2014-02-01 08:56:17

Sudan ya Kusini itajengwa katima msingi wa haki, amani, ukweli na upatanisho!


Baraza la Maaskofu Katoliki Sudan Kongwe na Sudan ya Kusini limehitimisha mkutano wake wa dharura ulioanza hapo tarehe 21 Januari hadi tarehe 31 Januari 2014, kwa kutoa tamko linalowataka wananchi wa Sudan ya Kusini kusimama kidete kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na ukweli.

Wanawataka viongozi wa kisiasa wanaohusika katika mgogoro wa kisiasa uliosababisha vita nchini humo kutekeleza bila mashari mkataba wa kusitisha vita, uliotiwa sahihi hapo tarehe 24 Januari 2014. Maaskofu wanasema, falsa ya kutumia mtutu wa bunduki kutafuta suluhu za kisiasa imepitwa na wakatu, umefika wakati kwa wananchi kujizatiti kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa.

Wale waliofanya mauaji dhidi ya jirani zao watubu na kusema ukweli kama sehemu ya mchakato wa kuponya madonda ya chuki na uhasama kati ya wananchi wa Sudan ya Kusini na kwamba, matukio haya yasijirudie tena miongoni mwa wananchi wa Sudan kwa ndugu wamoja kuanza kushambuliana na hatimaye, kusababisha vifo na watu kulazimika kuyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha na mali zao. Maaskofu wanasema, hawawezi kunyamaza kwani wameshuhudia mauaji ya kinyama kwa watu wa Sudan ya Kusini na Darfur; kwenye Milima ya Nuba; Abyei na Blue Nile.

Maaskofu wanasema kuna mambo kadhaa ambayo yamepelekea machafuko ya kisiasa nchini Sudan ya Kusini; mambo ambayo kimsingi yanapaswa kushughulikiwa kikamilifu ili kujenga na kuimarisha umoja wa kitaifa. Baadhi ya mambo haya ni: kinzani ndani ya chama tawala; kilio cha utawala bora; rushwa, ubinafsi pamoja na upendeleo wa kikabila na kindugu katika kugawana nyadhifa na madaraka mbali mbali; madonda ya chuki na uhasama ambayo bado hayajapatiwa dawa kamili ili yaponywe!

Maaskofu Katoliki Sudan Kongwe na Sudan ya Kusini wanasema, kuna haja ya kuanza mchakato wa ukweli na upatanisho; ili kuponya madonda ya chuki na utengano; watu waweze kusamaheana na kuanza kupatana tena, ili hatimaye waweze kuishi kwa amani. Ukweli na upatanisho ni mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza, ikiwa kama Sudan ya Kusini inataka kuishi katika amani na utulivu kwa sasa na kwa siku za usoni.

Serikali na wadau mbali mbali waanzishe mchakato wa majadiliano ya kweli, kwa kuwahusisha hata viongozi wa Kidini kwani mchango wao ni mkubwa. Inasikitisha kuona kwamba, katika majadiliano ya kutafuta suluhu ya mgogoro wa kivita huko Sudan ya Kusini, viongozi wa kidini waliwekwa kando kana kwamba, hawana mchango katika maisha na ustawi wa wananchi wa Sudan ya Kusini. Serikali haina budi kujikita katika ujenzi wa utawala bora pamoja na kuimarisha taasisi za kidemokrasia bila kutawaliwa na upendeleo na ukabila, sumu ya maendeleo ya taifa lolote lile!

Maaskofu wanavitaka vyombo vya habari kusaidia kutangaza na kueneza ukweli; kujenga na kusimamia haki na upatanisho na kamwe visiwe ni sababu na chanzo cha kutetea chuki na uhasama kati ya watu. Serikali inapaswa kujipanga katika kurekebisha muundo wa majeshi ya ulinzi na usalama kwa kutoyahusisha majeshi katika masuala ya kisiasa. Watoto hawana nafasi katika jeshi, kumbe, kuna haja ya kuzingatia mafunzo na kanuni maadili kwa vikosi vya ulinzi na usalama. Serikali iendelee kuwekeza katika sekta ya elimu kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wake wote.

Wakimbizi na wahamiaji wanapaswa kupewa haki zao msingi. Wananchi wa Abyei wanahaki ya kuchagua mustakabali wa maisha yao kwa siku za usoni na kwamba, Kanisa linaunga mkono kura ya maoni ili kuonesha mwelekeo wao! Kanisa halitakaa kimya kuona kwamba, baadhi ya viongozi wake wanaburuzwa na kuzuiwa kutekeleza wajibu wao msingi katika maisha ya watu wanaowahudumia: kiroho na kimwili. Kanisa litaendelea kuunga mkono juhudi za upatanisho Sudan ya Kusini pamoja na kusaidia Tuma ya taifa ya uponyaji, amani na upatanisho.

Baraza la Maaskofu Katoliki Sudan Kongwe na Sudan ya Kusini linasema, Nchi itajengwa katika msingi wa ukweli na haki na amani; kwa kuthamini na kuheshimu tofauti zilizopo kama utajiri na wala si kikwazo na chanzo cha vita na kinzani. Wananchi bado wanahamasishwa kusali kwa ajili ya kuombea: haki, amani na upatanisho wa kweli Sudan ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.