2014-02-01 09:31:59

Injili ya Furaha na Familia ni mada zinazoendelea kufanyiwa kazi na Maaskofu kwa wakati huu!


Waraka wa kichungaji wa Baba Mtakatifu Francisko, Injili ya Furaha na Maandalizi ya Sinodi ya Maalum ya Maaskofu kuhusu Familia, itakayoadhimishwa mjini Vatican mwezi Oktoba 2014 ni kati ya mada zilizofanyiwa kazi na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika, katika mkutano wake, ulioanza hapo tarehe 22 hadi tarehe 29 Januari 2014, Jimboni Manzini, nchini Swaziland.

Maaskofu wametafakari kwa kina na mapana umuhimu na changamoto za Waraka wa Injili ya Furaha kwa Maaskofu mahalia pamoja na mahusiano na majimbo ambayo wamekabidhiwa kuyaongoza wanapotekeleza dhamana ya kufundisha, kutakatifuza na kuwaongoza watu wa Mungu.

Baraza la Maaskofu limepitisha majibu yaliyotolewa na wadau mbali mbali kama sehemu ya Maandalizi ya Hati ya kutendea kazi. Itakubukwa kwamba, haya ni majibu ya maswali dodoso yaliyotolewa na Sektretarieti ya Sinodi za Maaskofu kwenda katika Majimbo ya Kanisa Katoliki sehemu mbali mbali za dunia.

Majimbo yamehamasishwa kuandaa siku moja ambamo wataadhimisha Siku ya Familia Jimbo, ili kuenzi na kutetea tunu msingi za maisha ya ndoa na familia; tunu ambazo zinakabiliwa na kinzani nyingi katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia bila kusahau ubinafsi na uchoyo; mambo yanayousonga moyo wa binadamu!

Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika wanajiandaa pia kuja mjini Vatican kwa ajili ya hija ya kitume inayofanywa na Maaskofu walau kila baada ya miaka mitano. Hija hii inatarajiwa kufanyika mwishoni mwa Mwezi Aprili, hii itakuwa ni fursa kwa Maaskofu wengi kutoka Kusini mwa Afrika kukutana na kuzungumza ana kwa ana na Baba Mtakatifu Francisko.

Maaskofu pia wamezindua kitabu kinachozungumzia majibu ya kichungaji kutoka kwa Kanisa Katoliki katika kukabiliana na changamoto za kichungaji kuhusiana na ugonjwa wa Ukimwi. Monsinyo Kevin Randall, Katibu wa Balozi wa Papa nchini Swaziland katika hotuba yake, amewasihii Maaskofu kuendelea kujikita katika maisha ya sala na unyofu wa moyo, wakijitahidi kuiga mfano wa Baba Mtakatifu Francisko kwa kuwaendea wale walioko pembezoni mwa Jamii, ili kuwaonjesha upendo na huruma ya Mungu.

Maaskofu pia walikuwa wamemwalika Rabbi Warren Goldstein aliyepambanua mikakati ya majadiliano ya kidini kati ya Kanisa Katoliki na Wayahudi Afrika ya Kusini. Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Kusini mwa Afrika linaandaa Waraka wa Kichungaji utakaozungumzia kuhusu uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika nchini Afrika ya Kusini sanjari na Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Miaka 20 tangu demorasia ya kweli iliporejeshwa tena Afrika ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.