Kanisa litaendelea kuchangia katika ustawi na maendeleo ya Italia na kwa ajili ya
mafao ya wengi!
Baraza la Maaskofu Katoliki Italia limehitimisha mkutano wake ulioanza hapo tarehe
27 hadi tarehe 29 Januari 2014 mjini Roma. Marekebisho ya Katiba ya Baraza la Maaskofu
katoliki Italia kama sehemu ya mchakato unaopania kujenga na kuimarisha mshikamano
na umoja miongoni mwa Maaskofu katika utekelezaji wa mikakati ya shughuli za kichungaji
kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa nchini Italia pamoja na kuzingatia Katiba ni
kati ya mambo yaliyochambuliwa kwa kina na mapana wakati wa mkutano huu.
Hayo
yameelezwa na Askofu Nunzio Galantino, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki
Italia. Maaskofu wanalipongeza Kanisa nchini Italia kwa kuchangia katika ustawi na
maendeleo ya wananchi wa Itali pamoja na kuendelea kusimama kidete kulinda na kutetea
mafao ya wengi. Maaskofu wameamua kwamba, Baba Mtakatifu ataendelea kuteuwa Rais wa
Baraza la Maaskofu katoliki Italia pamoja na Katibu wake ambaye anapaswa kuwa ni Askofu
kwa uhuru kamili, baada ya kupewa majina kadhaa yatakayokuwa yamependekezwa na Baraza
la Maaskofu Katoliki Italia.
Maaskofu wamekazia pia umuhimu wa mikutano ya
Maaskofu katika Kanda mbali mbali za Italia, katika kujenga na kuimarisha umoja na
mshikamano, ili sauti ya Maaskofu wengi iweze kusikika. Wamefafanua kwa kina na mapana
tume mbali mbali za Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, asili, dhamana na wahusika
wake wakuu katika utekelezaji wa mikakati mbali mbali ya shughuli za kichungaji nchini
Italia.
Baraza la Maaskofu limepitia majibu ya maswali dodoso yaliyotolewa
na Sekretariei ya Sinodi za Maaskofu kama sehemu ya Maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi
Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia itakayofanyika mjini Vatican mwezi Oktoba,
2014. Majibu yaliyotolewa yanaonesha kwamba, watu wana kiu ya kuona tunu msingi za
maisha ya ndoa na familia zinalindwa na kuendelezwa.
Ni matumaini ya waamini
wa Kanisa Katoliki nchini Italia kwamba, Mababa wa Sinodi ya Familia wataweza kutafakari
kwa kina changamoto zinazojitokeza katika maisha na utume wa Familia na hivyo kuibua
mbinu mkakati utakaofanyiwa kazi na Mama Kanisa ili kuenzi tunu msingi za maisha ya
ndoa na familia kadiri ya mpango wa Mungu kwa mwanadamu na wala si vinginevyo.
Maaskofu
wanasema, Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kulihamasisha Kanisa kuhakikisha kwamba
linawekeza zaidi na zaidi katika sekta ya elimu kama ushiriki wa Kanisa katika maendeleo
ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Kanisa linatambua kwamba, lina mchango wa pekee katika
sekta ya elimu, hii ni sehemu ya mikakati yake ya Uinjilishaji Mpya; kumbe, Kanisa
na shule ni chanda na pete. Kanisa Katoliki nchini Italia linataka kuonesha ushuhuda
na mchango wake katika sekta ya elimu, kwa kuwashirikisha wanafunzi, wazazi na walimu
katika utume huu.
Baraza la Maaskofu Italia, hapo tarehe 10 Mei 2014, litaungana
na Baba Mtakatifu Francisko kusimama kidete ili kulinda na kutetea dhamana ya Kanisa
katika sekta ya elimu.