Kongamano kuhusu matumizi ya rasilimali za gesi asilia, mafura na madini kwa amani
na maendeleo ya Tanzania
Hotuba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete wakati ufunguzi
wa kongamano la viongozi wa dini kuhusu matumizi ya rasilimali za gesi asilia, mafuta
na madini kwa amani na maendeleo ya Tanzania, Whitesands Hotel, Jijini Dar es Salaam,
tarehe 20-22 Januari 2014.
Waheshimiwa Viongozi wa Dini; Waheshimiwa Mawaziri; Waheshimiwa
Wakuu wa Mikoa; Ndugu Makatibu Wakuu; Wageni Waalikwa; Mabibi na Mabwana;
Naomba
nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha
kukutana hapa siku ya leo kujadili matumizi ya rasilimali zetu za gesi asilia, mafuta
na madini kwa amani na maendeleo ya nchi yetu. Kwa namna ya pekee nawashukuru viongozi
wa dini kwa kunishirikisha kwenye Kongamano hili muhimu na la aina yake. Mmenipa
heshima kubwa ambayo sikuitegemea. Asanteni sana.
Nawapongeza sana kwa uamuzi
wenu wa busara wa kuandaa Kongamano hili. Mmedhihirisha kwa vitendo uhodari wenu
wa kutekeleza jukumu lenu la msingi la kulea taifa letu kiroho na kushiriki kikamilifu
katika masuala mengine muhimu yahusuyo maendeleo na ustawi wa Tanzania na watu wake.
Ninyi ni wazalendo wa kweli. Ni matumaini yangu na ya Serikali ninayoingoza kuwa
ubia wa aina hii utaimarishwa na kudumishwa kwa faida ya nchi yetu.
Najua mlianza
kwa kukereketwa na athari za matumizi makubwa ya miti kwa matumizi ya nishati jambo
ambalo linachangia sana kuharibika kwa mazingira duniani. Mmeishia kwenye Kongamano
hili. Lina uwiano kabisa kwani tunakata miti kwa ajili ya kuni na mkaa. Tukitumia
gesi itatoa huko. Ni dhamira yetu hiyo.
Ndugu Viongozi wa Dini; Kongamano
hili linafanyika katika kipindi mwafaka kabisa, kipindi ambacho ugunduzi mkubwa wa
gesi tayari umefanyika na dalili za kugunduliwa zaidi zipo. Kipindi ambacho hazina
ya madini mbalimbali inazidi kugunduliwa na makampuni ya utafiti yanatupa moyo kuwa
mambo huenda yakawa mazuri zaidi. Pia, ni kipindi ambacho rasilimali zetu za wanyamapori
na misitu zinatishiwa kutoweka. Ni kipindi ambacho wakulima na wafugaji na wafugaji
na wahifadhi wa misitu na wanyamapori wanashindania ardhi ya kufanyia shughuli zao.
Sasa hivi ni kipindi mwafaka kabisa kukaa chini na kutafakari jinsi gani rasilimali
hizi zinaweza kulindwa na kutumika kwa manufaa ya nchi yetu na watu wake wote zikiwanufaisha
kule ambako rasilimali hizo zipo na hata kule ambako hazipo.
Ni
ukweli usiopingika kuwa Mwenyezi Mungu ameijalia nchi yenye utajiri mkubwa wa rasilimali
za asili. Ametujaalia ardhi kubwa yenye rutuba, madini ya aina mbalimbali, misitu
na mbuga za wanyama wa kila aina, hali ya hewa nzuri, bahari, maziwa makubwa, mito
mingi, watu wengi na kadhalika. Rasilimali hizi, kwa tabia yake, inatakiwa zitumiwe
vizuri ili kuboresha hali na maisha ya Watanzania wote sawia na kwa miaka mingi na
hata milele. Vinginevyo rasilimali hizi zinaweza kugeuka kuwa chanzo cha mifarakano,
magomvi na mauaji. Zinaweza kuwa balaa na kuleta maangamizi nchini badala ya kuwa
baraka na neema.
