2014-01-20 07:39:08

Mkutano wa Utume wa Bahari waanza mjini Vatican


Waratibu wakuu wa Utume wa Bahari, kitengo cha Baraza la Kipapa la wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, tangu tarehe 20 Januari hadi tarehe 24 Januari 2014 watakuwa na mkutano mkuu unaowajumuisha wajumbe kutoka katika kanda tisa za Utume wa Bahari. RealAudioMP3 RealAudioMP3

Hiki ni kipindi cha kufanya tafakari ya kina sanjari na kushirikisha uzoefu na mang’amuzi, tayari kuweka mikakati ya shughuli za kichungaji kwa Mabaharia na wavuvi sehemu mbali mbali za dunia.

Kardinali Antonio Maria Vegliò katika hotuba yake ya ufunguzi amewaambia wajumbe hao kwamba, watapata fursa ya kukutana na Baba Mtakatifu Francisko hapo tarehe 22 Januari 2014 wakati wa Katekesi yake. Kanisa linatambua mchango mkubwa unaoendelea kutolewa na Utume wa Bahari kama chombo cha Uinjilishaji, kinachotekeleza utume na dhamana yake kwa njia ya safari, wongofu wa ndani na majiundo makini ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Utume wa Bahari unaongozwa na Mafundisho Jamii ya Kanisa.

Kardinali Vegliò anahimiza umuhimu wa kujenga na kudumisha ari na moyo wa kiekumene katika ulimwengu wa bahari, kwa kushirikiana na Wakristo kutoka katika Madhehebu mbali mbali; utume ambao unapaswa kimsingi kuratibiwa na Idara za Utume wa Bahari kutoka katika Mabaraza ya Maaskofu Katoliki pamoja na kushirikiana na Maaskofu mahalia.

Shughuli za bahari zinazidi kuongezeka na kubadilika kwa haraka sana katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Wafanyabiashara wanataka kupata faida kubwa kwa kubana matumizi na kuongeza tija na ufanisi. Wanachama wa Utume wa Bahari wanapaswa kushirikiana na kushikamana kwa dhati, ili kutumia vyema rasilimali fedha na watu iliyopo kwa kujenga na kukuza tija na weledi katika sekta ya biashara baharini lakini kwa namna ya pekee katika kitengo cha uvuvi.

Utume wa Bahari anasema Kardinali Vegliò unapaswa kuendelea kuhamasishwa kwa ari, bidii na uvumilivu mkubwa pengine bado haujafahamika kwa wengi ndani ya Kanisa. Kipaumbele cha kwanza kiwe ni kwa ajili ya wavuvi na familia zao. Hapa kuna haja ya kuweka mikakati ya kichungaji kwa ajili ya kulisaidia kundi hili ambalo linaendelea kuteseka baharini, lakini lenye mafao makubwa kwa maisha na uchumi wa kimataifa.

Kwa upande wake Askofu mkuu Joseph Kalathiparambili, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, amewatambulisha wawezeshaji wakuu katika mkutano huu. Kwavile mkutano huu unafanyika katika Juma la kuombea Umoja wa Wakristo, hata wajumbe wa Utume wa Bahari katika mkutano huu watashiriki kwa namna yao.

Wajumbe pamoja na mambo mengine waanapembua kwa kina na mapana athari za utumwa mamboleo; dhuluma na nyanyaso kwa mabaharia na wavuvi ambao mara kwa mara wanatekwa nyara baharini.








All the contents on this site are copyrighted ©.