UNDP: Tanzania yaongoza katika Mpango wa Majaribio wa Mageuzi wa UN
Tanzania imefanya vizuri zaidi na kuonyesha mafanikio zaidi kuliko nchi nyingine yoyote
duniani kati ya nchi nane ambazo zilikuwa zinashiriki katika Mpango wa Majaribio wa
Kuuwezesha Mfumo wa Umoja wa Mataifa Kufanya Kazi kwa Pamoja wa Delivering as One
ambao sasa umepanuliwa kushirikisha nchi nyingi zaidi baada ya kuonyesha faida kubwa.
Hayo
yamesemwa Jumanne, Januari 14, 2014, na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo
la Umoja wa Mataifa (UNDP) na Mratibu Mkazi wa Shughuli za Umoja wa Mataifa (UN Resident
Coordinator) katika Tanzania, Dk. Alberic Kacou wakati alipokutana na kufanya mazungumzo
na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, Ikulu, Dar es
Salaam.
Dk. Kacou ambaye alikuwa anaagana na Rais Kikwete baada ya kuitumikia
UN katika Tanzania kwa miaka minne unusu ameondoka nchini baadaye leo adhuhuri kwenda
Makao Makuu ya UN, New York, Marekani, ambako atakuwa Mkuu wa Utawala (Chief of Staff)
na Mkurugenzi wa Ofisi ya Utawala na uendeshaji wa UNDP.
Katika mazungumzo
yao na Rais Kikwete, Dk. Kacou amemwelezea Rais Kikwete mafanikio ambayo yaliyopatikana
katika mahusiano ya UN/UNDP na Tanzania katika miaka minne iliyopita ikiwa ni pamoja
na shirika hilo la Umoja wa Mataifa kuunga mkono kifedha na kiufundi shughuli za uchaguzi
mkuu katika Tanzania.
Kuhusu mpango wa Delivering as One ambao unalenga kuuwezesha
Umoja wa Mataifa kuwa na ufanisi zaidi na kutoa huduma kwa haraka na ubora zaidi na
kupunguza matumizi, Dk. Kacou amemwambia Rais Kikwete: “Tanzania imetoa mchango mkubwa
sana katika mageuzi yanayofanyika ndani ya UN ya Delivering as One kiasi cha kwamba
nchi yako, Mheshimiwa Rais, imeongoza miongoni mwa nchi nane ambako majaribio ya mfumo
huo mpya yalikuwa yanafanyika. Serikali yake imeonyesha kiwango cha juu sana cha kuyakubali
na kuyaongoza majaribio hayo. Matokeo yake ni kwamba mpango huo sasa unapanuliwa na
kuanza kufanya kazi katika nchi nyingine 45 duniani.”
Dk. Kacou amesifia sana
amani na utulivu wa Tanzania na kusema kuwa sifa hizo ndizo zinaendelea kuifanya Tanzania
nchi ya mfano katika eneo ambako amani na utulivu ni tunu za nadra sana.
Naye
Rais Kikwete amemwambia Dk. Kacou: “Tunakushukuru sana. Wakati wa uongozi wako, uhusiano
wa Tanzania na UN umeimarika sana na nchi yetu imenufaika sana na hali hiyo ya kuimarika
kwa uhusiano. Uongozi wako umekuwa wa mfano kabisa na ni matarajio yetu kuwa mrithi
wako ataendeleza mazuri mengi ambayo unayaacha nyuma.”
Ameongeza Rais Kikwete:
“Umekuwa mmoja wa viongozi bora zaidi wa UNDP katika nchi yetu. Chini yako, UNDP imesaidia
kuleta uwiano bora zaidi baina ya taasisi mbali mbali za kimataifa na za Umoja wa
mataifa. Chini yako, UNDP imekuwa ni sauti ya busara katika dunia ambako busara ina
mipaka yake.”
“Tunathamini sana mchango wako katika maendeleo ya Tanzania.
Tunathamini juhudi zako na mafanikio yako katika miaka yako minne ya uongozi bora
wa UNDP katika nchi yetu. Tunakutakia heri na mafanikio makubwa katika kazi yako mpya
na katika maisha yako ya baadaye. Umethibtibisha kuwa wewe ni binadamu bora na ofisa
bora wa Umoja wa Mataifa.”