Tafakari ya Neno la Mungu kuhusu changamoto za kifamilia!
Kulingana na Sheria ya Musa, wanaume wote wa Israeli, walipaswa kwenda mbele ya Bwana
mara tatu kwa mwaka. Matukio makuu waliyopaswa kushiriki ni Sherehe ya Pasaka, Sherehe
ya Pentekoste na Sherehe ya Vibanda (soma Kut 12:24-27; 23:15; Kumb 16:1-17)*. Pahala
pa kukutana na Bwana palikuwa pale ambapo Sanduku la Ahadi lilikuwepo, chini ya ulinzi
wa makuhani. Mwanzoni Sanduku hili lilizunguka sehemu mbalimbali, mwishowe Mfalme
Daudi alilifikisha katika Mlima Sioni, ambapo baadaye Mfalme Selemani alilijengea
hekalu, jijini Yerusalemu (2Sam 6; 1Fal 8).
Kila Myahudi aliyekuwa akikaa karibu
na jiji la Yerusalemu alipaswa kushiriki katika ibada hizi. Kwa Wayahudi wengine waliokuwa
mbali ya Nchi Takatifu, ndoto yao ilikuwa kushiriki japo mara moja katika maisha yao.
Hivyo, twaweza kufikiria umati wa watu uliokuwa ukikusanyika jijini humu, katika sikukuu
hizi za kidini.
Akina mama walikuwa hawafungwi na sheria hii, lakini wengi
wao walikuwa wanakwenda kutokana na uchaji wao. Mfano ni familia ya Elkana, baba yake
nabii Samweli, mzee huyu na familia yake yote, yaani wake zake na watoto wake walikuwa
na desturi ya kwenda Silo kila mwaka, ambako Sanduku la Agano lilikuwepo. Familia
hii ilikwenda huku kuhiji na kutoa sadaka pamoja na waamini wengine (1Fal 1:3).
Watoto
wa kiume japokuwa wengine walikuwa wakienda kwenye hija hizi, lakini hakuwakuwa wakilazimika
kisheria. Watoto hawa wa kiume, walilazimika tu kwenda baada ya kutimiza mika kumi
na tatu. Baadhi ya wazazi walikuwa na desturi ya kuwazoeza watoto wao kushika mapokeo
haya mwaka mmoja kabla ya kutimiza umri uliotakiwa, watoto hawa waliitwa “wana wa
Sheria.” Licha ya wana hawa wa Sheria, wazazi wengi walikuwa wakiwachukua na kwenda
nao hija, hata katika umri mdogo kabisa.
Hivyo, hatuwezi kutia shaka kwamba
wazazi wa Yesu walikuwa na desturi ya kwenda nae hija Yerusalemu mara zote ambazo
wao wenyewe walikuwa wakienda kushiriki maadhimimisho haya matakatifu. Kwa hakika
wasingeweza kudiriki kumwacha Mtoto wao huyu wa thamani kuu machoni pao, nyumbani
kwao Nazarethi na wao kwenda Yerusalemu.
Mwinjili Luka ndiye anayetuhabari
juu ya tukio hili:
Kila mwaka wazazi wake walikwenda Yerusalemu kwa Sikukuu
ya Pasaka. Alipotimiza umri wa miaka kumi na miwili, walikwenda kama ilivyokuwa desturi
ya sikukuu. Baada ya siku zile, walirudi kwao, lakini Yesu alibaki Yerusalemu, wazazi
wake hawakuwa na habari (2:41-43).
Haya hizi tatu, ni sawa na kitunguu, kila
unapotoa ganda moja, unakutana na lingine. Hapa Mwinjili Luka anatufundisha mambo
mengini. Tuyadodoe machache kwa faida yetu.
Japokuwa kisheria ilitosha kukaa
kwa siku moja tu hekaluni, lakini Familia Takatifu ilikaa kwa juma zima la Sherehe
ya Mikate Isiyotiwa Chachu, jijini Yerusalemu, kama tunavyoambiwa “baada ya siku zile...”
Baada ya kumaliza shukrani yao, Maria na Yosefu walijiandaa kurudi nyumbani kwao Nazarethi,
pamoja na ndugu na majirani zao. Wazazi wanarudi nyumbani, Mtoto amebaki Yerusalemu,
bila wao kujua. Sababu ya tukio hili, hatuelezwi na mwandishi, ndio maana kuna wengi
waliojaribu kueleza sababu ya tukio hili. Tutaje maelezo yote, kwani kila moja lina
utajiri wake.
