Viongozi wa Nchi za Kiafrika kukutana na Rais Obama mjini Washington DC, Agosti, 2014
Rais Barack Obama wa Marekani ametuma mwaliko kwa wakuu wa Nchi za Kiafrika kushiriki
katika mkutano maalum utakaofanyika Washington DC, kati ya tarehe 5 hadi tarehe 6
Agosti 2014. Ikulu ya Serikali ya Marekani inasema kwamba, lengo la mkutano huu ni
kuimarisha ushirikiano kati ya Marekani na Bara la Afrika linaloendelea kukua na kucharuka
kwa maendeleo ya kiuchumi.
Katika mkutano huu, Marekani itafafanua maendeleo
yaliyokwishafikiwa tangu Rais Barack Obama wa Marekani alipofanya mara ya mwisho ziara
ya kikazi Barani Afrika. Mkazo ni katika ushirikiano wa kibiashara na uwekezaji Barani
Afrika. Marekani itaendelea kuunga mkono juhudi za Bara la Afrika katika masuala ya
ulinzi na usalama.