Wakristo msikumbatie malimwengu na kulitema neno la Mungu
Wakristo watambue kwamba, zawadi ya kuwa ni Watoto wa Mungu inawawajibisha kulisoma,
kulitafakari na kulimwilisha Neno la Mungu katika maisha yao na wala si kufanya vinginevyo
kana kwamba, hakuna Mwenyezi Mungu; kwa kutenda kadiri ya matakwa yao binafsi pamoja
na kukumbatia malimwengu.
Haya ndiyo yaliyowatokea Waisrael katika Agano la
Kale kwa kumkataa Mwenyezi Mungu na kutaka kukumbatia malimwengu kwa kuiga mtindo
wa maisha kutoka kwa nchi jirani. Waisraeli walimkataa Nabii Samueli wakadhani wanamkataa
yeye tu, lakini Mwenyezi Mungu aliwakumbusha kwamba, walikuwa wanamkataa hata Yeye
ambaye ndiye Mungu wao.
Baba Mtakatifu katika mahubiri yake Ijumaa, tarehe
17 Januari 2014 kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha anasema kwamba, Wazee wa Waisraeli,
walikuwa wanatema upendo, huruma na ukarimu kutoka kwa Mwenyezi Mungu; uliomsukuma
hata akawateuwa kuwa ni Taifa takatifu na wateule wa Mungu. Hii ni changamoto kwa
Wakristo kuwa waaminifu kwa Mwenyezi Mungu na kamwe wasikubali kishawishi cha kumkana
na kutaka kuyakumbatia malimwengu.
Wakristo waendelee kujishikamanisha na
Mwenyezi Mungu kwa kufuata sheria na amri zake. Neno la Mungu liwe ni dira na mwongozo
wa maisha ya Mkristo, kamwe wasijisie wanyonge mbele ya watu wa mataifa! Wao ni wana
wateule wa Mwenyezi Mungu, kumbe wanapaswa kutoka kifua mbele kushuhudia imani hii
kwa njia ya matendo adili. Walegeze mioyo yao, tayari kulipokea na kulimwilisha Neno
la Mungu katika uhalisia wa maisha.
Wakristo wajitahidi kuiga mfano wa Bikira
Maria aliyekuwa Tabernakulo ya kwanza ya Neno la Mungu, aliyefanyika Mwili, Mama aliyethubutu
kuhifadhi na kulitafakari Neno la Mungu katika hija ya maisha yake hapa duniani. Waamini
waoneshe unyenyekevu katika maisha ya kiroho, tayari kupokea neema na baraka kutoka
kwa Mwenyezi Mungu.