2014-01-30 09:17:55

Jubilee ya Miaka 100 ya Ukristo Swaziland


Kanisa Katoliki nchini Swaziland, linaadhimisha Jubilee ya Miaka 100 ya Uinjilishaji wa kina, sanjari na kumsimika Askofu Jose Luis Ponce de Leon aliyeteuliwa hivi karibuni kuwa Askofu wa Jimbo la Manzini, Swaziland. Sherehe hizi ambazo zimefanyika hivi karibuni zimehudhuriwa na wajumbe wa Shirikisho la Baraza la Maaskofu Kusini mwa Afrika, SACBC pamoja na viongozi wa Serikali ya Swaziland. Baraza la Maaskofu Kusini mwa Afrika lilikuwa na mkutano wake wa Mwaka Jimboni Manzini.

Askofu mkuu Bhuti Tlagale, Rais wa Baraza la Maaskofu Afrika ya Kusini amempongeza Askofu Jose Luis Ponce de Leon kwa kuteuliwa kwake kuwaongoza watu wa Mungu Jimboni Manzini.

Kazi kubwa iliyoko mbele yake ni kuhakikisha kwamba, anawatakasa kwa njia ya Sakramenti za Kanisa; anawafundisha Neno la Mungu na Mafundisho Jamii ya Kanisa pamoja na kuwaongoza, daima akijitahidi kuiga mfano wa Kristo Mchungaji mwema. Atoe kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukimizwa pembezoni mwa Jamii, ili waweze kuonja huruma na upendo wa Mungu katika hija ya maisha yao hapa duniani.

Serikali ya Swaziland inayoongozwa na Mfalme Mswati wa tatu, imelipongeza Kanisa Katoliki nchini humo kwa kujimbanua kwa huduma makini kwa wananchi wa Swaziland: kiroho na kimwili katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu. Hii imekuwa ni sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji wa kina, ulioanza kucharuka kunako tarehe 27 Januari 1914, Kanisa la kwanza likajengwa Mbabane, linayojulikana kama Kanisa la Bikira Maria wa Mateso.

Waamini wa Kanisa Katoliki nchini Swaziland wanakadiriwa kuwa ni laki sita, sawa na asilimia 5%. Wakristo katika ujumla wao wanaunda asilimia 40% ya idadi ya wananchi wote wa Swaziland. Wananchi wanaheshimiana na kuthaminiana hata katika tofauti zao za kiimani, jambo ambalo linasifiwa sana na Serikali ya Swaziland.

Shirikisho la Baraza la Maaskofu Kusini mwa Afrika katika mkutano wake, limejadili kwa kina na mapana mchango uliotolewa na Mzee Nelson Mandela wa Afrika ya Kusini aliyefariki dunia hivi karibuni katika ustawi na maendeleo ya wananchi wa Kusini mwa Afrika kwa kukazia zaidi: usawa, umoja na mshikamano wa kitaifa, demokrasia.

Afrika ya Kusini inakabiliwa na changamoto ya kuendeleza mchakato huu baada ya kifo cha Mzee Nelson Mandela kwani bado kuna mengi yanapaswa kufanyika katika maboresho ya demokrasia, uhuru na maendeleo ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.