Mifano ipo ya nchi mbalimbali duniani zilizojikuta zina migogoro
na vita vya wenyewe kwa wenyewe kutokana na kugombania utajiri wao wa rasilimali za
asili. Watu wa nchi hizo wanajuta kuwa na rasilimali ambazo zimekuwa chanzo cha
kuhatarisha amani, utulivu, usalama na hata uhai wao.
Kwa hapa Tanzania tunashukuru
Mungu rasilimali hazijageuka kuwa balaa na tunaomba hilo lisitokee. Tangu Tanganyika
ipate uhuru na Zanzibar kufanya Mapinduzi Matukufu na hatimaye nchi zetu mbili kuungana
na kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali za awamu zote zimesimamia kwa makini
rasilimali za nchi yetu ili ziwanufaishe Watanzania wote. Tumetunga sheria na sera
mbalimbali kuhakikisha kuwa lengo letu hilo linatimia.
Hata hivyo, usimamizi
wa sheria hizo na utekelezaji wa sera zetu nzuri umekuwa unakabiliwa na changamoto
mbalimbali kwa nyakati mbalimbali. Mpaka hapa tulipofika ni umahiri wa viongozi wetu
ndiyo uliotuwezesha kuzuia mambo yasiharibike na kugeuka kuwa matatizo makubwa. Tumefanikiwa
kiasi chake ingawaje hatujaweza kuzuia kabisa matatizo yasitokee hapa na pale.
Taarifa
za kugombea rasilimali zimekuwa zinasikika na nyingine zikiwa zimesababisha watu kupoteza
maisha, kujeruhiwa na mali kuharibiwa. Tutafanya nini kukomesha hali hiyo isijitokeze,
ni jambo ambalo sisi kama taifa, yaani Serikali, wananchi na wadau mbalimbali, wakiwemo
viongozi wa dini hatuna, budi kulizungumza na kulipatia ufumbuzi.
Ndugu Viongozi
wa Dini; Nimefarijika sana na uamuzi wenu wa kufanya mkutano huu kuzungumzia rasilimali
ya mafuta na gesi. Juhudi za kutafuta mafuta na gesi imeanza tangu ukoloni, zikaendelea
katika awamu zote baada ya Uhuru. Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) lilianzishwa
mwaka 1969 kuongoza juhudi hizo na kusimamia sekta ya mafuta nchini kwa manufaa ya
Watanzania wote. Hatujajaaliwa kupata mafuta mpaka sasa lakini tumefanikiwa kupata
gesi. Ugunduzi wa kwanza wa gesi asilia ulifanyika Songosongo mwaka 1971 na baadae
Msimbati, Mtwara mwaka 1982. Utafutaji na ugunduzi huo uligharimiwa na Serikali yetu
na hivyo gesi hiyo ni mali ya Serikali. Baada ya ugunduzi huo makampuni binafsi yalipata
shauku ya kutafuta mafuta na gesi nchini.
Mwaka 1980 ikatungwa Sheria ya Utafutaji
wa Uzalishaji wa Mafuta kwa nia ya kuweka masharti na utaratibu wa makampuni kushiriki
katika utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi nchini. Pia unatoa mwongozo wa mgawanyo
wa mapato baina ya makampuni na Serikali. Sheria hiyo imeendelea kufanyiwa maboresho
kwa nyakati mbalimbali kulingana na mahitaji ya wakati husika. Kuanzia mwaka 2007
shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia ziliongezeka kwa nguvu na kasi kubwa.
Juhudi hizo zilizaa matunda mwaka 2010 kwa uvumbuzi wa kwanza wa gesi katika Bahari
Kuu uliofanywa na Kampuni za Orphir na British Gas. Baada ya hapo ugunduzi umeendelea
hadi kufikia futi za ujazo trilioni 46.5 za rasilimali ya gesi nchini mpaka sasa.
