Mshikamano wa kidugu na kiimani na wananchi wanaoishi Nchi Takatifu
Maaskofu kutoka Ulaya, Marekani na Afrika ya Kusini, hivi karibuni wamehitimisha hija
ya kiroho Nchi Takatifu, kama kielelezo cha mshikamano wa imani na mapendo kwa wananchi
wanaoishi katika Nchi Takatifu pamoja na kuwatia moyo Wakristo wanaoendelea kuteseka
na kunyanyasika kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.
Mshikamano
huu ulianzishwa kunako Mwaka 1998 na kila mwaka kuanzia tarehe 11 hadi tarehe 16 Januari,
Maaskofu wanafanya hija ya kiroho katika Nchi Takatifu. Maaskofu wanasema, Waisraeli
na Wapalestina wana kiu na njaa ya kuona kuwa haki, amani na utulivu vinatawala tena
katika mipaka ya nchi zao.
Maaskofu wanawataka viongozi wa Israeli na Palestina
kuonesha utashi wa kisiasa kwa kuwajengea wanachi wao matumaini na kwamba, pasiwepo
na mtu ambaye atakuwa ni kikwazo cha majadiliano ya amani na utulivu!
Maaskofu
wanasema, wameridhishwa na uwepo wa Jumuiya za Kikristo hata katika udogo wake huko
Nchi Takatifu. Wanaendelea kuwatia moyo na ari ya kusonga mbele pasi na kukata tamaa
na kwamba, wakristo sehemu mbali mbali za dunia wataendelea kuwaunga mkono katika
mchakato wa maendeleo endelevu kwa kuwasaidia katika kugharimia sekta ya elimu na
mapambano dhidi ya umaskini. Hizi ni juhudi zinazowalenga wananchi wote wanaoishi
katika Nchi Takatifu bila ubaguzi wa kidini.
Maaskofu wanawaalika Wakristo
katika Nchi Takatifu kuendelea kutolea ushuhuda katika imani, matumaini na mapendo
na kwamba, mapendo ya dhati ni chemchemi ya matumaini mapya kwa wale waliokata tamaa.
Ni matumaini haya yanayowasukuma wadau mbali mbali kuendelea kuunga mkono mchakato
wa majadiliano ya amani, ili kweli amani ya kudumu iweze kupatikana na kudumishwa
katika Nchi Takatifu.
Hii ni amani inayopaswa kujikita katika haki na usawa
kati ya Waisraeli na Wapalestina. Ukanda wa Ghaza ni kashfa na ukosefu wa haki msingi
za binadamu; jambo linalohitaji kupatiwa ufumbuzi na Jumuiya ya Kimataifa. Maaskofu
wanawaomba wanasiasa na wapenda amani duniani kusaidia maboresho ya maisha katika
Ukanda wa Ghaza, ili watu waweze kupata mahitaji yao msingi kwa gharama nafuu.
Maaskofu
wanaonesha matumaini makubwa kwa Hija ya Sala itakayofanywa na Baba Mtakatifu Francisko
katika Nchi Takatifu, mwezi Mei, mwaka huu. Itakuwa ni fursa ya kuimarisha imani na
matumaini katika Nchi Takatifu. Wanaamini kwamba, amani ya kudumu ni jambo linalowezekana
kabisa.