwe. Nileteeni mapendekezo niteue. Vilevile idadi ya Mahakimu imeongezeka zaidi na kufikia 672 na tayari kibali cha kuajiri wengine 300 kimeshapatikana. Hivi sasa mchakato wa ajira ya wahitimu wa sheria katika Mahakama za Mwanzo unaendelea.


Kufuatia mapendekezo ya Kamati za Jaji Mrosso na ya Jaji Lubuva, tumekamilisha mchakato wa kutenganisha shughuli za kutenda haki na utawala kwa kuanzisha nafasi ya Mtendaji Mkuu. Sasa hivi naambiwa pamekuwa na nafuu sana kwani mzigo waliokuwa nao Majaji kwenye masuala ya utawala haupo tena. Nasikitika kuwa idhini ya Muundo wa Mahakama umechelewa kuliko kawaida. Naahidi kuwa litakamilika wiki hii. Tumeendelea kuziongezea uwezo wa rasilimali fedha, vitendea kazi na nguvu kazi Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka na TAKUKURU.

Mheshimiwa Jaji Mkuu;
Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali nayo pia imefanyiwa marekebisho makubwa. Shughuli za Wizara zilizokuwa zimechanganyika na zile za Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali sasa hivi zimetenganishwa. Wizara imebaki na jukumu lake la kusimamia sera na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu inafanya shughuli za kisheria. Hatukuishia hapo. Tumefikia hatua nzuri ya kutenganisha shughuli za upelelezi na za kuendesha mashtaka. Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka imebaki na majukumu yake ya kusimamia mashtaka na Polisi, TAKUKURU na wengineo wanabaki na majukumu yao ya ukamataji wa wahalifu na upelelezi. Tunafanya yote haya kuboresha mifumo ya kutoa haki nchini.

Mwisho

Mheshimiwa Jaji Mkuu;
Mabadiliko yaliyofanyika yana lengo zuri la kuboresha taratibu zetu za kutoa haki nchini. Jambo kubwa ni mabadiliko kwa jamii na watendaji wenyewe. Watoaji haki ni lazima wajipime kwa matakwa na mahitaji yao. Endeleeni kutekeleza majukumu yenu mkielewa kwamba wananchi na jamii wanawategemea katika kuhakikisha kwamba haki inatolewa kwa wakati. Wadau wa utoaji haki muendelee kutimiza wajibu wenu wa kutatua migogoro, kuwapatanisha wananchi na kuwaadhibu wahalifu ili amani na utulivu nchini mwetu idumu. Watu wawe na maelewano na waishi bila wasiwasi.

Naomba kila mmoja wetu ashiriki kikamilifu kuhakikisha lengo letu linafikiwa. Kila mmoja wetu anayo nafasi yake, hili siyo jukumu la polisi peke yao, Mwanasheria Mkuu au Jaji Mkuu. Ni jukumu la wote. Basi mwaka huu tujitahidi kufanya vizuri zaidi, kila mtu afanye hivyo mahali alipo. Bila shaka haki itapatikana kwa wakati. Asanteni sana kwa kunisikiliza.








All the contents on this site are copyrighted ©.