Utafiti unaendelea na matumaini ya kupata gesi zaidi yapo. Kufuatia ugunduzi
huo, Tanzania sasa ni moja ya nchi zimazohesabiwa kuwa na gesi nyingi duniani na ni
nchi inayovutia wawekezaji wengi katika sekta ya gesi. Kwa sababu hiyo, tukaamua
kuifanyia mapitio Sheria ya Utafutaji na Uzalishaji wa Mafuta na Gesi. Mwaka 2013
tumetunga Sera ya Gesi na kurekebisha masharti ya Mkataba wa Kugawana Mapato yatokanayo
na gesi (Production Sharing Agreement) na kuongeza mgao wa Serikali.
Ndugu
Viongozi wa Dini; Sera ya Gesi Asilia iliyopitishwa mwezi Oktoba, mwaka jana
(2013) imeeleza wazi, tena kwa lugha nyepesi, kuwa gesi ya Tanzania ni mali ya Watanzania
wote na itatumika kwa manufaa ya Watanzania wote – wa kizazi hiki na kijacho. Katika
matumizi ya gesi, kipaumbele kitakuwa matumizi ya ndani. Msingi wa hoja yetu ni ule
ukweli kwamba ukiuza nje gesi yote, unapata mapato peke yake lakini unakosa faida
nyinginezo. Ukiitumia ndani unapata mapato na faida nyingine nyingi, kwa mfano, uzalishaji
wa umeme, matumizi ya majumbani, kwenye magari na viwandani kuzalisha bidhaa mbalimbali.
Hivyo basi mnapoitumia ndani gesi inakuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo ya nchi
yetu.
Vilevile tupo katika mchakato wa kuandaa sera ya kuwashirikisha
zaidi Watanzania (Local Content Policy) ili wanufaike zaidi na rasilimali yao ya gesi.
Kwa sasa nimewaagiza TPDC wajiandae kushiriki katika utafutaji wa gesi, uzalishaji
wake mpaka inapofika sokoni. Wasiwe wagawaji vitalu tu pekee. Katika sera hiyo mpya
pia tunaangalia shughuli zinazoweza kufanywa na Watanzania ili tuone njia bora ya
kuwawezesha kushiriki. Kwa sasa tunadhani wanaweza kushiriki kwa urahisi katika utoaji
wa huduma kwa kampuni zinazofanya utafiti na uzalishaji wa gesi na mafuta. Wapo walioanza
na wanafaidika. Nia yetu ni kuona idadi yao inaongezeka.
Mabibi na Mabwana;
Tumeanza pia mchakato wa kuiboresha TPDC ishiriki katika uwekezaji kwenye sekta
ya mafuta na gesi kwa niaba ya Watanzania. Katika utaratibu huo, baadaye TPDC itauza
hisa zake kwenye Soko la Mitaji ili Watanzania washiriki moja ka moja katika kumiliki
rasilimali hii muhimu.
Ndugu Viongozi wa Dini; Mambo yote hayo yanafanyika
ili kuhakikisha masilahi ya taifa yanalindwa na Watanzania wote wananufaika na rasilimali
zao kwa usawa. Changamoto kubwa tunayoiona kuhusu ushiriki wa Watanzania kwenye utafutaji
na uzalishaji wa mafuta na gesi ni uwezo mdogo wa fedha, utaalamu na teknolojia tulionao.
Fedha zinazohitajika kwenye shughuli ya utafutaji mafuta na gesi, kwa mfano, ni nyingi
mno na Watanzania wenzetu hawanazo na hakuna uhakika wa benki iliyo tayari kumkopesha
mtu asiyekuwa nacho.
Namna nyingine ni kuwapa maeneo ili wao watafute wabia
wawekeze. Lakini, mnapokuwa mnasheria inayoshirikisha ubia baina ya Serikali na mwekezaji,
kuamua kuacha Serikali ili badala yake apewe Mtanzania binafsi si uamuzi rahisi sana
kuufanya. Mtu binafsi ananufaika mwenyewe wakati Serikali inanufaisha wengi. Ninachokiona
nafuu kufanya ni kutumia mwanya wa ushiriki wa TPDC ili tuone baadhi ya hisa ziuzwe
kwa Watanzania. Hapa kunakuwa na ubia wa TPDC na wananchi upande mmoja na Serikali
upande mwingine.
