Shirika la Masista wa Pendo la huruma wa Mtakatifu Vincent wa Paulo, Mitundu Tanzania
Kuzinduliwa kwa kanda mpya ya Shirika la Masista wa pendo la huruma wa Mtakatifu Vincenti
wa Paulo - Mitundu nchini Tanzania ni kielelezo makini cha ushirikiano na ukomavu
wa kimissionari, unaowasukuma Wamissionari kutoka sehemu mbali mbali za dunia kujitosa
kimasomaso kwa ajili ya ujenzi wa ufalme wa Mungu.
Hii ni sehemu
ya mchakato wa mwendelezo wa kazi ya ukombozi wa mtu mzima: kiroho na kimwili. Kunako
mwaka 1981 Masista wa kwanza kutoka Innsbruck, Austria waliwasili nchini Tanzania
kwa mwaliko wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu waliokuwa wanatekeleza
utume wao Jimboni Singida, hususan wilaya ya Manyoni.
Masista hawa wakawa ni
wadau wakuu katika azma ya Uinjilishaji kwa kujikita kikamilifu katika sekta ya elimu,
afya na maendeleo endelevu sanjari na katekesi ya kina kwa waamini waliokuwa na kiu
ya kufahamu kweli za Kikristo. Wakajenga moyo ya ari ya kulitegemeza Shirika kwa kuwekeza
zaidi katika majiundo ya wainjilishaji katika nyanja mbali mbali za maisha. Pengine
Shirika la Masista wa pendo la huruma wa Mtakatifu Vincenti wa Paulo ni kati ya Mashirika
ya kimissionari yaliyowekeza zaidi katika rasilimali watu na hivyo kuwa na idadi kubwa
ya wataalam katika elimu, afya, uchumi na maendeleo endelevu ya Jamii.
Kuundwa
kwa Kanda mpya ya Shirika ni matokeo ya uvumilivu na saburi iliyooneshwa na Masista
wa kwanza waliowasili kutoka Austria, wakawa tayari kukabiliana na changamoto, vingiti
mbali mbali wakati wa ujenzi wa msingi wa Shirika nchini Tanzania pasi na kukata tama.
Walijenga na kuimarisha uhusiano wa dhati na wenyeji wa Kata ya Mitundu, kiasi cha
kujisikia kuwa wako nyumbani kwani ndani ya Kanisa hakuna mgeni wala mtu wa kuja!
Walionja upendo, ukarimu na tunza ya kibaba kutoka kwa Hayati Askofu Bernard Mabula
wa Jimbo la Singida, wakasonga mbele kwa ari na matumaini thabiti.
Masita wa
pendo la huruma wa Mtakatifu Vincenti wa Paulo - Mitundu, Tanzania, tangu mwanzo
walionesha na kujitahidi kujenga mshikamano wa dhati na wananchi wa Kata ya Mitundu,
katika raha na shida; mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mafno wa Mungu akapewa kipaumbele
cha kwanza katika sera, mikakati na huduma za Shirika. Wakasimama kidete kusikiliza
kilio cha wananchi wakati wa baa la njaa, milipuko ya magonjwa pamoja na kuhamasisha
elimu kama njia ya kuwakomboa watoto wa wakulima katika baa la umaskini wa hali na
kipato. Wakajenga, zahanati na shule na kunako mwaka 1985 huduma za kijamii zikaanza
kushika kasi ya ajabu; Kata ya Mitundu ikaanza kucharuka kwa maendeleo ya watu!
Wamissionari
kutoka Innsbruck walihitaji mshikamano wa dhati na watawa wazalendo ambao wangeendeleza
dhamana na utume waliokuwa wameuanzisha kwa ari na moyo mkuu. Kwa mara ya kwanza msichana
Maria Kitiku aliwasili Mitundu, tarehe 19 Machi 1985, huu ukawa ni mwanzo wa hamasa
za watawa wazalendo kutoka Tanzania.
Baada ya majiundo ya kina, akafunga nadhiri
zake za kwanza kunako mwaka 1989, akawa kweli ni nyota ya matumaini kwa ajili ya kuwahudumia
maskini na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii. Wasichana wengi wakavutwa
kwa karama na maisha ya Masista hawa, kiasi cha kujiunga nao, leo kuna jumla ya watawa
119 na kuna idadi kubwa ya wasichana walioko kwenye hatua mbali mbali za malezi ya
kuwa watawa!
Kuongezeka kwa idadi ya watawa na maboresho ya utume pamoja na
kuanza kujitegemea kwa asilimia kubwa, ukawa ni msingi wa kulipandisha Shirika nchini
Tanzania ili liweze kuwa n na hadhi ya kituo cha kimissionari, hapo mwaka 1996. Mwaka
2006 wajumbe wa mkutano mkuu wa Shirika wakaamua kwamba, ifikapo mwaka 2012, Shirika
nchini Tanzania lijitegemee na kuwa ni Kanda kamili: katika masuala ya uongozi na
shughuli za kiuchumi. Mwanzoni watawa wengi walikuwa na wasi wasi ikiwa kama wangeliweza
kufanikisha azma hii kwa kujitegemea wenyewe hasa kutokana na changamoto mbali mbali
zilizokuwa zinaendelea kujitokeza!
Wakapiga moyo konde na kuanza mchakato wa
kipindi cha mpito, wakiongozwa na Padre Gottfried Ugolini kwani walihitaji neema ya
kuanza, lakini zaidi neema ya kudumu katika maisha na wito wa kitawa! Kunako Mwaka
2011, Shirika likapata viongozi wa Mkoa wa Tanzania, chini ya uongozi wa Sr. Verediana
Herman, aliyesaidiwa na wajumbe wanne. Tarehe 27 Septemba 2013, Masista wa pendo la
huruma wa Mtakatifu Vincent – Mitundu- Tanzania, “wakabwaga manyanga” na kutangazwa
kuwa Kanda kamili inayojitegemea katika Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Askofu
Michael Msonganzila wa Jimbo Katoliki Musoma. Wanashirika wakakabidhiwa Katiba ya
Shirika, kama mwongozo na dira ya maisha na utume wao katika mchakato wa kuyamwilisha
mashauri ya Kiinjili.
Askofu Msonganzila aliwakumbusha watawa hawa kwamba,
Katiba kuu ya Shirika ni Yesu mwenyewe, aliyeteseka, akafa na kufufuka kutoka katika
wafu. Yesu anayewashirikisha katika dhamana ya Uinjilishaji, ili watu waweze kumfahamu,
kumpenda na kumtumikia Mwenyezi Mungu. Wanachangamotishwa kuhakikisha kwamba, wanasoma
alama za nyakati kwa kumwilisha katiba hii mintarafu mazingira, watu na nyakati. Wakuze
ndani mwao ari, wito na utume wa maisha ya Mtakatifu Vincent wa Paulo aliyejitosa
kimasomaso bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa maskini.
Masista wa pendo
la huruma wa Mtakatifu Vincent- Mitundu- Tanzania wanahimizwa kuwa ni watu wa sala;
wakiendelea kutoa kipaumbele cha kwanza kwa malezi msingi na endelevu; kwa kujituma
kwa juhudi, bidii na maarifa katika kazi, ili kuleta ufanisi na tija katika huduma
mbali mbali zinazotolewa na Masista hawa sehemu mbali mbali za Tanzania.
Imeandaliwa
na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.