Askofu mstaafu Paolo de Nicolo, Jumapili tarehe 19 Januari 2014 anatarajiwa kutoa
daraja takatifu la Ushemasi kwa Mafrateri wawili wa Shirika la Warosmini, kwenye Kanisa
kuu la Giovanni Porta Latina, majira ya saa 10:00 Jioni kwa saa za Ulaya. Mashemasi
wateule ni Fulgence Oisso na Richard Mwazia kutoka Jimbo Katoliki la Machakosi, Kenya.
Ifuatayo ni historia fupi ya Frt. Fulgence Oisso.
Naitwa Frate
Fulgence Oisso. Nimezaliwa katika Parokia ya Useri, Jimbo Katoliki la Moshi, Tanzania.
Ninatoka katika Familia ya watoto saba na mimi nikiwa ni mtoto wa sita. Nililelewa
katika misingi ya kikristo tangu nikiwa mdogo. Mama alipenda sana kunipeleka Kanisani
na ndipo nilipotamani kuwa kasisi kabla hata sijaanza shule, pia Bibi mzaa mama alikuwa
akitufundisha sala mbali mbali hasa sala za jioni, asubuhi na kabla ya kula na kisha
kula. Wazazi walikuwa wakinihimiza kama ninataka kuwa Padre basi ni sharti niwe mtu
wa sala na mtoto mwenye nidhamu na bidii ya kazi. Wito.
Nilipofika darasa
la nne nilijiunga na kikundi cha Mtakatifu Aloisi, kinachotoa huduma ya kutumikia
Kanisani. Nilikuwa pia ni mwanachama wa Chama cha Wito, kitalu cha kulelea miito mbali
mbali ndani ya kanisa. Hapa nilijifunza mambo mengi, kiasi cha kuwa na hamu ya kumtumikia
Mungu Altareni kama Padre.
Nilipomaliza darasa la saba, nilijiunga na Seminari
Ndogo ya Uru, inayoendeshwa na Shirika la Mitume wa Yesu, kwa kidato cha kwanza hadi
cha nne. Nilipohitimu kidato cha nne nilitaka kujiunga na Umbwe Shule ya Sekondari
ila moyo haukunisukuma sana kwenda huko kwani nilikuwa nimeomba kujiunga na Shirika
la kazi ya Roho Mtakatifu (Holy Ghost Fathers) walinikubali na niliweza kumalizia
masomo yangu ya kidato cha Tano na Sita katika Seminari ya Usa river Arusha, Jimbo
kuu la Arusha.
Baada ya kidato cha sita nililiwafahamu Warosmini kupitia kwa
mwanafunzi mwenzangu na niliandika barua ya maombi ila sikupata jibu mapema. Nilikuwa
nimeomba kujiunga na mashirika mengine na walinikubali ila mwishoni Warosmini walinijibu.
Nilienda kukaa nao kwa wiki moja na nilivutiwa na kazi na maisha yao kwa ujumla, baada
ya kutembelea sehemu mbali mbali wanazofanya kazi.
Nilijiunga na Warosmini
kunako mwaka 2003 kwa malezi huko Lushoto, Jimbo Katoliki la Tanga. Malezi yalichukua
miaka mitatu: kama mpostulanti na mnovisi. Baada ya hapo nilianza masomo ya Falsafa
nchini Kenya katika Chuo cha Waconsolata kwa miaka mitatu na baadaye nilitumwa nchini
Italia kwa masomo ya taalimungu katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterani. Kwa sasa
niko mwaka wa mwisho. Miaka hii ya malezi na majiundo ya Kipadre nimekuwa nikifanya
mazoezi ya uchungaji sehemu mbali mbali kama, Hospitalini, kukaa na watoto wanaoishi
katika mazingira hatarishi, kutembelea wafungwa na wazee na pia kusaidiana Parokiani.
Mpaka
sasa nafurahia maisha niliyochagua mwenyewe hasa katika Shirika la Warosmini na kuwa
mrosmini baada ya kuweka Nadhiri za Daima mwaka 2012 na sasa namshukuru Mungu ninapokaribia
kupokea Daraja Takatifu la ushemasi hapo tarehe 19 Januari 2014. Na yote yawezekana
kwa sala na kuwa na matumaini. Napenda kuwashukuru wazazi na walezi wangu na wale
wote walionisaidia kwa hali na mali mpaka nikafikia hatua hii. Mungu azidi kuwabariki
na kuwajalia mema katika maisha na kazi zao.
Natambua kwamba, ushehasi ni huduma
kwa Neno la Mungu, linalopaswa kutangazwa kwa njia ya ushuhuda wa maisha. Ni daraja
la huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, watu wanaopaswa
kuonjeshwa Injili ya Furaha kwa njia ya matendo ya huruma na upendo. Shemasi ni mhudumu
wa Sakramenti za Kanisa kadiri ya daraja hili ndani ya Kanisa: kwa kulisha na kuimarisha
Imani ya Familia ya Mungu.
Shemasi anapaswa kuwa ni mtu wa sala na Ibada;
anapaswa kuwa ni shahidi wa utakatifu wa maisha unaofumbatwa katika Mashauri ya Kiinjili.
Ni matumaini yangu kwamba, mtaendelea kunisindikiza katika maisha na utume wangu kama
Shemasi wa Shirika la Warosmini.