2014-01-11 08:39:50

Unafiki ni sumu ya miito mitakatifu!


Askofu Nunzio Galantino, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, CEI anaendelea kuhimiza umuhimu wa sala katika kulea na kukuza miito mitakatifu ndani ya Kanisa. Huu ndio mwelekeo mpya unaotolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika kuhamasisha miito mitakatifu ndani ya Kanisa, jambo ambalo linapaswa kuvaliwa njuga na idara za kichungaji. RealAudioMP3

Hivi karibuni, Baraza la Maaskofu Katoliki Italia liliendesha kongamano la miito mitakatifu lililokuwa linaongozwa na kauli mbiu “Jiweke wazi katika ukweli, utakuwa na maisha. Miito ni ushuhuda wa maisha”. Mikakati ya kichungaji kuhusiana na miito haina budi kutoa kipaumbele cha kwanza katika maisha ya sala, kwani bila sala kazi yote ya kuhamasisha miito ni bure! Ni sawa na “kumpigia mbuzi gitaa ukimtegemea aserebuke” anasema, Askofu Nunzio Galantino.

Sala na ushuhuda wa maisha ni chanda na pete, kwani haya ni mambo yanayotegemeana. Mapadre na watawa wawe ni mifano bora ya kuigwa katika maisha na matendo yao, ili vijana wanapowaona waweze kuvutika kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani zao kwa njia ya Kanisa. Ushuhuda huu ujikite katika ile furaha inayobubujika kutoka katika undani wa maisha ya Padre au mtawa, kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko.

Kwa njia hii, Kanisa litaweza kuwapata Mapadre na Watawa ambao si wafanyakazi wa mshahara, watu wanaojitafuta wenyewe kwa ajili ya masilahi yao binafsi, bali ni watu wanaomwamini Yesu Kristo, kiasi cha kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Mapadre na watawa katika ushuhuda wa maisha yao wawe ni watu wanaopenda na kusimamia ukweli. Maisha yao yawe ni kielelezo cha ushuhuda wa ukweli wanaoufundisha, kuutangaza na kuumwilisha katika vipaumbele vya maisha yao ya kila siku. Unafiki ni sumu ya miito mitakatifu.

Kwa upande wake, Monsinyo Nico Dal Molin, mkurugenzi wa Idara ya miito, Baraza la Maaskofu Katoliki Italia anasema kwamba, kuna haja ya kutangaza na kushuhudia ukweli katika ulimwengu mamboleo ambamo watu wanapendelea kujikita katika “umbea” ambao kimsingi si mtaji na mambo yasiokuwa na mashiko wala mafao ya wengi. Watu wajifunze kutafuta ukweli, kuzingatia umuhimu wa maisha na kwamba, ukweli hauna mjadala, daima una gharama ambayo inapaswa kulipwa!

Dunia inahitaji mashahahidi wanaoshuhudia ukweli na uwazi; mambo msingi yanayobubujika kutoka katika undani wa mtu mwenyewe! Kwa kupenda na kuthamini ukweli, kuna maanisha ya kuwa ni watoto wa mwanga wanaotembea katika Mwanga wa ukweli ambao ni Yesu Kristo mwenyewe. Ni watu wanaofahamu na kuthamini upendo, tayari kuwashirikisha wengine. Kwa njia hii waamini wanaweza kuwa ni mwanga wa mataifa unaofukuza giza la ubaya na dhambi.







All the contents on this site are copyrighted ©.