2014-01-22 07:23:32

Matumizi ya ndege za "droni" hayana budi kudhibitiwa kimaadili!


Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Ofisi za Umoja wa Mataifa zilizoko mjini Geneva, hivi karibuni, alizungumzia kuhusu mwelekeo wa kimaadili katika matumizi ya ndege zisizokuwa na rubani, kwani zinaweza kusababisha maafa kwa watu wasiokuwa na hatia pamoja na kuwaletea watu madhara ya kisaikolojia. RealAudioMP3

Jambo la msingi kwa Jumuiya ya Kimataifa ni kuhakikisha kwamba, inasimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu; maisha ya binadamu yakipewa kipaumbele cha kwanza.

Matumizi ya ndege zisizokuwa na rubani zinazojulikana kama “droni” yameendelea kuongezeka katika maeneo yenye vita, mgogoro na kinzani za kijamii. Ni teknolijia inayosaidia kupunguza matumizi ya wanajeshi katika migogoro ya kivita. Kumbe, matumizi ya ndege hizi hata kama yanaonesha kuwa na faida kubwa, hayana budi kusimamiwa na: sheria, kanuni na maadili, kwani wakati mwingine madhara yake yamekuwa ni makubwa kwa raia na mali zao.

Hii inatokana na ukweli kwamba, hakuna uwazi wa taarifa na wakati mwingine teknolojia hii inapania kutoa faida kubwa kwa watengenezaji, badala ya kuzingatia gharama ya maisha, mali ya raia husika na sanjari na madhara ya kisaikolojia na kiuchumi kwa kuishi daima katika hali ya wasi wasi. Haya ni mambo ambayo kimsingi yanapaswa kuangaliwa na Jumuiya ya Kimataifa katika kuhalalisha matumizi ya “droni”.

Kuna haja ya kuangali pia uwajibikaji wa wale wanaotumia vifaa hivi, kwani wakati mwingine yamekuwepo makosa ya kibinadamu na madhara yake yakawa ni makubwa kwa maisha ya watu na mali zao. Hapa kuna haki ya kimataifa, ni nani atakeywajibishwa kwa makosa ya kibinadamu yanayoweza kutendwa na “droni” katika maeneo ya kivita?

Hapa Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi anasema, kuna haja ya kukazia ukweli, uwazi na uwajibikaji. Matumizi ya silaha zinazojiendesha zenyewe hayana budi kudhibitiwa sana. Mtu aliyeandaliwa barabara; wenye habari kamili na makini katika matumizi ya silaha za “droni” ni muhimu sana, ili kuweza kufikia uamuzi wa kimaadili kwa kuongozwa na busara. Matumizi ya roboti katika masuala ya vita ni jambo ambalo linapaswa kufanyiwa utafiti mkubwa zaidi kabla ya Jumuiya ya Kimataifa haijaanza kuhalalisha matumizi yake.

Utafiti unaonesha kwamba, athari hizi si tu kwa walengwa, bali hata kwa askari wanaozitumia, ndiyo maana sheria na kanuni maadili hazina budi kuzingatiwa katika vita kwa nyakati hizi za maendeleo ya sayansi na teknolojia. Kuna hatari kwamba, teknolojia ya matumizi ya “droni” ikasambaa na hivyo kuhatarisha amani na usalama duniani.








All the contents on this site are copyrighted ©.