2014-01-30 07:44:54

Kumekucha!


Padre Raymond Saba, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, baada ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, bado kuna haja kwa waamini kuendelea kuimarisha imani yao kwa Kristo na Kanisa lake kwa njiaya ushuhuda wa maisha adili na matakatifu! RealAudioMP3

Baada ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliotangazwa, ukazinduliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa XVI; ukaadhimishwa kwa nguvu na ari kuu na hatimaye kufungwa na Papa Francisko, Wakristo wasidhani kwamba, hapa mambo yamekwisha, ndio kwanza waamini wanachangamotishwa na Mama Kanisa kujifunga kibwebwe ili kuimarisha misingi ya imani inayojikita kwa Kristo na Kanisa lake.

Umefika wakati kwa Wakristo kushuhudia imani yao kwa njia ya matendo na kwamba, maisha yao yawe ni mahubiri tosha kabisa kwa watu wanaokutana nao katika hija ya maisha yao hapa ulimwenguni. Wakristo wanahamasishwa kujifunza imani yao kwa bidii na juhudi kubwa! Wajitahidi kuifahamu, kuilinda na kuitetea!

Ni mwaliko wa kuikiri kama inavyofafanunuliwa kwenye Kanuni ya Imani; kuiadhimisha katika Sakramenti mbali mbali za Kanisa na Liturujia; kuimwilisha kwa kufuata Amri za Mungu na kanuni maadili pamoja na kuisali. Haya ndiyo mambo makuu yaliyokaziwa wakati wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani na kweli yanapaswa kuendelezwa kwa ari na kasi kubwa zaidi kwani bado kuna changamoto nyingi za uvunjivu wa misingi ya uhuru wa kuabudu pamoja na uwepo wa misimamo mikali ya kidini inayotishia imani na maisha kwa ujumla.

Waamini wasikubali kupoteza dira na mwelekeo wa imani na maisha yao kwa kukosa msingi thabiti. Ndiyo maana Baba Mtakatifu Francisko kwa wakati huu anaendeleza Katekesi kuhusu Sakramenti za Kanisa ni vyema waamini wakajitahidi kuzifahamu na kushiriki vyema katika maisha ya Kisakramenti, pamoja na kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Mungu na jirani, huu ndio muhtasari mkuu wa Imani kwa Kristo na Kanisa lake.







All the contents on this site are copyrighted ©.