2014-01-22 09:01:51

Kongamano kuhusu matumizi ya rasilimali za gesi asilia, mafura na madini kwa amani na maendeleo ya Tanzania


Hotuba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete wakati ufunguzi wa kongamano la viongozi wa dini kuhusu matumizi ya rasilimali za gesi asilia, mafuta na madini kwa amani na maendeleo ya Tanzania, Whitesands Hotel, Jijini Dar es Salaam, tarehe 20-22 Januari 2014.

Waheshimiwa Viongozi wa Dini;
Waheshimiwa Mawaziri;
Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa;
Ndugu Makatibu Wakuu;
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;

Naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kukutana hapa siku ya leo kujadili matumizi ya rasilimali zetu za gesi asilia, mafuta na madini kwa amani na maendeleo ya nchi yetu. Kwa namna ya pekee nawashukuru viongozi wa dini kwa kunishirikisha kwenye Kongamano hili muhimu na la aina yake. Mmenipa heshima kubwa ambayo sikuitegemea. Asanteni sana.

Nawapongeza sana kwa uamuzi wenu wa busara wa kuandaa Kongamano hili. Mmedhihirisha kwa vitendo uhodari wenu wa kutekeleza jukumu lenu la msingi la kulea taifa letu kiroho na kushiriki kikamilifu katika masuala mengine muhimu yahusuyo maendeleo na ustawi wa Tanzania na watu wake. Ninyi ni wazalendo wa kweli. Ni matumaini yangu na ya Serikali ninayoingoza kuwa ubia wa aina hii utaimarishwa na kudumishwa kwa faida ya nchi yetu.

Najua mlianza kwa kukereketwa na athari za matumizi makubwa ya miti kwa matumizi ya nishati jambo ambalo linachangia sana kuharibika kwa mazingira duniani. Mmeishia kwenye Kongamano hili. Lina uwiano kabisa kwani tunakata miti kwa ajili ya kuni na mkaa. Tukitumia gesi itatoa huko. Ni dhamira yetu hiyo.

Ndugu Viongozi wa Dini;
Kongamano hili linafanyika katika kipindi mwafaka kabisa, kipindi ambacho ugunduzi mkubwa wa gesi tayari umefanyika na dalili za kugunduliwa zaidi zipo. Kipindi ambacho hazina ya madini mbalimbali inazidi kugunduliwa na makampuni ya utafiti yanatupa moyo kuwa mambo huenda yakawa mazuri zaidi. Pia, ni kipindi ambacho rasilimali zetu za wanyamapori na misitu zinatishiwa kutoweka. Ni kipindi ambacho wakulima na wafugaji na wafugaji na wahifadhi wa misitu na wanyamapori wanashindania ardhi ya kufanyia shughuli zao. Sasa hivi ni kipindi mwafaka kabisa kukaa chini na kutafakari jinsi gani rasilimali hizi zinaweza kulindwa na kutumika kwa manufaa ya nchi yetu na watu wake wote zikiwanufaisha kule ambako rasilimali hizo zipo na hata kule ambako hazipo.



Ni ukweli usiopingika kuwa Mwenyezi Mungu ameijalia nchi yenye utajiri mkubwa wa rasilimali za asili. Ametujaalia ardhi kubwa yenye rutuba, madini ya aina mbalimbali, misitu na mbuga za wanyama wa kila aina, hali ya hewa nzuri, bahari, maziwa makubwa, mito mingi, watu wengi na kadhalika. Rasilimali hizi, kwa tabia yake, inatakiwa zitumiwe vizuri ili kuboresha hali na maisha ya Watanzania wote sawia na kwa miaka mingi na hata milele. Vinginevyo rasilimali hizi zinaweza kugeuka kuwa chanzo cha mifarakano, magomvi na mauaji. Zinaweza kuwa balaa na kuleta maangamizi nchini badala ya kuwa baraka na neema.

