2014-01-15 07:55:07

Biashara haramu ya watoto yashamiri nchini DRC!


Padre Henri de la Kethule hivi karibuni ameiomba Serikali ya DRC pamoja na wadau wengine kuhakikisha kwamba, wanakomesha biashara haramu ya watoto inayoendelea kushamiri katika miji ya Kikwit na Kinshasa nchini DRC. Kwa zaidi ya miezi tisa sasa biashara haramu ya watoto imeendelea kufanywa na baadhi ya watu wenye uchu wa mali na utajiri wa haraka haraka katika mkoa wa Bandundu. RealAudioMP3

Padre Henri de la Kethule ameyasema hayo wakati alipokuwa anazungumza na Radio Okap kwa kukazia kwamba, kuna baadhi ya watu wanatumia mgongo wake kutokana na huduma anayoitoa kwa ajili ya watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi kupata watoto ambao baadaye wanawatumbukiza katika biashara haramu ya watoto, jambo ambalo linakwenda kinyume kabisa cha haki msingi za binadamu, uhuru na ustawi wa watoto hao kwa siku za usoni.

Baadhi ya watu hao wanawalaghai wazazi wa watoto wanaoishi katika hali ya umaskini kuwapatia watoto wao ili waweze kuwatunza na kuwawezesha kupata kesho iliyo bora zaidi mjini Kinshasa, kumbe, lengo ni kutaka kuwauza kwenye soko la biashara haramu ya binadamu ambalo kwa sasa linashika kasi ya ajabu mjini Kinshasa anasema Padre Henri de la Kethule.

Wazazi wengi wanadhani kwamba, watoto wao watapelekwa na kutunzwa kwenye nyumba za watoto yatima, kumbe, ukweli wa mambo ni kwamba wanauzwa kama bidhaa mjini Kinshasa. Padre Henri anawataka viongozi wa Serikali na wadau mbali mbali kusimama kidete kusitisha biashara ya binadamu nchini DRC, kabla hawajachelewa!








All the contents on this site are copyrighted ©.