Jambo lingine tunalolifanya ni kuhakikisha kuwa rasilimali
ya gesi inatumika vizuri, kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazo vijavyo. Tutaanzisha
mfuko maalum wa kuhifadhi mapato ya gesi na kuwekewa masharti ya matumizi yake. Tutatunga
sheria maalum kwa ajili hiyo na tutafanya hivyo kwaka huu.
Mabibi na Mabwaba; Kwa
upande wa rasilimali ya madini mabadiliko makubwa ya kiuchumi yaliyoanza miaka 1980
katikati, Serikali ilijitoa katika uwekezaji na ikabaki kuwa mhamasishaji na kuweka
mazingira mazuri ya uwekezaji. Kufuatia hali hiyo wawekezaji wengi walianza kuja
kuwekeza katika maeneo mbalimbali pamoja na utafutaji na uchimbaji wa madini. Serikali
ikaweka Sera (1997) na Sheria (1998) ya madini kusimamia sekta hiyo. Ni kweli mapato
ya Serikali na fedha za kigeni ziliongezeka kutokana na uzalishaji wa madini. Lakini
palikuwa na manung’uniko mengi kutoka kwa wananchi kuwa hawafaidiki sana na rasilimali
zao.
Kamati mbalimbali ziliundwa kuangalia tatizo lipo wapi ili jawabu lake
litafutwe. Nilipochaguliwa kuwa Rais wa nchi yetu mwaka 2005 niliyakuta manung’uniko
hayo na kuamua tuyatafutie jawabu. Mwaka 2006 nikaunda Kamati ya Jaji Bomani ili
ichambuwe mapungufu yaliyopo na kutoa mapendekezo ya hatua za kuchukua. Matokeo ya
taarifa ya Kamati ile ni Sera Mpya ya Madini (2009) na Sheria Mpya ya Madini (2010).
Sera na Sheria hii inalenga kuongeza faida zaidi kwa Serikali na jamii, bila kuwasahau
wale wanaozunguka migodi.
Faida hizo ni pamoja na kuhimiza kampuni za uchimbaji
wa madini kufungamanisha uchumi kati ya sekta ya madini na nyingine. Vilevile tumewataka
waongeze nafasi ya ajira kwa Watanzania na ununuzi wa huduma na bidhaa nchini. Aidha,
tumeamua Serikali iwe inapata hisa katika migodi mikubwa itakayoanzishwa siku za usoni.
Ndiyo maana tunaendelea kufanya mazungumzo na kampuni zitazochimba uranium na nickel.
Hatujamaliza lakini tunakwenda vizuri.
Halikadhalika, Sheria na Sera vimeweka
mkazo wa kuendeleza wachimbaji wadogo ambao ni Watanzania tu. Katika kutekeleza hilo,
tumeanza kutenga maeneo kwa ajili yao. Changamoto kubwa inayowakabili ni ukosefu
wa mitaji, vifaa na utaalamu. Kuhusu fedha, tumeanzisha mfuko wa kuwasaidia na mwaka
huu wa fedha tumewatengea jumla ya shilingi bilioni 2.5. Vile vile tunakamilisha
taratibu za kuanza kuwakodisha vifaa kupitia ofisi zetu za madini za Kanda.
Jambo
lingine kubwa ambalo tunajiandaa kulifanya ili kunufaisha wananchi na nchi yetu ni
kutunga Sheria itakayohakikisha kuwa madini mengi yanayochimbwa nchini yanaongezewa
thamani hapahapa nchini. Hatua hii itachangia sana kuongeza mapato na fursa ya ajira
kwa watu wetu.
Nduvu Viongozi wa Dini; Nimeyasema haya yote kuwaonesha kuwa
Serikali haina mchezo katika usimamizi wa rasilimali zetu za asili. Tunafanya hayo
kwa vile tunafahamu kuwa zinaweza kutuletea maendeleo ya haraka. Lakini pia zinaweza
kusababisha nchi yetu kuingia kwenye dimbwi la migogoro inayotokana na rasilimali.
Yote mawili yanaweza kutokea kutegemea tutasimamiaje na kuzitumiaje rasilimali zetu.
