2014-01-16 08:43:31

Parokia ya Moyo Mtakatifu ya Yesu inajiandaa kumpokea na kuadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu na Papa Francisko! Yaani, we acha tu!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili jioni tarehe 19 Januari 2014, Siku ya Wahamiaji na Wakimbizi Duniani, anatarajiwa kutembelea na kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Parokia ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, iliyoko Jimboni Roma. Baba Mtakatifu atapata fursa ya kukutana na Familia ya Mungu, Parokiani hapo pamoja na maskini, wahamiaji na wakimbizi wanaohudumiwa kila siku Parokiani hapo kama kielelezo cha upendo na mshikamano na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Padre Valerio Baresi, Paroko wa Parokia ya Moyo Mtakatifu wa Yesu iliyojengwa na Mtakatifu Yohane Bosco kunako Mwaka 1881 na kuwekwa chini ya usimamizi wa Shirika la Wasalesiani, anasema, walimwandikia barua Baba Mtakatifu wakimwomba atembelee Parokia yao kwani ni kati ya Parokia ambazo ziko pembezoni mwa Jiji la Roma, kama kielelezo cha upendo na mshikamano na maskini, wanaotafuta kuonja huruma na upendo kutoka kwa Kristo na Kanisa lake.

Baba Mtakatifu akiwa Parokiani hapo atapata nafasi ya kuwaungamisha baadhi ya waamini watakaokuwa wamejiandaa kwa ajili ya kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani zao, changamoto ya kuthamini na kupokea Sakramenti ya Upatanisho, ili kuonja huruma na upendo wa Mungu. Waamini wanaendelea kujiandaa kiroho na kimwili ili kukutana na hatimaye kuadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu na Baba Mtakatifu Francisko! Wanasema, Parokiani hapo hapatoshi! Yaani we acha tu!







All the contents on this site are copyrighted ©.