- Yesu alibaki Yerusalemu, bila wazazi wake kujua, kwa kuwa alitumia
uwezo wake wa kiungu kuondoka katikati yao, bila kuonekana. Lakini twaweza kujiuliza,
chini ya uangalizi makini ya wazazi haya, ingewezekanaje Mtoto huyu kutoonekana siku
nzima bila wazazi wake kugutuka?
- Safari ya wahujaji kurudi makwao, baada
ya maadhimisho haya matakatifu ilikuwa na utaratibu wake. Ili kutowachanganya wanawake
na wanaume, walikusanyika pekee yao, na kuondoka katika jiji takatifu, kundi la akina
mama mbele na akina baba wakifuatia. Safari iliendelea hivyo mchana kutwa, mpaka jioni
walipofika katika kituo cha kupumzika kwa siku hiyo. Watoto walikuwa huru, ama kuwa
katika kundi la akinamama au akina baba. Hivyo, Maria na Yosefu ulipofika wakati wa
kuondoka, kila mmoja alijua kwamba Mtoto Yesu yupo na mwenzake katika kundi lao.
Maria
d’Agreda, katika maono yake anasema kwamba Maria na Yosefu walikuwa wamezama katika
tafakari ya makuu waliyokwisha kuyaadhimisha katika sadaka ya Pasaka hekaluni. Wazazi
hawa walijua kuwa Yesu ndiye sababu, mhanga na lengo ya sadaka kuu iliyokuwa ikitolewa
na taifa lao. Wazazi waliendelea kupiga hatua mbele, bila wasiwasi wowote, kwani tukio
kama hili kamwe halikuwa limewahi kutokea katika familia yao. Tukio hili lilikuwa
la pekee na huru, ambalo Mtoto Yesu hakuwa amewahi kuonesha mfano wala dalili zake.
Tukio
hili twaweza kulielewa kuwa lilikuwa na mtazamo wa kiungu, kutokana na matukio mengine
yaliyotukia wakati wa utume wake.
Siku alipokataliwa na wana
mji wake wa Nazarethi. Wanamji alikasirika, wakambeba mzobemzobe ili wamtupe toka
mlimani ambapo mji huu ulikuwa umejengwa, lakini Yeye akapita katikati yao, bila wao
kumwona (soma Lk 4:28-30)
Wayahudi walipomzingira
Yesu alipokuwa hekaluni akizungumza nao juu ya ukuu wake dhidi ya Ibrahimu, alibeba
mawe ili wampige, ila yeye aliwaponyoka kati yao bila wao kujua (soma Yoh 8:59).
Bila
matukio haya mawili ni vigumu kuelewa kutoonekana huku kwa Yesu, tukizingatia upendo
mkuu, malezi mema na uangalizi makini ambao wazazi wake walikuwa wakimpatia siku zote.
Kupotea huku hakukutokana na kosa au uzembe wa wazazi. Lakini yalikuwa mapenzi ya
Mungu, ili kutoonekana kwake kuoneshe utukufu wa Baba yake, fadhila ya wazazi wake
na maongozi makuu ya majaaliwa ya kiungu.
Maria na akina mama wenzake walianza
safari mpaka wakafika mji wa Machmas (unaojulikana leo El Bir). Safari yao ilitawaliwa
na nyimbo zenye matamanio ya ujio wa Masiya. Twafahamu fika kuwa wakati wa kwenda
hija, kulikuwa na zaburi maalumu, Wimbo wa Kupandia (Zabb 120-134). Bila shaka wakati
wa kurudi bado kulikuwa na mwangi wa nyimbo hizi si tu mioyoni mwao, bali pia katika
midomo yao.
Katika moyo wa Maria kulikuwa na huzuni kwa kukosekana kwa mtoto
wake, ambaye alikuwa ni chemchemi ya furaha yake. Lakini kila alivyopiga hatua mbele
alikuwa akijifariji kwamba Mwana wake alikuwa, salama katika uangalizi wa baba yake.
Hakunung’unika moyoni kuwa mume wake amependelewa kwa kuwa na Mtoto wao pamoja. Mawazo
haya haya yalikuwa yanapita katika akili ya Yosefu.
