Jubilee ya Miaka 150 ya Uinjilishaji endelevu Jimbo Katoliki Zanzibar
Jimbo Katoliki la Zanzibar, Jumapili tarehe 19 Januari 2014 limeadhimisha kilele cha
Jubilee ya Miaka 150 ya Uinjilishaji endelevu Visiwani Zanzibar, kwa Ibada ya Misa
Takatifu, iliyoongozwa na Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar
es Salaam na kuhudhuriwa na Idadi kubwa ya Maaskofu Katoliki Tanzania, Wawakilishi
wa Makanisa na Dini mbali mbali kutoka ndani na nje ya Visiwa vya Zanzibar.
Ibada
hii ya Misa Takatifu ilikuwa pia ni kilele cha kufunga Maadhimisho ya Mwaka wa Imani
uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI na kufungwa rasmi
na Papa Francisko wakati wa Sherehe ya Kristo Mfalme wa Ulimwengu. Jimbo Katoliki
la Zanzibar limesherehekea na kufunga rasmi Maadhimisho ya Siku kuu ya Utoto wa haki
na amani.
Askofu Augustine Shao wa Jimbo Katoliki Zanzibar anabainisha kwamba,
tangu mwanzo wa uwepo wake, Kanisa Katoliki limeendelea kuwa ni mdau mkubwa wa maendeleo
endelevu ya wananchi wa Zanzibar katika ujumla wao. Limechangia kwa hali na mali katika
sera na mikakati ya maboresho katika sekta ya elimu, afya na maendeleo ya umma. Hii
ni dhana inayojionesha kwa Makanisa mengi yanayoendelea kutangaza Habari Njema ya
Wokovu nchini Tanzania.
Askofu Shao anaendelea kueleza kwamba, tangu mwanzo
wa Uinjilishaji, Kanisa lilitoa kipaumbele cha kwanza kwa mikakati ya elimu na afya,
kama sehemu ya mchakato wa ukombozi wa mtu mzima: kiroho na kimwili. Mikakati hii
inaendelea kufanyiwa kazi hata baada ya Miaka 50 ya Mapinduzi Zanzibar.
Kanisa
bado linatoa huduma ya kutukuka katika sekta ya elimu na afya kama walivyofanya Wamissionari
wa Shirika la Roho Mtakatifu walipofika kwa mara ya kwanza Visiwani Zanzibar, kunako
mwaka 1863. Jimbo Katoliki la Zanzibar linaundwa na Parokia 8 zenye jumla ya Wakristo
11, 600. Kuna Parokia sita Kisiwani Unguja na Parokia mbili ziko Kisiwani Pemba.
Ukristo
ulianza kuingia Zanzibar kunako Karne ya kumi na tano, juhudi hizi hazikuzaa matunda
na Wamissionari wa Shirika la Roho Mtakatifu wakarudi tena Visiwani hapo kwa kasi
na nguvu mpya, miaka 150 iliyopita, leo Jimbo Katoliki Zanzibar linaadhimisha Jubilee
ya miaka 150 ya Uinjilishaji endelevu. Kardinali Polycarp Pengo katika mahubiri yake,
amewataka waamini kulinda na kudumisha matunda ya kazi za Uinjilishaji endelevu yaliyopatikana
katika kipindi cha Miaka 150 iliyopita hasa katika masuala ya imani, elimu na afya.
Zanzibar ni lango la Imani ya Kikristo Afrika ya Mashariki.
Askofu Augustino
Shao kwa upande wake anasema, watanzania kwa miaka mingi walikuwa na utamaduni wa
kuheshimiana, kuvumiliana na kuthaminiana hata katika tofauti zao za kidini, kikabila
na kiimani. Uvulimivu na mshikamano wa kitaifa unaanza kuyeyuka taratibu; lakini jambo
la msingi kwa watanzania ni kukataa kugawanywa kwa misingi ya udini, ukabila na siasa.
Itakumbukwa
kwamba, hivi karibuni Familia ya Mungu nchini Tanzania imeadhimisha Jubilee ya Miaka
150 ya Uinjilishaji nchini Tanzania sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliofungwa
mjini Bagamoyo, Jimbo Katoliki la Morogoro na kuhudhuriwa na umati mkubwa wa wawakilishi
kutoka Majimbo yanayounda Kanisa Katoliki Tanzania.
Baraza la Maaskofu Katoliki
Tanzania. Linatarajia kufanya Hija ya Kitume mjini Vatican kuanzia tarehe 4 hadi tarehe
7 Aprili, 2014. Baraza la Maaskofu litapata fursa ya kuonana na kuzungumza na Baba
Mtakatifu Francisko. Historia inaonesha kwamba, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania
kwa mara ya mwisho lilifanya Hija ya Kitume Mjini Vatican wakati wa uongozi wa Mwenyeheri
Yohane Paulo II kunako mwaka 1987 na Mwaka 1996.
Mwezi Machi, 2005 Mwenyeheri
Yohane Paulo II alikuwa amelazwa Hospitalini Gemelli, akabahatika kuonana na Kardinali
Polycarp Pengo Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam pamoja na Askofu Severinus
Niwemugizi aliyekuwa Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kwa wakati huo.
Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili akawakabidhi ujumbe wake kwa Maandishi. Tarehe 2 Aprili
2004, Papa Yohane Paulo II akafariki dunia.
Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania
halikubahatika kufanya Hija ya Kitume Mjini Vatican wakati wa uongozi wa Baba Mtakatifu
mstaafu Benedikto VXI.