Tafakari ya neno la Mungu, Jumapili ya Pili ya Kipindi cha Mwaka wa A wa Kanisa
Mpendwa msikilizaji wa kipindi tafakari masomo Dominika, Dominika iliyopita tulimaliza
kipindi na shamrashamra za Noeli na tulianza kipindi cha kawaida cha mwaka wa Kanisa.
Ndiyo kusema sasa tunatafakari masomo Dominika ya II ya mwaka A.
Masomo Dominika
hii: Somo la kwanza tunalipata katika Kitabu cha Isaya 49:3, 5-6. Somo II 1Kor. 1:1-3
na Injili Yn. 1:29-34 Mwaliko ni kutafakari na kuishi WITO WA KIKRISTO. Nabii Isaya
yuko katika ndoto na anapokea wito wa Mungu kwa ajili ya taifa lake la Israeli. Isaya
anaalikwa kutegemea nguvu za Mungu katika shughuli hiyo ya wito kwa ajili ya kuwarejeza
watu wa Israeli katika amani na usalama. Mungu anamwahidia kuwa atakuwa nuru ya mataifa
na hata miisho ya dunia. Tuko pia katika Juma la kuombea Umoja wa Wakristo, linaloongozwa
na kauli mbiu ”Je, Kristo amegawanyika?”
Mpendwa mwana tafakari, ni vema na
inafaa kujiuliza huyu mtumishi wa Mungu ni nani? Katika Agano la Kale tunakutana na
sura ya mtumishi katika kitabu cha Nabii Yeremia 1:5 na hapa tunaona Mungu akimwambia
Nabii Yeremia yakuwa alimteua tangu hajatungwa mimba na amemteua kuwa nabii kwa mataifa.
Mwinjili Lk 1:15 anamtaja mtumishi ambaye hatakunywa divai wala kileo, na atajazwa
Roho Mtakatifu tangu tumboni mwa mama yake. Fundisho hili linakuja wakati Waisraeli
wako utumwani Babeli wanateseka na kwa njia ya nabii, Mungu anatangaza uhuru watakaoupata
kwa njia ya mtumishi wa Mungu.
Kwa hakika aguo hili linakamilika katika Masiha,
Yesu Mnazareti aliyezaliwa katika kipindi cha Noeli. Hawa manabii waliotangulia ambao
walikuwa vyombo vyake wanatoa picha ya Masiha ambaye atatenda kadiri ya mpango wa
Baba yake. Mpendwa msikilizaji kazi yako hivi leo pamoja na jumuiya na familia ni
kuwa mtumishi mwaminifu kwa ajili ya kupeleka habari njema ya wokovu kwa mataifa.
Mtume
Paulo akiwaandikia Wakorinto anawakumbusha juu ya wito wake na wito wa Sosthene na
hasa ule wito mkuu wa kuwa watakatifu. Katika barua yake hiyo anaonesha kazi ya wito
ikiwa ni kwa ajili ya kuwatakia wengine yaani taifa la Mungu mema yote ya mbinguni.
Ndiyo kusema mpendwa msikilizaji wito ni kwa ajili ya kufariji na kushona mahali ambapo
pamechanika katika harakati ya kuuendea uhuru kamili wa wana wa Mungu. Yafaa kukumbua
kuwa wakati Paulo anawaandikia Wakorinto walikuwa katika ugomvi na ukosefu wa utulivu
katika jumuiya yao. Akitangaza kwanza mamlaka aliyokabidhiwa na Kristo anawakemea
na kuwambia nini maana ya kuwa mkristu. Kwa hakika ni kutumikia kwa furaha na kutenda
kadiri ya matakwa ya Injili. Umoja kamili unajikita katika mafundisho ya Kristo ndiyo
msingi wa maisha ya wito wetu.
Katika Injili nabii Yohane Mbatizaji anakiri
ukuu wa Masiha akisema yeye ndiye aliyenipeleka na hivi ni kabla yangu na kabla ya
yote. Ndiyo kusema Yohane Mbatizaji yuko tayari kushuka kwa maana wito ni ule wa kuonesha
kwa mataifa yakwamba Kristu ni Mwanakondoo wa Mungu aondoaye dhambi za ulimwengu.
Kwa hakika ile sifa yakwamba nilikuchagua kabla ya kutunga mimba haimwangukii Masiha
kama wale manabii wa Agano la Kale, ndiyo maana basi Yohane anamtambulisha kama Mwanakondoo
wa Mungu, ambaye utume wake ni kuondoa dhambi za dunia, dhambi zetu sote.
Kwa
kutumia Mwanakondoo wa Mungu, anataka kuturudisha nyuma kutafakari ule usiku mtakatifu
Waisraeli walipotoka Misri. Tunakumbuka kila familia ilichinja mwanakondoo na ilitumia
damu kupaka milango na ikawa ni alama kwa wokovu wao. Ni kwa mantiki hiyo basi Yohane
mwinjili anaweka mbele yetu Yesu atakaye toa maisha yake kwa njia ya kumwaga damu
yake takatifu. Mtumishi huyu atateswa lakini kwa njia ya mateso yake atauokoa ulimwengu.
Mpendwa msikilizaji Yohane Mbatizaji analo jambo la kutuambia yakwamba hakumfahamu
Masiha, hii ni hatua nzuri ambayo hivi leo wakatekumeni wanaanza nayo. Hawajui chochote
lakini Mungu huwaita na polepole humtambua Bwana. Kama ambavyo nabii alibadilisha
mwono wake kwa Masiha ndivyo ambavyo mkatekumeni anavyoalikwa kusafiri polepole katika
njia ya utambuzi mpaka kilima kitakatifu. Mpendwa msikilizaji, twaweza kuzama katika
ukatekumeni na kusahau kwamba hata sisi tunao wajibu wa kuendelea kutafuta maana ya
wito wetu na hasa kutambua Masiha wetu si yule mfalme mkandamizaji bali mwenye huruma
na hasa akiwatumikia wengine. Ndiyo kusema wito wetu tukimfuata yeye ni kuwa watumishi
waaminifu wa Injili yake.
Mtazame Yohane Mbatizaji anakiri yakwamba, yeye mwenyewe
hakumfahamu na ndiyo maana alitumwa akamshuhudie mbele ya mataifa kabla na katika
udogo wake huo alitumwa akawabatize watu kwa maji ili kujiandaa kumpokea Masiha. Tena
zaidi ya hilo anasema anapokuja habatizi kwa maji bali kwa moto na Roho Mtakatifu.
Hii ni alama ya Masiha alama ambayo yamtofautisha toka Yohane Mbatizaji. Huyu kadiri
ya Yohane Mbatizaji ni Mwana wa Mungu. Basi kukiri kwa nabii kutusaidie kuwa wanyenyekevu
katika maisha yetu na hapo itakuwa rahisi kuhubiri habari njema.
Nikutakie
furaha na amani katika kuwa mtumishi wa Mungu na hivi kuwa chombo cha mapatano na
wokovu. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya
C.PP.S.