Kanisa litaendelea kutangaza Injili ya Furaha, Kujenga na kudumisha mshikamano kati
ya watu!
Kanisa linaendelea kuhamasishwa kutangaza Injili ya Furaha kwa watu wa mataifa, kwa
kuwaimarisha katika imani, matumaini na mapendo; kwa njia ya Tafakari ya Neno la Mungu
na maisha ya Kisakramenti; kwa njia sala na matendo ya huruma yanayodhihirisha imani
tendaji. Kanisa halina budi kushikamana na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni
mwa Jamii pamoja na kudumisha moyo na ari ya kimissionari; Mwenyezi Mungu akipewa
kipaumbele cha kwanza.
Hii ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Kardinali Angelo
Bagnasco, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia katika ufunguzi wa mkutano wa
Baraza la Maaskofu katoliki Italia, CEI uliofunguliwa rasmi hapo tarehe 27 Januari
na unatarajiwa kufungwa tarehe 30 Januari 2014. Maaskofu wanawahimiza waamini na watu
wenye mapenzi mema nchini Italia kujenga na kuimarisha utamaduni wa mshikamano kwa
kuondokana na ubinafsi; hali ya kutovumiliana, nyanyaso na mateso kwa watu wasiokuwa
na hatia.
Maaskofu Katoliki nchini Italia wanaendelea kukazia umuhimu wa Uinjilishaji
Mpya na Kanisa kuendelea kujikita katika sekta ya elimu kwa umma, kama sehemu ya mchakato
wa kurithisha imani na tunu msingi za maisha ya kiutu na kijamii. Kanisa linatambua
kwamba, huduma ya elimu ni sehemu ya vinasaba na dhamana yake ya Uinjilishaji kwa
Watu wa Mataifa. Maaskofu wanapinga kitendo cha shule na taasisi za Kidini kubaguliwa
na Serikali katika huduma msingi.
Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linakemea
kwa nguvu zote vitendo vya rushwa na ufisadi vinavyofanywa na baadhi ya wanasiasa
kwa ajili ya mafao yao binafsi, kutokana na uchu wa mali na madaraka. Wanawataka wananchi
kamwe wasikubali kupokonywa matumaini ya maisha yaliyo bora kwa siku za usoni. Kanisa
kwa upande wake, litaendelea kuwa ni sauti ya wanyonge ndani ya Jamii pamoja na kushirikiana
na wadau mbali mbali katika mapambano dhidi ya umaskini na ukosefu wa fursa za ajira
kwa vijana.
Kardinali Bagnasco anasema kwamba, Jamii inahitaji wafanyakazi
na familia; mambo yanayohitaji ujenzi wa mshikamano wa dhati, kwa kutambua dhamana
na utume wa familia ndani ya Jamii. Sinodi Maalum ya Maaskofu kuhusu Familia iliyoitishwa
na Baba Mtakatifu Francisko ni kuonesha umuhimu wa familia katika maisha na utume
wa Kanisa sanjari na kutafuta mbinu mkakati wa kichungaji ili kukabiliana na changamoto
mbali mbali zinazojitokeza katika utume na maisha ya kifamilia.
Ndoa na familia
kadiri ya mpango wa Mungu inapaswa kuungwa mkono katika medani mbali mbali za maisha
bila kubaguliwa wala kubezwa!