2014-01-24 15:05:09

Mchango wa Jimbo la Papa katika Mkutano wa Geneva II


Askofu Mkuu Silvano Tomasi, Mwakilishi wa Jimbo la Papa katika Ofisi za Umoja wa Mataifa za Geneva, kwa niaba ya Jimbo la Papa, ameomba kusitishwa mara moja vita inayoendelea Syria. Wito huo aliutoa Alhamis katika Mkutano wa Kimataifa wa juu ya mgogoro wa vita Syria,Mkutano uliopewa jina Geneva II, uliohudhuriwa na wajumbe kutoka maeneo mbalimbali, hasa nchi za Mashariki ya kati, umoja wa Mataifa na kutoka Shirikisho la Nchi za Kiarabu. Mazungumzo haya ya amani ya kimataifa, yanalenga katika kujenga amani na maridhiano yanayoweza kumaliza mgogoro katika Syria.

Askofu Mkuu Silvano M. Tomasi alisema, vurugu zinapaswa kusitishwa mara moja kwa sababu zimeleta mahangaiko makubwa kwa watu wa Syria na mkoa huo kwa ujumla . Na kwamba ushiriki wa wanasiasa katika mkutano a Geneva II, ni ishara ya dhamira ya safi ya kisiasa katika kutoa kipaumbele cha mazungumzano badala ya utumiaji wa bunduki.Na hivyo , uwakilishi wa madhehebu mbalimbali ya kidini katika mkutano wao uliotangulia mkutano huu, waliweza kuthibitisha kwa mara nyingine, njia hii ya mazungumzo kuwa njia pekee na msingi katika kuleta hadhi sawa kwa kila mtu aliyeumbwa kwa mfano na sura ya Mungu na katika kuwa wazi kwa wengine.

Alielendelea kusema , wakati umefika wa kuchukua hatua madhubuti, kutekeleza nia nzuri zinazo tolewa na pande zote katika mgogoro wa sasa. Katika hali hii, Jimbo Takatifu , linarudia kutoa wito wake kwa pande zote zinazohusika katika mgogoro huu , kukubali kwa moyo mkunjufu na kwa ajili ya heshima ya utu wa binadamu, kusitisha kila aina ya ukatili dhidi ya binadamu katika taifa hili pendwa la Syria.
Pamoja na wito huo, Jimbo la Papa limependekeza kusitishwa kwa vita bila ya kuwa na masharti yanayofunga upande mmoja. Silaha zote ziwekwe chini , na fedha zote zilizolegwa kununua silaha zitumike katika mipango ya kutoa msaada kwa waathirika wa vita, na huduma nyingine msingi za kibinadamu.
Ukomeshaji wa uhasama lazima uandamane na ongezeko la misaada ya kibinadamu kama hatua ya kwanza katika ukarabati wa haraka wa maisha ya watu kurudi kawaida.
Vita vimesababisha uchumi wa nchi kuanguka, na hivyo juhudi za kurejesha tena hali ya kawaida ni lazima kuanza upya kwa pamoja kupitia mazungumzo endelevu na mshikamano wa ukarimu wa jumuiya ya kimataifa, na katika moyo na mwelekeo wa kidini .

Jimbo la Papa limeonyesha imani yake kwamba, amani Syria inaweza kuwa kichocheo cha amani katika maeneo mengine ya kanda hii ya nchi za Kiarabu.

Askofu Mkuu Tomasi, alihitimisha mchango wa Jimbo la Papa, na maneno ya Papa Francisko, yaliyozitaka pande zote katika mgogoro huu kusikiliza dhamiri yao kwa kina na kutojifungia katika nia zao binafsi , bali kutenda kwa manufaa ya wote kama ndugu na kwa ujasiri kuamua kufuata njia ya kukutana na majadiliano, na hivyo kuondokana na upofu unaoleta migogoro. Papa alihimiza wakumbuke si utamaduni wa mapambano wala utamaduni wa migogoro unaoweza kujenga maelewano ndani na baina ya watu, lakini badala yake ni utamaduni wa kukutana na utamaduni wa mazungumzo , ndiyo njia pekee ya kufikia amani endelevu.







All the contents on this site are copyrighted ©.