Mifano ipo ya nchi mbalimbali duniani zilizojikuta zina migogoro na vita vya wenyewe kwa wenyewe kutokana na kugombania utajiri wao wa rasilimali za asili. Watu wa nchi hizo wanajuta kuwa na rasilimali ambazo zimekuwa chanzo cha kuhatarisha amani, utulivu, usalama na hata uhai wao.

Kwa hapa Tanzania tunashukuru Mungu rasilimali hazijageuka kuwa balaa na tunaomba hilo lisitokee. Tangu Tanganyika ipate uhuru na Zanzibar kufanya Mapinduzi Matukufu na hatimaye nchi zetu mbili kuungana na kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali za awamu zote zimesimamia kwa makini rasilimali za nchi yetu ili ziwanufaishe Watanzania wote. Tumetunga sheria na sera mbalimbali kuhakikisha kuwa lengo letu hilo linatimia.

Hata hivyo, usimamizi wa sheria hizo na utekelezaji wa sera zetu nzuri umekuwa unakabiliwa na changamoto mbalimbali kwa nyakati mbalimbali. Mpaka hapa tulipofika ni umahiri wa viongozi wetu ndiyo uliotuwezesha kuzuia mambo yasiharibike na kugeuka kuwa matatizo makubwa. Tumefanikiwa kiasi chake ingawaje hatujaweza kuzuia kabisa matatizo yasitokee hapa na pale.

Taarifa za kugombea rasilimali zimekuwa zinasikika na nyingine zikiwa zimesababisha watu kupoteza maisha, kujeruhiwa na mali kuharibiwa. Tutafanya nini kukomesha hali hiyo isijitokeze, ni jambo ambalo sisi kama taifa, yaani Serikali, wananchi na wadau mbalimbali, wakiwemo viongozi wa dini hatuna, budi kulizungumza na kulipatia ufumbuzi.

Ndugu Viongozi wa Dini;
Nimefarijika sana na uamuzi wenu wa kufanya mkutano huu kuzungumzia rasilimali ya mafuta na gesi. Juhudi za kutafuta mafuta na gesi imeanza tangu ukoloni, zikaendelea katika awamu zote baada ya Uhuru. Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) lilianzishwa mwaka 1969 kuongoza juhudi hizo na kusimamia sekta ya mafuta nchini kwa manufaa ya Watanzania wote. Hatujajaaliwa kupata mafuta mpaka sasa lakini tumefanikiwa kupata gesi. Ugunduzi wa kwanza wa gesi asilia ulifanyika Songosongo mwaka 1971 na baadae Msimbati, Mtwara mwaka 1982. Utafutaji na ugunduzi huo uligharimiwa na Serikali yetu na hivyo gesi hiyo ni mali ya Serikali. Baada ya ugunduzi huo makampuni binafsi yalipata shauku ya kutafuta mafuta na gesi nchini.

Mwaka 1980 ikatungwa Sheria ya Utafutaji wa Uzalishaji wa Mafuta kwa nia ya kuweka masharti na utaratibu wa makampuni kushiriki katika utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi nchini. Pia unatoa mwongozo wa mgawanyo wa mapato baina ya makampuni na Serikali. Sheria hiyo imeendelea kufanyiwa maboresho kwa nyakati mbalimbali kulingana na mahitaji ya wakati husika. Kuanzia mwaka 2007 shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia ziliongezeka kwa nguvu na kasi kubwa. Juhudi hizo zilizaa matunda mwaka 2010 kwa uvumbuzi wa kwanza wa gesi katika Bahari Kuu uliofanywa na Kampuni za Orphir na British Gas. Baada ya hapo ugunduzi umeendelea hadi kufikia futi za ujazo trilioni 46.5 za rasilimali ya gesi nchini mpaka sasa.