Jioni ilipokuwa ikikaribia
waliweza kuziona kuta za mji wa Machmas ambao ndio ulikuwa kituo chao cha mapumziko
ya siku kwa wahujaji waliokuwa wakirejea Galilaya. Wazazi hawa wawili walipokutana,
kama radi ukweli ukweli ukawatokea, Yesu hayupo kati yao, hakuwa katika kundi la mbele,
wala hakuwa katika kundi la nyuma.
Wazazi hawa wawili waligubikwa na huzuni,
isiyo na mfano. Tunatambua hili kwa kinywa cha Mama Maria “... tukikutafuta kwa huzuni...”
Huzuni yao haikuweza kufichika, Maria Malkia wa huzuni, ambaye moyo wake ulikuwa ni
bahari ya huzuni, anamweleza Mtu wa Huzuni, Yeye aliye Ukweli ambaye alijua kina cha
huzuni yao. Moyo wa Yosefu ulijawa na jakamoyo lisiloweza kuelezeka.
Kartagena
anauliza: kwa nini wote walikuwa na huzuni? Maria alikuwa na huzuni kwa kuwa alikuwa
mama, Yosefu alikuwa na huzuni kwa kuwa alikuwa baba, wote kwa pamoja walihuzunika.
Upendo wa Maria ulikuwa ni upendo wa Yosefu. Huzuni na upendo wao kwa Yesu ilikuwa
sawa, ilikuwa ni isiyoweza kupimika kwa ukuu wala haikuwa na ukomo. Maria ni huzuni
na upendo wote, hali kadhalika Yosefu kwa Yesu.
Upendo na upole wa Yosefu kwa
ajili ya Mtoto huyu wa kiungu hatuwezi kuelezea; huzuni yake pia ilikuwa kama ya Maria,
ni bahari sisi ambao mioyo yetu ni sawa na kidimbwi haiwezi kuzama katika bahari hiyo.
Licha ya hali hii, lakini alikuwa na huzuni ya pekee kwa kuwa alikuwa na jukumu maalumu
la kumtunza Yesu, je atatoa maelezo gani kwa kuipoteza hazina hii aali ya Mungu?
-
Mwandishi mwingine anatupatia ufafanuzi huu, kutokana na maneno haya“Wakamtafuta kati
ya ndugu...” Tunaona hapa kwamba hakukuwepo na utengano kati ya Maria na Yosefu, bali
walisafiri pamoja. Katika kusafiri huku, Yesu hakuwa karibu nao, waliridhika kwa kuwa
walidhani amejichanganya na watoto wenzake wa ndugu na majirani zao.
Je wazazi
walaumiwe, kwani kutomwona mtoto kwa siku nzima na wao wasiwe hata na tashwishwi?
La hawastahili lawama, hasa kama tutajivika miwani ya desturi za wakati huo. Kulielewa
hili, nitoe mfano kwanza: Leo wazazi wanawapeleka watoto wao shuleni kwa magari au
boda boda. Aidha, shule nyingi zina mabasi yao, ya kuwachukua na kuwarudisha wanafunzi
wao. Lakini kwa sisi tuliosoma ‘enzi za Mwalimu’ tulikwenda shule wenyewe, tena kwa
miguu, na shule zenyewe zilikuwa umbali mrefu.
Desturi za wakati wa Yesu, ni
kuwa mtoto aliyefikisha miaka kumi na tatu, alifungwa na sheria zote za Musa na hivyo
aliwajibika kwa matendo yake mwenyewe. Ulikuwa ni umri wa kujipatia uhuru kutoka katika
utawala wa wazazi, ndio maana wazazi walianza kuwaandaa mwaka mmoja kabla, kwa kulegeza
baadhi ya maagizo na uangalizi wao, kama kamba ililegezwa kidogo, hivyo walikuwa na
uwanda mpanda zaidi wa uhuru.
Japokuwa jambo hili halikuwa linahitajika kwa
Mwana huyu wa kiungu, Yosefu aliona fika kuwa anapaswa kuendana na kawaida ya wazazi
wengine, ili isijefichuka siri ambayo wazazi hawa wa Yesu walikuwa wanaihifadhi mioyoni
mwao. Lakini twaweza kujiuliza, Maria na Yosefu baada ya purukushani zote za utoto
wa Yesu, wangediriki vipi kutembea siku nzima bila Yesu kuwepo katikati yao na wao
kuwa na amani, kwani akina Herode kamwe hawaishi duniani?
