2014-01-14 08:39:41

Mabalozi na wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa wanaunga mkono jitihada za Papa Francisko katika kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu!


Jumuiya ya Kimataifa inakabiliana na changamoto kubwa kutokana na ongezeko la watu wanaokabiliana na baa la njaa duniani, wahamiaji na wakimbizi wanaotafuta usalama na ubora wa maisha; biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo; nyanyaso na madhulumu dhidi ya Wakristo sehemu mbali mbali za dunia. Wanadiplomasia wanakubaliana kimsingi na changamoto hii inayoendelea kutolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika utume na maisha ya Kanisa.

Hayo yamesemwa na Balozi Jean-Claude Michel, Dekano wa Mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao mjini Vatican wakati alipokuwa anatoa salam za matashi mema kwa Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican, Jumatatu tarehe 13 Januari 2014 wakati Mabalozi walipokutana na Baba Mtakatifu Francisko.

Mabalozi wanampongeza Baba Mtakatifu kwa kuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi mambo yote yanayotaka kufisha utu na heshima ya binadamu katika medani mbali mbali za maisha. Mabalozi wameahidi kwamba, watafikisha kilio cha Baba Mtakatifu Francisko kwa Serikali zao, ili kukifanyia kazi kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi, utu na heshima ya binadamu vikipewa kipaumbele cha kwanza.

Balozi Jean- Claude Michel amegusia vita na kinzani za kijamii zinazotokana na misimamo mikali ya kidini na hali ya kutovuliana; mambo ambayo yameendelea kusababisha majanga makubwa kwa maisha ya watu sehemu mbali mbali za dunia. Anasema, Waraka wa kitume wa Baba Mtakatifu Francisko Injili ya Furaha, Evangelii Gaudium ni muhimu sana katika mchakato wa majadiliano ya kidini miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali, ili kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na upatanisho wa kweli.

Balozi Michel anasema, majanga asilia yaliyojitokeza sehemu mbali mbali za dunia kwa kiasi kikubwa yanachangiwa na binadamu mwenyewe kwa kutopea katika ubinafsi; kwa kutozingatia misingi ya amani, haki na usawa ndani ya Jamii. Baadhi ya watu wameelemewa mno na uchu wa mali, hali ambayo imeendelea kusababisha vita, kinzani na uharibifu mkubwa wa mazingira. Kuna mamillioni ya watu wanaolazimika kuzikimbia nchi zao kutokana na sababu mbali mbali, hawa nao wanapaswa kuhudumiwa kikamilifu.

Mabalozi na wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa mjini Vatican ameahidi kuunga mkono jitihada za Baba Mtakatifu Francisko katika mchakato unaopania kuifanya dunia kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi; kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; uhuru wa kidini. Uhusiano wa Vatican na Jumuiya ya Kimataifa umekuwa na manufaa makubwa kwa ajili ya mafao ya wengi. Mwaka 2015, Vatican itakuwa inasherehekea Jubilee ya Miaka 50 tangu ilipoanzisha uhusiano wa Kidiplomasia na Umoja wa Mataifa.







All the contents on this site are copyrighted ©.