Utafiti unaendelea na matumaini ya kupata gesi zaidi yapo. Kufuatia ugunduzi huo, Tanzania sasa ni moja ya nchi zimazohesabiwa kuwa na gesi nyingi duniani na ni nchi inayovutia wawekezaji wengi katika sekta ya gesi. Kwa sababu hiyo, tukaamua kuifanyia mapitio Sheria ya Utafutaji na Uzalishaji wa Mafuta na Gesi. Mwaka 2013 tumetunga Sera ya Gesi na kurekebisha masharti ya Mkataba wa Kugawana Mapato yatokanayo na gesi (Production Sharing Agreement) na kuongeza mgao wa Serikali.

Ndugu Viongozi wa Dini;
Sera ya Gesi Asilia iliyopitishwa mwezi Oktoba, mwaka jana (2013) imeeleza wazi, tena kwa lugha nyepesi, kuwa gesi ya Tanzania ni mali ya Watanzania wote na itatumika kwa manufaa ya Watanzania wote – wa kizazi hiki na kijacho. Katika matumizi ya gesi, kipaumbele kitakuwa matumizi ya ndani. Msingi wa hoja yetu ni ule ukweli kwamba ukiuza nje gesi yote, unapata mapato peke yake lakini unakosa faida nyinginezo. Ukiitumia ndani unapata mapato na faida nyingine nyingi, kwa mfano, uzalishaji wa umeme, matumizi ya majumbani, kwenye magari na viwandani kuzalisha bidhaa mbalimbali. Hivyo basi mnapoitumia ndani gesi inakuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo ya nchi yetu.


Vilevile tupo katika mchakato wa kuandaa sera ya kuwashirikisha zaidi Watanzania (Local Content Policy) ili wanufaike zaidi na rasilimali yao ya gesi. Kwa sasa nimewaagiza TPDC wajiandae kushiriki katika utafutaji wa gesi, uzalishaji wake mpaka inapofika sokoni. Wasiwe wagawaji vitalu tu pekee. Katika sera hiyo mpya pia tunaangalia shughuli zinazoweza kufanywa na Watanzania ili tuone njia bora ya kuwawezesha kushiriki. Kwa sasa tunadhani wanaweza kushiriki kwa urahisi katika utoaji wa huduma kwa kampuni zinazofanya utafiti na uzalishaji wa gesi na mafuta. Wapo walioanza na wanafaidika. Nia yetu ni kuona idadi yao inaongezeka.

Mabibi na Mabwana;
Tumeanza pia mchakato wa kuiboresha TPDC ishiriki katika uwekezaji kwenye sekta ya mafuta na gesi kwa niaba ya Watanzania. Katika utaratibu huo, baadaye TPDC itauza hisa zake kwenye Soko la Mitaji ili Watanzania washiriki moja ka moja katika kumiliki rasilimali hii muhimu.

Ndugu Viongozi wa Dini;
Mambo yote hayo yanafanyika ili kuhakikisha masilahi ya taifa yanalindwa na Watanzania wote wananufaika na rasilimali zao kwa usawa. Changamoto kubwa tunayoiona kuhusu ushiriki wa Watanzania kwenye utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi ni uwezo mdogo wa fedha, utaalamu na teknolojia tulionao. Fedha zinazohitajika kwenye shughuli ya utafutaji mafuta na gesi, kwa mfano, ni nyingi mno na Watanzania wenzetu hawanazo na hakuna uhakika wa benki iliyo tayari kumkopesha mtu asiyekuwa nacho.

Namna nyingine ni kuwapa maeneo ili wao watafute wabia wawekeze. Lakini, mnapokuwa mnasheria inayoshirikisha ubia baina ya Serikali na mwekezaji, kuamua kuacha Serikali ili badala yake apewe Mtanzania binafsi si uamuzi rahisi sana kuufanya. Mtu binafsi ananufaika mwenyewe wakati Serikali inanufaisha wengi. Ninachokiona nafuu kufanya ni kutumia mwanya wa ushiriki wa TPDC ili tuone baadhi ya hisa ziuzwe kwa Watanzania. Hapa kunakuwa na ubia wa TPDC na wananchi upande mmoja na Serikali upande mwingine.

