2014-01-22 08:12:35

Makanisa ya Kiprotestanti yahamishia Makao yake makuu kutoka Geneva kwenda Hannover!


Dr. Olav Fyske Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni hivi karibuni alizindua Makao Makuu Mapya ya Makanisa ya Kiprotestanti huko mjini Hannover, Ujerumani baada ya Makanisa haya kuhamisha Makao makuu yake kutoka Geneva, Uswiss ambako yalikuwepo huko kwa miaka 65. Makanisa haya yameenea katika nchi mbali mbali duniani na ni mwanachama wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni.

Uamuzi wa kuhamisha Makao makuu ulitolewa hivi karibuni na Kamati tendaji ya Makanisa ya Kiprotestanti baada ya kuona kwamba, wanaweza kushindwa kumudu gharama za pango na uendeshaji wa shughuli za Makanisa kutokana na kupanda kwa gharama ya maisha mjini Geneva.

Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni anawatakia kheri na baraka katika Makao Makuu mapya na kwamba waendelee kushikamana katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene, kwa ajili ya ushuhuda wa pamoja. Kama wajumbe wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni waendelee kusimama kidete kulinda na kutafuta haki katika masuala ya kijamii na kiuchumi sanjari na kuunga mkono juhudi za Makanisa ambayo yako kwenye migogoro na kinzani za kivita kama vile Sudan ya Kusini na Syria.

Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni anawaalika Makanisa wanachama kuungana pamoja ili kufanya hija ya haki na amani duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.