2014-01-13 15:22:45

Vatican itaendelea kushirikiana na wadau mbali mbali katika ujenzi wa udugu na upendo kati ya watu kiini cha maridhiano na amani!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 13 Januari 2014 amekutana na kuzungumza na Mabalozi pamoja na wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa mjini Vatican kwa kuwatakia kheri na baraka kwa Mwaka mpya wa 2014. Amekumbuka kwa namna ya pekee Hayati Balozi Alejandro Valladares Lanza, aliyekuwa dekano wa Mabalozi kwa miaka mingi, aliyefariki dunia hivi karibuni.

Baba Mtakatifu anasema, mwaka 2013 umesheheni matukio makubwa katika maisha na utume wa Kanisa. Katika masuala ya Kidplomasia Vatican imefanya mikataba ya uhusiano wa kimataifa na nchi kama: Sudan ya Kusini, Cape Verde, Hungari, Chad pamoja na kuridhia mkataba na nchi ya Guinea Equatorial, kunako mwaka 2012. Vatican inaendelea kuwa na wawakilishi katika Mashirikisho ya Kimataifa huko Amerika ya Kusini, Asia na Barani Afrika, hususan katika Jumuiya ya Uchumi kwa Nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS.

Baba Mtakatifu anasema, udugu kama msingi na njia ya amani ni changamoto inayopata chimbuko lake tangu mtu anapozaliwa tumboni mwa mama yake, kimsingi, dhana hii ya upendo inapaswa kujidhihirisha katika moyo wa huduma ili kujenga na kuimarisha amani bila ubaguzi, kila mtu akijitahidi kutekeleza wajibu wake, kwani familia ndio kiini na msingi wa amani. Lakini familia nazo zinaendelea kukabiliana na hali ngumu kiasi hata cha kukosa mahitaji msingi, jambo linalohitaji sera makini zitakazosaidia kuimarisha misingi bora ya kifamilia.

Baba Mtakatifu anasema, vijana na wazee ni tumaini la Jamii kwani wao ni hazina ya hekima na mang'amuzi ya maisha na vijana wanao mwelekeo wa maisha kwa siku za usoni. Kuna haja ya kuwekeza kwa vijana ili waendelee kuwa na matumaini kwa kesho iliyo bora zaidi. Baba Mtakatifu anasema, ameyaona matumaini ya vijana wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani huko Rio de Janeiro. Vijana walisali na kuonesha ari na mwamko wa kukumbatia maisha kwa kuendelea kushirikiana na vijana wenzao, changamoto ya kujenga utamaduni wa kukutana, ili kuimarisha umoja, furaha pamoja na kudumisha amani.

Baba Mtakatifu anasema, Mwaka uliopita ulisheheni matukio yanayokumbatia utamaduni wa kifo, unaojidhihirisha katika: ubinafsi, chuki na uhasama; uchu wa mali na madaraka. Inaonekana kana kwamba, hali hii limekuwa ni jambo la kudumu. Kwa Wakristo, Noeli ni siku kuu ya kuzaliwa kwa Mfalme wa amani anayegeuza ubafsi kuwa ni sehemu ya majitoleo binafsi na kisasi kugeuzwa kuwa ni kielelezo cha msamaha.

Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, Mwaka 2014 utakuwa ni Mwaka wa amani na Syria ambayo anaendelea kuipatia kipaumbele cha pekee kwa sala na kufunga itaonja tena amani na utulivu. Anawashukuru wote wanaounga mkono juhudi za kutafuta amani nchini Syria na kwamba, tarehe 22 Januari 2014 utakuwa ni mwanzo wa mchakato wa upatanisho; kwa kuheshimu na kuthamini haki msingi za binadamu na kwamba, raia wasiokuwa na hatia wataendelea kulindwa. Baba Mtakatifu anatoa mwaliko kwa Jumuiya ya Kimataifa kuendelea kutoa msaada wa kibinadamu kwa wananchi wa Syria na nchi jirani kama vile Lebanon na Jordan zinazotoa msaada kwa wakimbizi na wahamiaji kutoka Syria.

Katika hotuba yake, Baba Mtakatifu ameonesha wasi wasi kuhusu hali ya kisiasa na kijamii nchini Lebanon jambo linaloweza kuhatarisha amani na utulivu huko Mashariki ya Kati. Kuna haja ya kuwa na makubaliano ya kisiasa na kijamii nchini Misri na huko Iraq watu wakijikite zaidi katika kudumisha utulivu na amani. Papa ameridhika na hatua iliyofikiwa katika majadiliano kuhusu silaha za nyuklia kati ya Iran na Kundi la Nchi 5 kujumlisha Moja. Kuna umuhimu wa kujenga na kudumisha utamaduni wa majadiliano yanayoongozwa na nguvu ya kimaadili na haki badala ya kukimbilia matumizi ya mtutu wa bunduki.