Kupotea huku kati
ya wazazi wake bila shaka lilikuwa ni fumbo toka mwanzo. Mungu ndiye aliyeficha siri
ya kutokuwepo kwake kati yao. Kutokuonekana kwa Yesu mbele ya wazazi wake kwa siku
tatu, akiwa jijini Yerusalemu, ni kivuli cha siku tatu ambazo Yesu alikuwa kaburini!
Kwa
Maria huzuni hii, ilikuwa sawa na aliyoipata alipokuwa chini ya Msalaba. Lakini watakatifu
wengi wanaamini huzuni ya siku tatu hizi ilikuwa kubwa zaidi. Maria hakupoteza amani
yake ya ndani, na hali hii ni ya kustaajabisha na ilimpatia mastahili makuu. Mungu
kwa siku hizi tatu alimwacha katika hali ya neema ya kawaida, alimnyima upendeleo
maalumu ambao roho yake ilitajirishwa nao wakati mwingine.
Maria anatuambia
kwamba na Yosefu pia alihuzunika vikali. Bila shaka faraja aliyoipata toka kwa Maria
ilimtia nguvu kuendelea kumtafuta Yesu. Upendo aliokuwa nao Yosefu kwa Mtoto huyu
wa kiungu ulimsukuma kumtafuta bila kupumzika au kula. Baada ya siku tatu za mahangaiko
na huzuni, hamadi wanamkuta Mtoto wao hekaluni, katikati ya waalimu “akiwasikiliza
na kuwauliza.” Luka anatuambia wale waliokuwa wakimwona na kumsikia, walishangazwa
na hekima yake.
Kwa hakika hotuba yake hii ya kwanza, iliwagusa watu, si tu
kuwaandaa, lakini kwa baadhi yao, ilikuwa mbegu ya kwanza ya ufuasi. Huyu aliyemfanya
Petro katika hotuba yake ya kwanza apate wafuasi lukuki (Mdo 2:41), Yeye mwenyewe
kwa hakika hasingeshindwa kupata walau mfuasi mmoja siku hiyo.
Jambo la kustaajabisha
hata Maria na Yosefu walishikwa na mshangao “Walipomwona walishangaa...” (2:48). Kulikuwa
na kitu kipya kwao, katika sauti yake, jinsi alivyokuwa amekaa mbele ya kadamnasi
hii na mtazamo wake. Katika kumbukumbu zao wazazi wao, hawakuwahi kumwona akiwa hivyo.
Walipigwa na butwaa, kimya kiliwashika cha furaha na kicho. Yosefu aliendelea kuwa
kimya, hakuwa anaamini macho na masikio yake! Kwani kwa nafasi yake ya kiongozi wa
familia, alikuwa na haki kumuuliza Mtoto wake nini kilichomfanya habaki Yerusalemu
wakati wote walikuwa wanarejea nyumbani, baba huyu hakutoa hata neno moja. Mkewe ndiye
anajitokeza mbele na kumuhoji Mtoto wake na Mungu wake “Kwa nini umetufanya hivi...”
Maria
hataji kwanza huzuni yake, anataja huzuni ya mume wake kwanza. Twaweza kujiuliza kwa
nini anafanya hivi? Mosi, japokuwa mateso ya Maria yalikuwa makuu na yasiyoweza kupimika,
hali hii haikumfanya hayasahau machungu ya Yosefu. Pili alifahamu jinsi Yesu alivyompenda
Yosefu, ndio maana anataja huzuni ya baba yake kuufanya moyo wa Yesu huguswe na kuona
kile alichokitenda kwa yule aliyempenda, kama vile ambavyo Mtoto huyu angekuswa na
kutambua jinsi alivyougusa upendo wa mama yake huyu.
Jibu la Yesu “Kwa nini
mmenitafuta...” Maana ya jibu hili lenye utata, ilifichika kwa wakati huo kwa wazazi
wake, tunaambiwa na mwinjili “Hawakuelewa alilosema.” Kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu
na ni Mungu, ya kuwa utume wake hapa duniani ni kuwakomboa wanadamu, kwa njia ya sadaka
ya maisha yake mwenyewe, haya yalikuwa wazi kwao, kwani Malaika alishawafunulia hili.