Jambo
la muhimu ni kusaidiana kuelimisha jamii ya Watanzania namna tulivyojipanga kusimamia
rasilimali zetu za gesi asilia, mafuta na madini. Waelewe kuwa utajiri huu ni mali
yao na hivyo ni haki yao kunufaika nao. Wafahamu kuwa ni wajibu wao kulinda na kuzitunza
rasilimali hizo ili zisipotee. Ninyi mnayo dhamana ya kuelimisha jamii waelewe nia
hiyo njema ya Serikali. Pia napenda kusema kuwa siyo kweli kwamba Serikali haijali
rasilimali za nchi au haitaki Watanzania wafaidike nazo; siyo kweli eti Serikali inapendelea
wawekezaji wageni kuliko wazawa na hakuna mkoa au eneo linapuuzwa au kubaguliwa.
Mimi na Serikali ninayoiongoza tutakua watu wa mwisho kupuuza wazawa na kupendelea
wageni au kupuuza watu wa maeneo ambako rasilimali zinapatikana au hazijapatikana.
Ndugu Viongozi wa Dini; Naomba muendelee kutekeleza jukumu lenu la msingi la
kulea taifa kiroho. Mhimize waumini wenu wawe waadilifu na wazalendo. Waache kujihusisha
na vitendo viovu vya wizi, ubadhilifu, matumizi mabaya ya madaraka na rushwa. Mkifanikiwa
hilo, rasilimali zetu zitakuwa salama. Vile vile muendelee kuhubiri upendo miongoni
mwenu, miongoni mwa waumini wenu na miongoni mwa watu wote. Watu wakumbushwe kuwa
sisi wote ni viumbe wa Mungu na mbele yake sisi wote ni ndugu na inabidi kuheshimiana
na kuvumiliana kwa tofauti zetu. Tukifaulu kwenye hili nchi yetu itabaki salama daima
milele.
Nafahamu kuwa wapo baadhi ya watu ambao wanafanya vitendo vya kuhujumu
rasilimali zetu. Wapo wanaoingia mikataba isiyozingatia maslahi ya taifa katika uvunaji
wa rasilimali zetu. Wapo wengine wanaokula njama na wawekezaji ili Serikali ipunjwe
mapato yake. Watu wa aina hiyo wapo katika jamii ye yote ile na sisi kuwa nao si
ajabu. Napenda mfahamu kuwa Serikali inapinga vitendo vya aina yoyote vya kuhujumu
rasilimali zetu. Ndiyo maana watu wa aina hiyo wanapobainika, wanachukuliwa hatua
na vyombo vinavyohusika. Ninyi pia msichoke kuwafichua, wapo miongoni mwa waumini
wenu.
Mabibi na Mabwana; Kabla ya kumaliza, napenda kumshukuru Waziri wa
Nishati na Madini, Profesa Sospiter Muhongo na timu yake Wizarani kwa kushirikiana
na viongozi wa dini katika jambo hili muhimu. Naamini hatua hii ya kuwapa taarifa
sahihi viongozi wa dini kuhusu matumizi ya rasilimali zetu hususan gesi na madini
itasaidia kuongeza uelewa wa waumini wenu na wananchi kwa jumla. Watafahamu fursa
zilizopo na jinsi ya kuzitumia ili wafaidike nazo. Nakushukuru pia kwa kusimamia
vizuri utekelezaji wa sera na mipango ya Serikali katika sekta ya nishati na madini.
Kazi yenu nzuri inaonekana na sisi wote ni mashahidi.
Mwisho, nawashukuru viongozi
wa dini kwa kunishirikisha kwenye Kongamano lenu. Naamini mkitoka hapa mtakuwa mabalozi
wazuri wa kueneza ujumbe kuwa rasilimali za Watanzania zipo kwenye mikono salama.
Baada ya kusema hayo, napenda kutamka kuwa Kongamano la Viongozi wa Dini kujadili
matumizi ya rasilimali zetu za gesi asilia, mafuta na madini kwa amani na maendeleo
ya nchi yetu limefunguliwa rasmi. Nawatakia kila la heri na mafanikio katika mwaka
huu wa 2014. Asanteni sana kwa kunisikiliza.