2014-02-01 11:06:48

AMECEA kuadhimisha mkutano wake wa 18 nchini Malawi kuanzia tarehe 16 - 26 Julai 2014


Maandalizi ya Mkutano mkuu wa 18 wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA, ni kati ya ajenda kuu zilizofanyiwa kazi na Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi, lililoanza mkutano wake mkuu hapo tarehe 28 hadi tarehe 31 Januari 2014 mjini Lilongwe.

AMECEA inatarajia kufanya mkutano wake mjini Lilongwe kuanzia tarehe 16 hadi 26 Julai 2014, kwa kuongozwa na kauli mbiu "Uinjilishaji Mpya kwa njia ya wongofu na ushuhuda wa imani ya Kikristo". Mkutano huo unatarajiwa kuhudhuriwa na wajumbe wapatao 300 kutoka katika nchi zinazounda AMECEA. Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi limejadili majibu yaliyotolewa kwenye maswali dodoso kuhusu familia kama sehemu ya mchakato wa maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia itakayofanyika mjini Vatican kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba 2014.

Majibu haya yatatumwa kwenye Sekretarieti ya Sinodi za Maaskofu, tayari kwa maandalizi ya Hati ya kutendea kazi kama inavyojulikana kwa lugha ya Kilatini "Instrumentum Laboris". Maaskofu wamepembua hali ya Vyuo vikuu vya Kikatoliki pamoja na Taasisi za Elimu ya juu zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa nchini Malawi; Majiundo ya Makleri pamoja na ulinzi kwa watoto wadogo. Maaskofu pia wameangalia hali ya kisiasa nchini Malawi sanjari na Maandalizi ya uchaguzi mkuu utakaofanyika nchini humo tarehe 20 Mei 2014.

Mwishoni, Maaskofu pia wamezungumzia kuhusu hatua mbali mbali zilizokwishafikiwa na Kanisa Katoliki nchini Malawi katika mchakato wa Majadiliano ya Kiekumene sanjari na tafsiri ya Misale ya Waamini kwa lugha ya Taifa, "Chichewa".







All the contents on this site are copyrighted ©.