2014-01-21 07:30:22

Ratiba elekezi ya Ibada zitakazoongozwa na Papa Francisko


Monsinyo Guido Marini, Mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa anaonesha kwamba, Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Jumapili ya Pili ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa, sanjari na Siku ya Mia Moja ya Wahamiaji na Wakimbizi Duniani, tarehe 19 Januari 2014, ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Parokia ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, Jimbo kuu la Roma. RealAudioMP3

Tarehe 25 Januari 2014, Siku kuu ya Kuongoka kwa Mtakatifu Paulo, Mtume na Mwalimu wa mataifa, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuongoza Ibada ya Masifu ya Jioni yatakayofanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo, nje ya kuta za Roma. Hiki kitakuwa pia ni kilele cha kufunga Juma la kuombea Umoja wa Wakristo ambao kwa Mwaka huu unaongozwa na kauli mbiu, Je, Kristo amegawanyika? Ibada hii itaanza saa 11:30 Jioni kwa Saa za Ulaya.

Tarehe 2 Februari 2014, Siku kuu ya kutolewa Bwana Hekaluni, sanjari na Maadhimisho ya Siku ya 18 ya Watawa Duniani iliyoanzishwa na Mwenyeheri Yohane Paulo II, Baba Mtakatifu anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume.

Tarehe 16 Februari 2014, Jumapili ya VI ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa takatifu kwenye Parokia ya Mtume Thoma, Jimbo kuu la Roma.

Tarehe 22 Februari, 2014, Siku kuu ya Ukulu wa Mtakatifu Petro, Baba Mtakatifu Francisko, kuanzia saa 5:00 kwa saa za Ulaya anatarajiwa kuwasimika Makardinali Wapya 19 walioteuliwa hivi karibuni.

Tarehe 23 Febuari 2014, Baba Mtakatifu ataadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu kwa kushirikiana na Makardinali wote wapya. Kama kawaida, Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican itaendelea kukujuza yale yanayojiri katika maisha na utume wa Kanisa hapa Vatican na kutoka sehemu mbali mbali za dunia.








All the contents on this site are copyrighted ©.