Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dr. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia Salamu
za Rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mheshimiwa Perseko Kone kutokana na vifo vya
watu wazima 12 na mtoto mmoja wa miezi minne vilivyotokea tarehe 20 Januari, 2014
kufuatia kugongana uso kwa uso kwa gari aina ya Toyota Noah lililokuwa limebeba abiria
likitokea Itigi kwenda Singida na lori katika eneo la Isuna Mkoani Singida.
“Nimeshtushwa,
nimesikitishwa na kuhuzunishwa mno na taarifa za vifo vya watu 13 akiwemo mtoto wa
miezi minne waliofariki papo hapo katika eneo la ajali tarehe 20 Januari, 2014 baada
ya gari aina ya Toyota Noah walilokuwa wakisafiria kutoka Itigi kwenda Singida kugongana
uso kwa uso na lori katika eneo la Isuna”.
Rais Kikwete amesema inatia simanzi
kuona ajali zikiendelea kutokea na kupoteza maisha ya watu wasio na hatia na hususan
mtoto mdogo kama huyu wa miezi minne, kusababisha ulemavu wa kudumu kwa baadhi ya
watu na uharibifu wa mali kutokana na makosa ya binadamu katika uendeshaji wa vyombo
vya moto.
“Kufuatia ajali hiyo ya kusikitisha, ninakutumia wewe Mkuu wa Mkoa
wa Singida, Mheshimiwa Perseko Kone salamu zangu za rambirambi kutokana na msiba huo,
na kupitia kwako, naomba unifikishie salamu zangu za rambirambi na pole nyingi kwa
familia zote zilizopoteza wapendwa wao katika ajali hiyo. Nawaomba wanafamilia wawe
na moyo wa uvumilivu, subira na ujasiri hivi sasa wanapougulia machungu ya kupotelewa
na ndugu zao”, amesema Rais Kikwete kwa masikitiko.
Aidha Rais Kikwete amesema
anamuomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema azipokee na kuzilaza Mahala Pema Peponi
Roho za Marehemu wote, na amewahakikishia wafiwa kuwa yuko pamoja nao katika kuomboleza
msiba huu mkubwa. Vilevile amemtakia ahueni kijana mmoja majeruhi wa ajali hiyo na
aweze kupona haraka na kurejea katika hali yake ya kawaida na kuungana tena na ndugu
na jamaa zake.