Jiwekeeni miiko ili kujenga na kulinda maisha yenu ya ndoa na familia!
Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, kwa mara nyingine tena karibu katika kipindi
chetu pendevu cha Kanisa la nyumbani. Lengo letu: tunataka kuunganisha nguvu za pamoja
katika kuzijenga na kuzichunga familia zetu vema, familia ambazo ni Kanisa la nyumbani.
Kanisa linataka
familia zetu ziwe shule, shule ya upendo, shule ya utii, shule ya uaminifu, shule
ya sala, na hata shule ya kazi, na shule ya fadhila nyingi. Kumbe sote tusaidiane,
kuandaa mazingira ya familia ili kweli yawe ya mwanadamu kufunzwa na kujifunza tunu
mbalimbali za utu wema. Kutoka humo, mwanadamu aandaliwe kuwa tunu kwa Kanisa na kwa
taifa na kwa familia nzima ya mwanadamu.
Katika kipindi kilichopita tuliangazia
Nyanja tatu za maandalizi ya kuupokea wito wa ndoa na kujenga Kanisa la nyumbani,
yaani familia. Kabla hatujaangazia ushiriki wa jamii katika maandalizi hayo; kwanza
tukazie maarifa kwa waoanaji wenyewe. Baada ya kufanya kila aina ya maandalizi; kwa
hakika wanajua kabisa kwamba wanaingia katika maisha mapya, yenye majukumu mapya tena
mazito.
La muhimu kabisa hapa ni kutunza hadhi na heshima ya maisha ya ndoa
na familia. Ili hilo liweze kutimizwa vema, wajifunze sasa kujiwekea miiko. Miiko
hapa, tuelewe kama makatazo binafsi na mipaka unayojiwekea mwenyewe ili usilete harufu
mbaya au ukakasi katika mahusiano ya ndani ya ndoa. Miiko hiyo ipo mingi sana. Kwetu
sisi, tuitazame WALAO MITANO.
Mosi, MWIKO WA MAHUSIANO: Ndugu, wewe sasa umekuwa
mke wa mtu au mume wa mtu; angalia sana aina ya watu unaohusiana nao. Maisha ya ndoa
ni maisha ya watu wakomavu tu. Ukomavu huo uonekane pia katika kudhibiti mahusiano
yako na watu. Kuna watu ambao walikuwa marafiki zako zetu kabla hatujaingia katika
agano, mlikuwa mnashinda pamoja, mnakula na kunywa siku nzima hadi asubuhi.
Wewe
ni mtu wa ndoa sasa; KUNA BAADHI YA MARAFIKI ITABIDI UWASADAKE TU, weka umbali nao
au uwaache kabisa.. Wapo wengine wanaofaa sana, lakini wengine hawafai, watakuharibia
ndoa yako; kwa maneno yao na matendo yao. LA MSINGI NI KWAMBA UNAHUSIANA NA NANI,
KWA NINI NA HADI WAPI. Wewe ni mume wa mtu! Sasa unajisahau, kila wakati upo na wasichana
wengine mnakula na kunywa, unamwacha mwenzio kulinda nyumba. Au eti kila siku upo
kazini hadi saa za usiku, na ukitoka huko, unapitiliza kwenda bar kupoteza mawazo;
unarudi nyumbani ukiwa hauna mawazo tena. Yote yamepotelea bar. Hapo hautajenga Kanisa
la Nyumbani.
Pili , MWIKO WA MAZINGIRA: Mtu wa ndoa, tunza heshima yako. Usipende
kuwa kila mahali. Kuna mazingira mengine ile kuonekana tu; tayari utaleta mashaka
ya lazima; hata kama hujafanya kosa, kuonekana tu hapo ni tatizo. Wewe kila siku upo
vijiweni baba, unafanya nini? Mama, kila siku uko nyumba za waganga wa vienyeji; au
unaonekana ukitoka kwenye nyumba za wageni. Hutawasadikisha watu wote kwamba ulikwenda
kumsalimu mjomba. Mazingira tu, yanatia wasiwasi. JILINDE!!
