Tambueni uzuri wa imani, ili muweze kushiriki kikamilifu katika Sakramenti za Kanisa
na Maisha ya Kijumuiya!
Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Sherehe ya Ubatizo wa
Bwana, Jumapili tarehe 12 Januari 2014, amemshukuru Mwenyezi Mungu kwa ajili ya watoto
32 waliozaliwa kwa Maji na Roho Mtakatifu, kielelezo cha imani na furaha ya Familia
ya Mungu. Kwa Ubatizo wa Bwana, kwenye Mto Yordani, mbingu na dunia zilifunguka na
kuleta matumaini mapya kwa binadamu.
Ujio wa Mwana wa Mungu hapa duniani ulikuwa
ni mwanzo wa uwepo wa huruma na upendo wa Mungu kwa watu wake, baada ya mbingu kufungwa
kutokana na dhambi na hivyo kuweka kizingiti kati ya binadamu na Muumba wake. Kwa
kuzaliwa kwa Yesu Kristo Mwana wa Mungu, anasema Baba Mtakatifu, mbingu zilifunguka
tena na Mwenyezi Mungu akawapatia binadamu upendo wa kweli na kufungua mbingu, tukio
lililoshuhudiwa na wachungaji kule kondeni mjini Bethlehemu; Mamajusi kutoka Mashariki
ya mbali, Yohane Mbatizaji, Mitume wa Yesu na Mtakatifu Stefano, Shahidi wa kwanza
kuyamimina maisha yake kwa ajili ya Injili.
Baba Mtakatifu anasema, tukio hili
linaweza kuonekana na waamini wengine hata leo huii, ikiwa kama wataukumbatia upendo
wa Mungu, waliokirimiwa kwanza kabisa walipopokea Ubatizo kwa njia ya Roho Mtakatifu.
Yesu kwa kukubali kubatizwa Ubatizo wa toba, alionesha mshikamano wa dhati na wadhambi
waliokuwa wanafanya hija ya toba na wongofu wa ndani.
Kwa njia ya Ubatizo,
Mwenyezi Mungu anamtambulisha Mwanaye Mpendwa Yesu Kristo aliyependezwa naye! Kwa
njia hii Yesu anashiriki kwa ukamilifu ubinadamu na umaskini wake, ili aweze kuwapenda
pasi na ukomo, kiasi cha kuwaita ndugu zake, licha ya mapungufu yao ya kibinadamu.
Pamoja na Yesu, wanafanyika kuwa ni watoto wateule wa Mungu.
Baba Mtakatifu
anasema, huu ni wakati wa huruma ya Mungu, kila mwamini anapaswa kuwa na kiu ya kutaka
kushirikisha udugu na upendo wake kwa wengine, kwa vile anaguswa na mahangaiko pamoja
na shida za jirani zake. Kwa njia hii maisha yanapata ladha na mwelekeo mpya. Anawaalika
waamini kumwomba Bikira Maria ili aweze kuwaombea kwa Mwanaye wa pekee, waweze kumfuasa
Kristo katika njia ya imani na upendo inayofunguliwa mbele yao kwa njia ya Sakramenti
ya Ubatizo.
Mwishoni Baba Mtakatifu Francisko amewakumbuka kwa namna ya pekee,
wazazi na walezi waliobatiza na wale wote watakaowabatiza watoto wao, kuendeleza furaha
ya Ubatizo na kwamba, Sakramenti hii iwasaidie wazazi na walezi kutambua tena uzuri
wa Imani, ili hatimaye, kushiriki kikamilifu katika maisha ya Kisakramenti na kwenye
Jumuiya ya Kikristo.