Ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara hadi Dar Es Salaam kukamilika 2014
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema ameridhishwa na kazi ya ujenzi wa bomba
la gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam na kwamba anaamini kazi hiyo itakamilika
mwaka huu kama ambavyo wataalamu wameamuahidi. Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo Ijumaa,
Januari 24, 2014, wakati akiendelea na ziara yake ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa
bomba hilo la gesi lenye urefu wa kilometa 542.
Kwa mujibu wa Meneja wa mradi
huo, Eng. Kapullya Musomba, kazi hiyo ilipangwa kukamilika Juni mwakani, lakini sasa
hivi wanatarajia kazi hiyo itakamilika Desemba, mwaka huu. Akizungumza na waandishi
wa habari eneo la Somanga-Fungu wilayani Kilwa, mkoani Lindi, Waziri Mkuu alisema
jumla ya mabomba ya kutosha km. 440 yamekwishawasili nchini. “Hii ni sawa na asilimia
81 ya mabomba yanayohitajika kwa ajili ya kazi hii,” alisema.
Alisema kwamba
kazi ya utandikaji wa mambomba hayo imefanyika vizuri kiasi kwamba km. 114 kati ya
hizo zimekwishachimbwa (trenching) zinasubiri mabomba yaanze kutandazwa ardhini.
“Kwa kweli kazi inayofanywa ni nzuri, mabomba yaliyokwishaunganishwa mpaka sasa yanaweza
kutosha kutosha km. 263 ambayo ni zaidi ya nusu. Nina imani kwamba kazi hii itakamilika
mapema kama alivyosema mshauri mwelekezi wa mradi huu,” alisema.
Mapema, akitoa
maelezo kwa Waziri Mkuu kuhusu maendeleo ya mradi huo, Msimamizi Mkuu wa Mradi
wa Bomba, Eng. Thomas Baltazar alisema mabomba hayo yakishatandazwa ardhini yanaweza
kudumu kwa miaka 30 lakini yakifanyiwa matengenezo na kuangaliwa mara kwa mara
yanaweza kudumu kwa miaka 50.
Naye Mshauri Mwelekezi wa mradi huo, Eng,
Peter Erasmus wa kampuni ya Worley Parson ya Afrika Kusini alisifu uimara wa mabomba
yaliyotumika kwenye mradi huo na kumhakikishia Waziri Mkuu kwamba, yana ubora wa hali
ya juu ilikinganishwa na miradi mingine ambayo kampuni yake imesimamia katika bara
la Afrika.
Waziri Mkuu alikagua hatua mbalimbali za ujenzi wa bomba hilo kuanzia Vikindu
na Bungu mkoani Pwani; Somanga Fungu na Kitomanga mkoani Lindi ambako alionyeshwa
uwekaji wa zege nje ya mabomba ili yasielee baharini; utandazaji wa mabomba ardhini
na baharini na upindaji wa mabomba kwa kutumia mashine maalum. Pia aliweka jiwe
la msingi la Kiwanda cha Saruji cha Meis kilichopo eneo la Machole nje kidogo ya mji
wa Lindi.