Baba Mtakatifu anasema, Jumuiya ya Kimataifa Mwaka huu inaadhimisha Kumbu kumbu ya Miaka 100 tangu ilipotokea Vita kuu ya Kwanza ya Dunia, changamoto ya kulinda na kuheshimu utu kwa kuthamini hata tofauti zinazojitokeza kati ya watu. Majadiliano ya amani kati ya Israeli na Palestina hayana budi kuendelezwa kwa mchango wa Jumuiya ya Kimataifa ili kupata suluhu na amani ya kudumu.

Bado inasikitisha kuona kwamba, kuna Wakristo wanaokimbia kutoka Mashariki ya Kati na Afrika ya Kaskazini. Hawa ni watu wanaopaswa kushiriki katika ujenzi wa nchi zao katika medani mbali mbali za maisha, kwa kutafuta daima mafao ya wengi, haki, amani na upatanisho wa kitaifa.

Baba Mtakatifu anasema, Wakristo katika baadhi ya nchi wanalazimika kutolea ushuhuda wa upendo na huruma ya Mungu, hata pale wanapodhulumiwa na kuteswa katika nchi zao wenyewe, kama inavyojitokeza nchini Nigeria, Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati ambao wanaendelea kukabiliana na utamduni wa kifo. Ni matumaini yake kwamba, Jumuiya ya Kimataifa itawasaidia wakimbizi na hatimaye, kusitisha vita na kinzani katika nchi hizi; tayari kuanza mchakato wa upatanisho, haki na amani kati ya wananchi wote. Upatanisho na amani ni mambo ambayo yanapaswa kupewa kipaumbele hata katika Nchi nyingine za Kiafrika; hususan, Mali na Sudan ya Kusini.

Vatican inayo matumaini makubwa kwamba, Jubilee ya uhusiano kati ya Vatican na Korea kitakuwa ni kichocheo upatanisho kwa ajili ya mafao ya wananchi wa Korea katika ujumla wao, kwa ajili ya mafao ya wengi. Kuna haja ya kuendeleza utamaduni wa kuheshimiana, ushirikiano na amani Barani Asia. Misimamo mikali ya kidini haina budi kudhbitiwa na uhuru wa kidini kuheshimiwa na wote. Vatican itaendelea kushirikiana na nchi mbali mbali duniani kwa ajili ya kujenga na kuimarisha mafao ya wengi.

Baba Mtakatifu anasema, bado kuna vita, njaa na magonjwa mambo yanayokuzwa zaidi kutokana na utandawazi wa kutojali shida na mahangaiko ya wengine sanjari na kukumbatia utamaduni wa kifo kwa sera za utoaji mimba na watoto kupelekwa vitani kwa kunyanyaswa na kudhalilishwa utu na heshima yao. Bado kuna kundi kubwa la watoto linalotumbukizwa katika biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo.

Kuna mamillioni ya watu wanaokimbia nchi zao kutokana na majanga asilia na vita hasa kwenye nchi zilizoko kwenye Pembe ya Afrika na Eneo la Maziwa Makuu. Kuna wakimbizi wanaotambulikana kwa namba na wala si katika utu wao! Hali hii inajionesha pia Amerika ya Kusini wanaokimbilia nchini Marekani bila kuwasahau Wahamiaji wanaotoka Afrika wakitafuta maisha bora zaidi Barani Ulaya, lakini wengi wao wanakufa maji hata kabla ya kufika Ulaya, kama inavyojionesha kwenye Visiwa vya Lampedusa, Kusini mwa Italia. Wote hawa ni watu wanaohitaji kuonjeshwa moyo wa ukarimu na mshikamano.

Baba Mtakatifu anasema, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kulinda na kutunza mazingira kama sehemu ya mchakato wa ujenzi wa amani. Baba Mtakatifu anawaalika wakuu wa Jumuiya ya Kimataifa na wadau mbali mbali kuhakikisha kwamba, wanatunga sera makini zitakazolinda na kutunza mazingira. Uharibifu mkubwa wa mazingira umeendelea kuwa ni chanzo kikubwa cha maafa asilia sehemu mbali mbali za dunia.

Baba Mtakatifu anahitimisha hotuba yake kwa Mabalozi na Wawakilishi wa Jumuiya ya Kimataifa kwa kuwakumbusha kwamba, amani inajengwa kila siku ya maisha, kwa kuzingatia haki. Hii ndiyo dhamana inayotekelezwa na Mama Kanisa katika maisha na utume wake, sehemu mbali mbali za dunia kwa kumhudumia mtu mzima: kiroho na kimwili, ili watu wengi zaidi waweze kuonja huruma na upendo wa Mungu. Vatican itaendelea kushirikiana na nchi mbali mbali katika ujenzi wa udugu na upendo kati ya watu, kiini na msingi wa maridhiano na amani kati ya watu!







All the contents on this site are copyrighted ©.