2014-02-02 13:56:31

Wafanyakazi hewa wanavyokomba fedha ya Serikali ya Kenya!


Askofu Joseph Mbatia wa Jimbo Katoliki Nyahururu, nchini Kenya amelaani kitendo cha baadhi ya wafanyakazi wa serikali nchini Kenya kutokuwa waaminifu kwa kuendelea kuchukua mishahara ya wafanyakazi hewa. Huu ni uchu wa fedha na mali, kielelezo cha kumong'onyoka kwa tunu msingi za kimaadili na utu wema pamoja na kukosa uzalendo, hali inayoonesha jinsi ambavyo baadhi ya wafanyakazi wanashindwa kuwajibika.

Hivi karibuni, Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya alisema kwamba, serikali yake inapoteza wastani wa shilingi Billioni 1. 8 za Kenya kwa kulipa mishahara ya wafanyakazi hewa Serikalini, tabia inayochochewa na uchu wa mali na fedha miongoni mwa wananchi wa Kenya. Wafanyakazi wa Serikali wanachangamotishwa kujisadaka kwa ajili ya kuchangia mchakato wa maboresho ya maisha ya wananchi wa Kenya katika ujumla wao.

Askofu Joseph Mbatia ameyasema hayo hivi karibuni alipokuwa anaadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa shule ya Msingi ya Yohane Paulo II kuwa kinara katika mitihani ya darasa la saba nchini Kenya. Amewataka wazazi kuwashirikisha watoto wao furaha na matumaini kwa kuwaonesha malezi bora na makini. Wazazi waendelee kuwajibika kikamilifu kwa watoto na jamii kwa ujumla wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.