Jambo lingine tunalolifanya ni kuhakikisha kuwa rasilimali ya gesi inatumika vizuri, kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazo vijavyo. Tutaanzisha mfuko maalum wa kuhifadhi mapato ya gesi na kuwekewa masharti ya matumizi yake. Tutatunga sheria maalum kwa ajili hiyo na tutafanya hivyo kwaka huu.

Mabibi na Mabwaba;
Kwa upande wa rasilimali ya madini mabadiliko makubwa ya kiuchumi yaliyoanza miaka 1980 katikati, Serikali ilijitoa katika uwekezaji na ikabaki kuwa mhamasishaji na kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji. Kufuatia hali hiyo wawekezaji wengi walianza kuja kuwekeza katika maeneo mbalimbali pamoja na utafutaji na uchimbaji wa madini. Serikali ikaweka Sera (1997) na Sheria (1998) ya madini kusimamia sekta hiyo. Ni kweli mapato ya Serikali na fedha za kigeni ziliongezeka kutokana na uzalishaji wa madini. Lakini palikuwa na manung’uniko mengi kutoka kwa wananchi kuwa hawafaidiki sana na rasilimali zao.

Kamati mbalimbali ziliundwa kuangalia tatizo lipo wapi ili jawabu lake litafutwe. Nilipochaguliwa kuwa Rais wa nchi yetu mwaka 2005 niliyakuta manung’uniko hayo na kuamua tuyatafutie jawabu. Mwaka 2006 nikaunda Kamati ya Jaji Bomani ili ichambuwe mapungufu yaliyopo na kutoa mapendekezo ya hatua za kuchukua. Matokeo ya taarifa ya Kamati ile ni Sera Mpya ya Madini (2009) na Sheria Mpya ya Madini (2010). Sera na Sheria hii inalenga kuongeza faida zaidi kwa Serikali na jamii, bila kuwasahau wale wanaozunguka migodi.

Faida hizo ni pamoja na kuhimiza kampuni za uchimbaji wa madini kufungamanisha uchumi kati ya sekta ya madini na nyingine. Vilevile tumewataka waongeze nafasi ya ajira kwa Watanzania na ununuzi wa huduma na bidhaa nchini. Aidha, tumeamua Serikali iwe inapata hisa katika migodi mikubwa itakayoanzishwa siku za usoni. Ndiyo maana tunaendelea kufanya mazungumzo na kampuni zitazochimba uranium na nickel. Hatujamaliza lakini tunakwenda vizuri.

Halikadhalika, Sheria na Sera vimeweka mkazo wa kuendeleza wachimbaji wadogo ambao ni Watanzania tu. Katika kutekeleza hilo, tumeanza kutenga maeneo kwa ajili yao. Changamoto kubwa inayowakabili ni ukosefu wa mitaji, vifaa na utaalamu. Kuhusu fedha, tumeanzisha mfuko wa kuwasaidia na mwaka huu wa fedha tumewatengea jumla ya shilingi bilioni 2.5. Vile vile tunakamilisha taratibu za kuanza kuwakodisha vifaa kupitia ofisi zetu za madini za Kanda.

Jambo lingine kubwa ambalo tunajiandaa kulifanya ili kunufaisha wananchi na nchi yetu ni kutunga Sheria itakayohakikisha kuwa madini mengi yanayochimbwa nchini yanaongezewa thamani hapahapa nchini. Hatua hii itachangia sana kuongeza mapato na fursa ya ajira kwa watu wetu.

Nduvu Viongozi wa Dini;
Nimeyasema haya yote kuwaonesha kuwa Serikali haina mchezo katika usimamizi wa rasilimali zetu za asili. Tunafanya hayo kwa vile tunafahamu kuwa zinaweza kutuletea maendeleo ya haraka. Lakini pia zinaweza kusababisha nchi yetu kuingia kwenye dimbwi la migogoro inayotokana na rasilimali. Yote mawili yanaweza kutokea kutegemea tutasimamiaje na kuzitumiaje rasilimali zetu.