Tatu, MWIKO WA
MAVAZI: Jambo hili litazamwe kwa hekima yote. Siku hizi kunajengeka utamaduni wa kutopenda
nguo. Kuna vijivazi vifupi au vinavyobana sana. Hizi fasheni zisituibie utu na heshima
yetu. Wewe ni mke wa mtu sasa, kuna mavazi mengine hayakufai kabisa kuvaa hadharani.
Utaalika dharau au utaalika wahuni wafikiri kwamba na wewe bado ni mmoja wao.
Baba
wa familia, mume wa mtu kabisa , amening’iniza suruali nusu mlingoti, utadhani anajiandaa
kuchomwa sindano; hapana!! Mavazi huweza kupendekeza tabia ya mtu. Usikubali jamii
ikakuweka katika kundi ambalo halikuhusu kwa kuwa mzembe katika mavazi.
Nne,
MWIKO WA VYAKULA NA VINYWAJI: Leo hii katika utaratibu wetu wa soko huria katika ulimwengu
wa watu ambao wanajali zaidi pesa kuliko uhai na utu wa watu; tuwe macho, vyakula
vingi havifai na vipo ambavyo vinaharibu kabisa hata miundombinu ya ndoa na familia.
Hili tutalifafanua kitaalamu kwa wakati wake. Lakini tuseme pia juu ya kiasi katika
matumizi ya pombe. Kwa ujumla wake, ULEVI NI SUMU KUBWA KATIKA NDOA. Ndoa za walevi
hazina amani hata siku mmoja. Baba akilewa anarudi na MATUSI, KELELE NA KUWA MKOROFI
TU, watoto wanasikia na wanaona. Mama naye akirudi amelewa, NI KELELE NA MATUSI YA
KILA AINA.
Mwisho ulevi unawapelekea kwenye madeni makubwa, baadaye madeni
yanawafanya wauze hata vitu vya familia, na huku familia itaendelea kuteseka. JE HADI
HAPO ULEVI UNA THAMANI GANI? Ndugu, CHA MUHIMU NI KWAMBA USITAMADUNISHE ULEVI. Wanaume
wasome YBS. 19:1-3.
Tano, MWIKO WA MAWASILIANO: Ndugu wewe ni mke wa mtu au
mume wa mtu; yakupasa kuwa mwangalifu na watu unaowasiliana nao, iwe ana kwa ana au
kwa kutumia vyombo vya mawasiliano hasa SIMU. Usipende kuwasiliana na kila mtu, hata
pasipo sababu za msingi. NDOA ZA WATU WENGI ZIMEJERUHIWA KWA SABABU YA SIMU. Usipowadhibiti
rafiki zako juu ya mawasiliano, wataandika UJUMBE WENYE MATATA utakaoleta fujo katika
ndoa yako. Sio lazima kila mtu awe na namba yako ya simu.
Na sio lazima uwepo
katika mitandao yoote na kijamii. Sio busara sana kupenda kupiga picha na kila mtu
au kupigwapigwa picha kila mahali na kila mtu. Wewe hujawa maua! Ipo siku picha hizo
zitaning’inizwa katika mitandao na safari ya ndoa yenu itachechemea tu. Wengi siku
hizi tumepoteza dhamiri ya uadilifu, hatuoni haya kuwaharibia wengine maisha.
Mpendwa
msikilizaji, mambo haya tutayaangazia tena tutakapohekimishana juu ya ushiriki wa
jamii katika maandalizi na katika kuifanya ndoa changa ianze kwa mwondoko unaostahili.
Sote kama jumuiya tunawajibika kulijenga Kanisa la nyumbani.
Kwa leo tunaishia
hapa; hadi kipindi kijacho, kutoka katika Studio za Radio Vatican, ni Mimi Padre Pambo
Martin Mkorwe OSB.