2014-01-14 07:56:10

Mkakati wa Makanisa ya Kiluteri katika kulinda na kutunza mazingira!


Shirikisho la Makanisa ya Kiluteri Duniani kwa Mwaka 2014 linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kushiriki katika kampeni ya kulinda na kutunza mazingira kama sehemu ya kazi ya uumbaji kwa kufunga walau siku moja kwa kila mwezi, tangu Januari 2014 hadi Mwezi Desemba, 2014, wakati ambapo kutaanza mkutano kuhusu Mazingira huko Lima, PerĂ¹. RealAudioMP3
Kwa njia hii, Shirikisho la Makanisa ya Kiluteri Duniani linataka kuwashirikisha waamini wake na watu wote wenye mapenzi mema, kufanya tafakari ya kina kuhusu umuhimu wa utunzaji bora wa mazingira, kama sehemu ya Maandalizi ya Mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu mabadiliko ya tabianchi unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa Mwaka 2014 huko Lima, PerĂ¹.
Viongozi wakuu wa Shirikisho hili wanasema, wameamua kufunga na kusali kila mwezi, kama njia ya kuonesha mshikamano wao na waathirika wa mabadiliko ya tabianchi sehemu mbali mbali za dunia. Kuna mamillioni ya watu wameathirika kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi sehemu mbali mbali za dunia. Hii itakuwa ni nafasi pia kwa ajili ya kuwakumbuka wanaofariki dunia kutokana na majanga asilia.
Lengo kuu ni kujaribu kuwaunganisha waamini na watu wenye mapenzi mema ili waweze kujenga hoja ya nguvu ili kusaidia katika mchakato wa kulinda na kutunza mazingira. Kufunga na kusali ni tendo la maisha ya kiroho, lakini lina faida yake hata katika maisha ya kawaida. Uamuzi huu ulifikiwa hapo tarehe 18 Desemba 2013. Siku ya kwanza ya mfungo na sala, ilikuwa ni hapo tarehe Mosi, Januari 2014.
Kufunga na kusali ni kuwashirikisha wengine tunu msingi za maisha ya kiroho. Ni changamoto ya kufanya magezu katika mitindo ya maisha kwa kusoma alama za nyakati. Kwa mwamini ni fursa ya kufanya toba na kuomba msamaha wa dhambi; tayari kuwajibika barabara katika kulinda na kutunza mazingira kwa ajili ya mafao ya wengi.
Athari za mabadiliko ya tabianchi ni changamoto ambayo inaendelea kufanyiwa kazi na Shirikisho la Makanisa ya Kiluteri Duniani na ni sehemu ya mkakati wake wa shughuli za kichungaji kuanzia Mwaka 2012 hadi Mwaka 2017. Lengo ni kujitahidi kupata haki ya tabianchi sanjari na utunzaji bora wa mazingira, kwa ajili ya kizazi hiki na kile kijacho, ili watu waweze kuwa na afya njema.







All the contents on this site are copyrighted ©.