Jambo la muhimu ni kusaidiana kuelimisha jamii ya Watanzania namna tulivyojipanga kusimamia rasilimali zetu za gesi asilia, mafuta na madini. Waelewe kuwa utajiri huu ni mali yao na hivyo ni haki yao kunufaika nao. Wafahamu kuwa ni wajibu wao kulinda na kuzitunza rasilimali hizo ili zisipotee. Ninyi mnayo dhamana ya kuelimisha jamii waelewe nia hiyo njema ya Serikali. Pia napenda kusema kuwa siyo kweli kwamba Serikali haijali rasilimali za nchi au haitaki Watanzania wafaidike nazo; siyo kweli eti Serikali inapendelea wawekezaji wageni kuliko wazawa na hakuna mkoa au eneo linapuuzwa au kubaguliwa. Mimi na Serikali ninayoiongoza tutakua watu wa mwisho kupuuza wazawa na kupendelea wageni au kupuuza watu wa maeneo ambako rasilimali zinapatikana au hazijapatikana.


Ndugu Viongozi wa Dini;
Naomba muendelee kutekeleza jukumu lenu la msingi la kulea taifa kiroho. Mhimize waumini wenu wawe waadilifu na wazalendo. Waache kujihusisha na vitendo viovu vya wizi, ubadhilifu, matumizi mabaya ya madaraka na rushwa. Mkifanikiwa hilo, rasilimali zetu zitakuwa salama. Vile vile muendelee kuhubiri upendo miongoni mwenu, miongoni mwa waumini wenu na miongoni mwa watu wote. Watu wakumbushwe kuwa sisi wote ni viumbe wa Mungu na mbele yake sisi wote ni ndugu na inabidi kuheshimiana na kuvumiliana kwa tofauti zetu. Tukifaulu kwenye hili nchi yetu itabaki salama daima milele.

Nafahamu kuwa wapo baadhi ya watu ambao wanafanya vitendo vya kuhujumu rasilimali zetu. Wapo wanaoingia mikataba isiyozingatia maslahi ya taifa katika uvunaji wa rasilimali zetu. Wapo wengine wanaokula njama na wawekezaji ili Serikali ipunjwe mapato yake. Watu wa aina hiyo wapo katika jamii ye yote ile na sisi kuwa nao si ajabu. Napenda mfahamu kuwa Serikali inapinga vitendo vya aina yoyote vya kuhujumu rasilimali zetu. Ndiyo maana watu wa aina hiyo wanapobainika, wanachukuliwa hatua na vyombo vinavyohusika. Ninyi pia msichoke kuwafichua, wapo miongoni mwa waumini wenu.

Mabibi na Mabwana;
Kabla ya kumaliza, napenda kumshukuru Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospiter Muhongo na timu yake Wizarani kwa kushirikiana na viongozi wa dini katika jambo hili muhimu. Naamini hatua hii ya kuwapa taarifa sahihi viongozi wa dini kuhusu matumizi ya rasilimali zetu hususan gesi na madini itasaidia kuongeza uelewa wa waumini wenu na wananchi kwa jumla. Watafahamu fursa zilizopo na jinsi ya kuzitumia ili wafaidike nazo. Nakushukuru pia kwa kusimamia vizuri utekelezaji wa sera na mipango ya Serikali katika sekta ya nishati na madini. Kazi yenu nzuri inaonekana na sisi wote ni mashahidi.

Mwisho, nawashukuru viongozi wa dini kwa kunishirikisha kwenye Kongamano lenu. Naamini mkitoka hapa mtakuwa mabalozi wazuri wa kueneza ujumbe kuwa rasilimali za Watanzania zipo kwenye mikono salama.

Baada ya kusema hayo, napenda kutamka kuwa Kongamano la Viongozi wa Dini kujadili matumizi ya rasilimali zetu za gesi asilia, mafuta na madini kwa amani na maendeleo ya nchi yetu limefunguliwa rasmi. Nawatakia kila la heri na mafanikio katika mwaka huu wa 2014. Asanteni sana kwa kunisikiliza.








All the contents on this site are copyrighted ©.