Zingatieni kanuni maadili kwa kuwaheshimu na kuwathamini watu ambao ndio walengwa
wa matangazo ya Radio Na Luninga
Kampuni ya Televisheni ya Taifa nchini Italia, RAI imeadhimisha Miaka 90 tangu ilipoanza
kurusha matangazo yake kwa njia ya radio na miaka 70 ya matangazo kwa njia ya Luninga
kwa Ibada ya Misa Takatifu iliyoadhimishwa kwenye Ukumbi wa Paulo VI na kuongozwa
na Kardinali angelo Comastri, Makamu Askofu, mjini Vatican. Ibada hii imehudhuriwa
pia na wafanyakazi wa sekta ya mawasiliano kutoka nchini Italia kama kielelezo cha
ushirikiano wa dhati kati ya RAI na Vatican katika huduma ya mawasiliano ya Jamii
ndani na nje ya Italia.
Baba Mtakatifu Francisko ameipongeza taasisi hii kwa
ushirikiano wa dhati katika masuala ya mawasiliano yanayomwezesha Khalifa wa Mtakatifu
Petro kuwafikia wananchi wengi wa Italia na hata wale ambao wako nje ya Italia. Kuna
ushirikiano mkubwa kati ya RAI, Radio Vatican na Kituo cha Televisheni cha Vatican,
CTV. Kwa njia hii, RAI imeendelea kutoa huduma ya matangazo kwa hadhara na hivyo kuiwezesha
kufuatilia matukio mbali mbali ndani na nje ya Italia.
Kati ya matukio yaliyotajwa
na Baba Mtakatifu Francisko ni pamoja na: Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican,
miaka hamsini iliyopita; uchaguzi wa viongozi wakuu wa Kanisa; maziko ya Mwenyeheri
Yohane Paulo II bila kusahau Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 2000 ya Ukristo pamoja
na hija mbali mbali za kichungaji zinazofanywa na Khalifa wa Mtakatifu Petro nchini
Italia.
Baba Mtakatifu anasema, miaka ya 1950 na 1960, kilikuwa ni kipindi
cha maendeleo makubwa kwa RAI, kwani taasisi hii ilifanikiwa kurusha matangazo yake
nchi nzima; ikajikita katika mafunzo ya wafanyakazi wake pamoja na kuboresha matangazo
ambayo yanamgusa mtu mzima: kiroho na kimwili. Amegusia Sinema nyingi ambazo zimetengenezwa
na RAI na kubaki kuwa na umaarufu wake katika historia. RAI imeshuhudia mabadiliko
makubwa katika maisha na historia ya maisha ya wananchi wa Italia, kwa kusaidia mchakato
wa ujenzi wa umoja wa kitaifa kwa njia ya lugha ya Kiitalia.
Baba Mtakatifu
anawashukuru viongozi na wafanyakazi wa RAI na anawataka kujikita katika uwajibikaji
mpana zaidi kwa siku za usoni, kwa kutambua kwamba, kazi yao ni kwa ajili ya huduma
na mafao ya Jamii. Wafanyakazi wote wa RAI ni wadau muhimu sana katika mchakato wa
elimu inayotoa habari, inayofurahisha na kuburudisha; inayofunda na kuwajibisha. Huu
ni wajibu msingi unaopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza na wafanyakazi wote katika
huduma za kijamii.
Baba Mtakatifu Francisko anakazia kanuni maadili katika
mawasiliano ya jamii, kwa kuwaheshimu na kuwathamini watu, ambao kimsingi ni walengwa
wa matangazo yanayotolewa na RAI. Kila mtu katika nafasi yake anawajibika kutoa kipaumbele
cha kwanza kwa kanuni maadili. Baba Mtakatifu amewatakia kheri na baraka tele katika
Kipindi cha Mwaka 2014. Anawataka wafanye kazi kwa bidii, juhudi na maarifa; daima
wakiwa na imani na matumaini, ili kuweza kuionjesha Jamii ambayo ina kiu sana na tunu
hizi msingi za maisha.