Diplomasia haina budi kujikita katika utu na heshima ya binadamu!
Kardinali mteule Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican katika mahojiano maalum na
Kituo cha Televisheni cha Vatican, CTV anasema kwamba, sera ya kidiplomasia na ushirikiano
wa kimataifa inayotekelezwa na Vatican inajikita katika kujali, kuthamini, kulinda
na kudumisha utu na heshima ya binadamu. Mwanadamu na mahitaji yake msingi: kiroho
na kimwili yanapaswa kushughulikiwa kikamilifu katika sera na mikakati ya maendeleo
endelevu.
Hii ni changamoto ya kujenga na kudumisha mshikamano wa upendo unaongozwa
na kanuni auni hasa katika ulimwengu huu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na
teknolojia ambako: vita, kinzani, migogoro, njaa na magonjwa yanaonekana kuwa ni mambo
ya kawaida kabisa katika maisha ya mwanadamu. Katika hali kama hii inayoonesha kinzani,
kuna haja kwa binadamu kupewa kipaumbele cha kwanza.
Kardinali mteule Parolin
anasema, huduma ya Kidiplomasia inayotolewa na Vatican ni nyeti, yenye madai makubwa
na uwajibikaji makini kwa namna ya pekee katika uongozi wa Baba Mtakatifu Francisko
ambaye kwa sasa anafungua ukurasa mpya wa maisha na utume wa Kanisa. Changamoto na
kipaumbele cha pekee kwa wakati huu ni kuhakikisha kwamba, Kanisa linatoka kifua mbele
kutangaza Injili ya Furaha kwa kujikita katika dhana ya Kanisa ambalo ni la Kimissionari
kwani kila Mkristo anaalikwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya ushuhuda
wa maisha yake.
Kardinali mteule Parolin anasema kwamba, diplomasia ya Baba
Mtakatifu Francisko inajikita kwa namna ya pekee katika kanuni maadili inayosimikwa
katika mshikamano wa kidugu kwa ajili ya mafao ya wengi, jambo ambalo wengine wanadhani
kwamba, ni ndoto ya kufikirika katika ulimwengu ambao umesheheni ubinafsi na uchu
wa mali na madaraka.
Mara kwa mara Baba Mtakatifu ametoa mwaliko kwa ajili
ya ujenzi na udumifu wa misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano, lakini pengine
inaonekana kana kwamba, kilio hiki cha Baba Mtakatifu hakina tena msikilizaji. Ukweli
wa mambo ni kwamba, watu wana kiu na njaa ya haki, amani, upendo na mshikamano ambao
kimsingi ni kikolezo cha maendeleo endelevu yanayozingatia mahitaji msingi ya binadamu
wote. Kuna mikakati inayoendelea kufanywa na Jumuiya ya Kimataifa katika ujenzi wa
haki na amani sehemu mbali mbali za dunia.
Kardinali mteule Pietro Parolin,
Katibu mkuu wa Vatican anaendelea kufafanua kwamba, diplomasia na mikakati ya ushirikiano
wa kimataifa haina budi kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu na mahitaji yake
msingi. Huu ndio mkakati unaofanyiwa kazi na Baba Mtakatifu Francisko kwa nyakati
hizi. Mwanadamu apewe umuhimu unaostahili kwa kujenga na kudumisha pia mshikamano
wa dhati na maskini pamoja na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kutokana
na hali yao ya maisha.
Watu wajenge na kudumisha utamaduni wa kukutana ili
kuondokana na ubinafsi unaowafanya watu wengi kuishi kana kwamba, wako kisiwani bila
ya kuwa na mahusiano ya kidugu na jirani zao. Mshikamano wa kidugu unapania kudumisha
utamaduni unaojali na kuguswa na mahitaji ya jirani. Watu wasiridhike na idadi, bali
watambue kwamba, kila mtu mmoja mmoja anathamani kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu.
Ndiyo
maana hata wakati Baba Mtakatifu anapokutana na makundi makubwa ya watu, lakini hata
katika makundi haya, bado kuna watu anawaita kwa majina kuonesha kwamba, anawatambua
na kuwajali. Kwa maneno mengine, anasema Kardinali mteule Parolin, mahusiano ya kidiplomasia
hayana budi kusimikwa katika fadhila ya upendo; majadiliano ya kina yanayosimikwa
katika ukweli na uwazi; kuna haja ya kuheshimiana na kujaliana hata katika tofauti
msingi za kibinadamu.
Kamwe tofauti hizi zisiwe ni chanzo cha vita, vurugu
na kinzani za kisiasa, kijamii, kiuchumi na kikabila, bali utajiri unaopania kujenga
na kudumisha mafao ya wengi. Huu ndio mwelekeo sahihi wa diplomasia inayopigiwa debe
na Vaticani