2014-01-13 08:24:01

Wazazi wana dhamana na wajibu wa kurithisha imani kwa watoto wao!


Katika Sherehe ya Ubatizo wa Bwana inayofunga rasmi Kipindi cha Noeli, Baba Mtakatifu Francisko alitoa Sakramenti ya Ubatizo kwa watoto 32: kati yao kuna wasichana 18 na wavulana 14. Ibada hii ya Misa takatifu imeadhimishwa kwenye Kikanisa cha Sistina, kilichopo mjini Vatican.

Baba Mtakatifu katika mahubiri yake anasema kwamba, Yesu hakuwa na sababu msingi za kubatizwa na Yohane Mbatizaji, lakini kutokana na Umungu wake, aliweza kuyatakatifuza maji yote kiasi kwamba, yanaweza kutumika kwa Sakramenti ya Ubatizo. Tangu wakati huo, Sakramenti ya Ubatizo imeendelea kutolewa na Mama Kanisa kwa watoto wake wanaozaliwa kwa Maji na Roho Mtakatifu. Watoto hawa waliobatizwa watakuwa na dhamana ya kurithisha imani ya Kikristo kwa watoto wao katika siku za usoni.

Baba Mtakatifu Francisko amekazia kwamba, wazazi na walezi wanalo jukumu nyeti la kuhakikisha kwamba, wanarithisha imani ya Kikristo kwa watoto wao. Huu ndio urithi mkubwa wanaoweza kuwaachia watoto wao hapa duniani. Watoto hawa kwa sauti na kilio chao wanamwinulia Mungu wimbo wa sifa na shukrani. Baba Mtakatifu amewataka akina mama kuwanyonyesha watoto wao bila woga wowote kwani katika tukio hili wao ndio wahusika wakuu.







All the contents on this site are copyrighted ©.