Vijana Wakatoliki nchini Rwanda, Jumapili tarehe 26 Januari 2014 wanaadhimisha Siku
ya tisa ya Vijana Kitaifa, inayoongozwa na kauli mbiu “Heri walio maskini wa roho,
maana ufalme wa Mungu ni wao.”
Hii ndiyo
mada iliyochaguliwa na Baba Mtakatifu Francisko kunako Novemba 2013 kama changamoto
ya mwendelezo wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani iliyofanyika mjini Rio de Janeiro,
Brazil.
Maadhimisho ya Siku ya Vijana Kitaifa nchini Rwanda kwa mwaka huu yana
maana ya pekee kwani Tume ya shughuli za kichungaji kwa vijana kutoka Baraza la Maaskofu
Katoliki Rwanda, inasherehekea Jubilee ya Miaka 25 tangu ilipoanzishwa, kunako tarehe
21 Septemba 1989.
Kilele cha Jubilee hii kinatarajiwa kufanyika Mwezi Septemba,
2014 mjini Kabgayi, baadaye, Mwezi Novemba, Jimboni Byumba, kutafanyika Jukwaa la
Vijana Rwanda, Jukwaa ambalo linatarajiwa kuhudhuriwa na vijana kutoka Madhehebu mbali
mbali ya Kikristo kutoka ndani na nje ya Rwanda.