Wajengeeni vijana uwezo wa kupambana na makali ya maisha!
Mtakatifu Yohane Bosco alijipambanua kwa kujitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya
kuwajengea vijana uwezo wa kukabiliana na changamoto za maisha kwa njia ya eluimu
makini na endelevu. Akawa ni mfano wa Baba na Mlezi mwema kwa watoto waliokuwa wanatangatanga
bila ya kuwa na mahitaji msingi ya maisha; akawalisha kwa Neno la Mungu, Mkate wa
Uzima pamoja na kuwapatia elimu.
Ili kuendeleza utume wa Kanisa miongoni mwa
vijana, Mtakatifu Yohane Bosco akaanzisha Shirika la Wasalesiani wa Mtakatifu Bosco
na Shirika la Masista wa Bikira Maria Msaada wa Wakristo.
Ni mtakatifu aliyejitahidi
kusoma alama za nyakati na kwa kujibu kero za watu wake kwa kujikita katika Uinjilishaji
wa kina uliokuwa unamgusa mtu mzima: kiroho na kimwili, changamoto kwa Shirika la
Wasalesiani wa Mtakatifu Bosco kusoma alama za nyakati na kuendeleza utume huu katika
ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Hii ni sehemu
ya mahubiri iliyotolewa na Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Dodoma katika
Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Mtakatifu Yohane Bosco, iliyofanyika Jimbo Katoliki
Dodoma, mwishoni mwa Juma. Anasema, Mtakatifu Yohane Bosco alihakikisha kwamba, vijana
wanapata malezi makini na endelevu katika maisha yao ya kiroho, kiakili na kimwili;
akawajengea uwezo wa kupambana na makali ya maisha kwa njia ya ufundi stadi, hapa
akawa ameganga tatizo la ukosefu wa fursa za ajira, changamoto kwa Shirika la Wasalesiani
katika sekta ya elimu ili kusaidia kupunguza tatizo la ajira kwa kuwapatia vijana
elimu makini inayokwenda na wakati!
Mtakatifu Yohane Bosco alikazia umuhimu
wa elimu kwa vijana ili waweze kufahamu ukweli na kuutetea, kazi inayopaswa kuendelezwa
na Wasalesiani wa Mtakatifu Bosco kwa kuwapatia vijana ujuzi na maarifa pamoja na
Mafundisho ya Kanisa. Kazi ya majiundo kwa vijana inahitaji watu wanyenyekevu wanaoshuhudia
kwa maneno na matendo kazi kubwa iliyofanywa na mwanzilishi wa Shirika lao.
Askofu
Gervas Nyaisonga amewataka vijana wanaopata elimu na majiundo makini kutoka katika
shule na taasisi zinazoendeshwa na Wasalesiani wa Mtakatifu Bosco nchini Tanzania
kujenga na kudumisha utamaduni wa kupenda kusoma; kwa kukazia maadili na utu wema;
ili kuongeza ujuzi, maarifa na ubunifu mambo msingi katika kupambana na mazingira
mbali mbali ya maisha katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Vijana
wanaosoma kwenye taasisi za Wasalesiani wa Mtakatifu Yohane Bosco wawe ni mabalozi
wema kwa vijana wenzao kwa kushiriki kikamilifu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao
adili mchakato wa Uinjilishaji Mpya, sehemu mbali mbali watakakobahatika kwenda na
kufanya kazi. Wawe ni watu wanaoongozwa na Neno na Amri za Mungu.