2014-01-13 09:35:27

Hata Makanisa maskini na machanga yanayo uwezo wa kuchangia katika maisha na utume wa Kanisa la kiulimwengu


Padre Federico Lombardi Msemaji mkuu wa Vatican akifafanua kuhusu uteuzi wa Makardinali wapya uliofanywa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili iliyopita, tarehe 12 Januari 2014 anasema kwamba, Papa Francisko ameendelea kufuata sheria ya kuwa na Makardinali 120 walio chini ya miaka 80 wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura wakati wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Baba Mtakatifu ameamua kuteuwa Makardinali 16 wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura. Kati ya Makardinali wateule, 4 ni wale wanotekeleza dhamana na utume wao mjini Vatican. Makardinali wengine 12 ni Maaskofu wakuu wanaoishi katika Majimbo yao sehemu mbali mbali za dunia. Kimsingi, Baba Mtakatifu ameteuwa Makardinali 2 kutoka Ulaya; Amerika ya Kaskazini na Kati ni Makardinali 3, Amerika ya Kusini walioteuliwa ni Makardinali 3. Bara la Afrika limepata Makardinali wapya 3, hali kadhalika na Bara la Asia limepata Makardinali 2.

Baba Mtakatifu Francisko kwa kuamua kuwateuwa Maaskofu wakuu: Phillippe Nakellentuba Ouèdraogo kutoka Jimbo kuu la Ouagadougou, Bukrina Faso na Askofu Chibly Langlois, Jimbo la Les Cayes, Haiti anaonesha upendeleo wa pekee kwa Makanisa maskini, ambayo hata katika umaskini wao, bado yanaweza kuchangia katika maisha na utume wa Kanisa la Kiulimwengu. Hawa ni Makardinali wanaopaswa kuwa mabalozi wema katika mapambano dhidi ya umaskini, ujinga na maradhi.

Baba Mtakatifu ameamua pia kuteuwa Makardinali katika Majimbo ambayo kimsingi si Majimbo ya Kikardinali, kama ilivyotokea kwa Jimbo kuu la Perugia, Italia na Kisiwa cha Mindanao nchini Ufilippini. Kati ya Makardinali wateule, wenye sifa ya pekee licha ya kuwa na umri mkubwa ni Askofu mkuu mstaafu Loris Francesco Capovilla, mwenye umri wa miaka 98, ambaye alikuwa ni Katibu muhtasi wa Papa Yohane wa XXIII, anayetarajiwa kutangazwa kuwa Mtakatifu, kama sehemu ya Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Padre Federico Lombardi anasema, Makardinali wapya ambaye ni kijana kuliko wote ana umri wa miaka 55 ambaye ni Askofu Chilby Langlois kutoka Jimbo la Les Cayes, Haiti. Na Kardinali mzee kuliko wote ni Askofu mkuu mstaafu Loris Francesco Capovilla, mwenye umri wa miaka 98.







All the contents on this site are copyrighted ©.