Isipokuwa utaratibu, jinsi ya kutelekeza utume wenyewe, eneo na wakati wake, ndio
maana katika Arusi ya Kana, Yesu alimwambie mamaye “Saa yangu bado” (Yoh 2:4). Hapa
kwa mara ya kwanza twamuona Yesu akifungua pazia na watu wakaweza japo kidogo kuona
mwanga wa utukufu wake. Utukufu huu ulonekana vyema mjini Kana, kwa ombi la mama yake
(Yoh 2:11).
Tukio hili la Mtoto Yesu kubaki hekaluni peke yake wakati wazazi
wake wakirejea nyumbani, ni la kipekee. Mwinjili Luka peke yake ndiye anayetuahadithia
tukio hili. Katika masimulizi yake ya utoto wa Yesu, anaanza akiwa Yerusalemu na anahitimisha
kwa tukio hili akiwa pia hapo hapo katika jiji takatifu. Yosefu, mtumishi wetu mtukuka
naye leo amekamilisha wajibu wake, na kama ilivyo tabia yake anakamilisha wajibu wake
katika ukimya, na hatumsikii tena katika masimulizi ya wainjili wetu, bali anabaki
nasi katika maombezi yetu, na hasa katika saa ya kifo chetu.
Mtoto aliyekabidhiwa
kumtunza, kumlinda na kumlea, ameshafikia umri wa kujitegemea kulingana na Sheria
ya Musa, ni mtu mzima, mwenye uhuru katika kutenga na kuwajibika kwa matendo yake.
Yukio hili la huzuni, kila Yosefu alipokuwa akilitafakari, lilikuwa ni chemchemi ya
faraja.
Moyoni mwake alikuwa anasema, kazi niliyotumwa kuitenda, nimeitimiza,
na kama kuna mtu aamini, aende Yerusalemu akawauliza waalimu Sheria!
Tumejifunza
nini katika tafakari yetu hii, mintarafu kutoonekana kwa siku tatu kwa Mtoto Yesu,
tukio lililowatia simanzi kuu wazazi wake?
Familia yangu ina
desturi gani? Familia Takatifu wao walikuwa na desturi ya ibada, ya uchaji. Je ya
kwangu ni ugomvi, ulevi na ukosefu wa staa mbele ya jirani?
Tumeona
umuhimu wa hija katika maisha yetu ya imani. Hija inatukumbusha kwamba hapa duniani
tu wasafiri, makazi yetu ni ya mpito. Lengo la maisha yetu ni kuishi na Mungu milele,
Yerusalemu yaa mbinguni. Tuna vituo vingi vya hija, vya kijimbo, kitaifa na kimataifa:
Pugu, Bagamoyo, Nakijoga, Namugongo, Kibeho, Lurdi, Fatima, Nchi Takatifu na Roma,
je nasi tunashiriki katika kwenda hija, sisi na familia zetu?
Watoto wangu niwafundishe maisha ya kiroho: kumjua Mungu na kuwa na kicho
naye, kusali, kujisomea Maandiko Matakatifu na kuyazingatia, kupenda kwanda kanisa,
kushiriki sakramenti hasa Ekaristi na Upatanisho na kuhudhuria kwenye jumuiya. Siwezi
kuwafundisha watoto haya, kama mimi mwenyewe si mfano mwema.
Mzazi
waweza kuwa makini katika malezi kwa asilimia tisini, bado kukatokea shida katika
makuzi ya mtoto wako. Tumtegemee Mungu zaidi, kuliko uangalizi wa macho yetu tu.
Mtoto wangu, napaswa kumpa mazoezi mbalimbali ili wakue, waweze kujiamini
na kujitegemea. Wasibaki kuwa watoto wa mama au baba. Wajione kuwa wana huru na wanapaswa
kuwajibika kwa uhuru huo.
Katika huzuni, bado tuwe
na amani, ili lawezekana kama tutamtanguliza Mungu mbele katika maisha yetu.
Aidha, katika huzuni nisijione mwenyewe tu, na hivyo kujikatisha tamaa.
Tutambue wengi wana huzuni nasi au zaidi yetu. Hivyo katika ushirika na umoja wa wahuzika,
tusimame na kumtazama Mtu wa Huzuni, aliyetoa yote kwa ajili ya ukombozi wetu.
Tafakari hii imeandaliwa
na Padre Stephano Kaombe Jimbo kuu la Dar es Salaam.